Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwatia Watoto Nidhamu

Kuwatia Watoto Nidhamu

Siri ya Furaha ya Familia

Kuwatia Watoto Nidhamu

John: * Kabla ya kuniadhibu kwa sababu ya kosa nililofanya, wazazi wangu walijitahidi sana kuelewa nia yangu na hali zilizohusika. Mimi ninajaribu kuwaiga ninapowarekebisha binti zangu. Mke wangu, Alison, alilelewa kwa njia tofauti. Baba na mama yake waliwaadhibu mara tu walipokosea. Ni kana kwamba waliwachapa watoto wao bila kufikiria hali zilizohusika. Nyakati nyingine ninahisi kwamba mke wangu anawaadhibu watoto wetu kwa ukali kama wazazi wake.

Carol: Baba aliiacha familia yetu nilipokuwa na umri wa miaka mitano tu. Hakujishughulisha nami wala na dada zangu watatu. Mama alifanya kazi kwa bidii ili kutuandalia mahitaji yetu, nami nilikuwa na majukumu mengi ya kuwatunza dada zangu. Ilikuwa vigumu kufurahia maisha ya utotoni huku nikitimiza majukumu ya mzazi. Hadi leo, mimi ninachukua mambo kwa uzito sana na sipendi mzaha. Ninapohitaji kuwaadhibu watoto wangu, mimi ninafikiria sana kuhusu makosa yao. Ninapenda kujua kwa nini walifanya kosa hilo na walikuwa wakifikiria nini. Kwa kutofautisha, mume wangu, Mark, huwa hafikirii sana jambo lililotukia. Alilelewa na baba mwenye upendo lakini thabiti ambaye alimtunza sana mama ya Mark. Wasichana wetu wanapokosea mume wangu anasuluhisha upesi matatizo. Anachanganua hali, anaishughulikia, na haifikirii tena.

KAMA maneno ya John na Carol yanavyoonyesha, malezi yako yanaweza kuamua sana jinsi utakavyowatia nidhamu watoto wako. Malezi ya mume na mke yanapotofautiana, huenda watakuwa na maoni tofauti sana kuhusu jinsi ya kuwazoeza watoto. Nyakati nyingine, tofauti hizo zinaweza kusababisha matatizo katika ndoa.

Uchovu unaweza kuzidisha matatizo hayo. Wazazi ambao wamepata mtoto wao wa kwanza wanagundua kwamba kumzoeza mtoto ni kazi inayochosha, na inayochukua muda mwingi. Joan pamoja na mume wake, Darren, wamewalea wasichana wao wawili. Joan anasema hivi: “Ninawapenda wasichana wangu, lakini mara nyingi hawakupenda kwenda kulala wakati nilipowaambia wakalale. Waliamka wakati walipopaswa kuwa wamelala. Walinikatiza nilipotaka kuzungumza. Hawakurudisha viatu, mavazi, na vitu vyao vya kuchezea mahali panapofaa, na waliacha chakula bila kukifunika.”

Jack, ambaye mke wake alishuka moyo baada ya kujifungua mtoto wao wa pili, anasema hivi: “Mara nyingi ningetoka kazini na kurudi nyumbani nikiwa nimechoka kisha ningemtunza mtoto wetu mdogo karibu usiku wote. Hilo lilifanya iwe vigumu kumtia nidhamu kwa ukawaida binti yetu mkubwa. Alimwonea wivu dada yake mdogo kwa sababu aliona kwamba tunamkazia sana fikira.”

Wazazi waliochoka wanapobishana juu ya kumzoeza mtoto, mabishano hayo yanaweza kusababisha magombano makali. Hali ya kutoelewana inaweza kuwatenganisha wazazi na kumfanya mtoto awagonganishe. Ni kanuni gani za Biblia zitakazowasaidia wenzi wa ndoa kudumisha uhusiano wa karibu wanapowazoeza watoto wao kwa njia inayofaa?

Tenga Wakati kwa Ajili ya Mwenzi Wako

Ndoa inapaswa kuwepo kabla ya watoto kuzaliwa, na inakusudiwa iendelee muda mrefu baada ya watoto kuondoka nyumbani. Biblia inasema hivi kuhusu ndoa: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:6) Kwa kutofautisha, simulizi hilohilo linaonyesha Mungu alikusudia kwamba mwishowe mtoto “atamwacha baba yake na mama yake.” (Mathayo 19:5) Hivyo, kuwalea watoto ni sehemu fulani tu ya ndoa, si msingi wa ndoa. Kwa kweli, wazazi wanapaswa kutumia wakati mwingi kuwazoeza watoto wao, lakini wanapaswa pia kukumbuka kwamba msingi bora wa kufanya hivyo ni kuwa na ndoa imara.

Ni njia gani moja ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kudumisha uhusiano wao ukiwa imara wanapowalea watoto? Ikiwezekana, tengeni wakati wa kuwa peke yenu kwa ukawaida bila watoto. Kufanya hivyo kutawasaidia mzungumzie masuala muhimu ya familia na kufurahia kuwa pamoja. Ni kweli kwamba si rahisi kutenga wakati wa kuwa na mwenzi wako. Alison, mama aliyetajwa mapema, anasema, “Wakati tu mimi na mume wangu tunapopata wakati wa kuwa pamoja, binti yetu mdogo anataka kupewa uangalifu au binti yetu mwenye umri wa miaka sita analia kwa sababu kalamu zake zimepotea.”

Joan na Darren, waliotajwa mapema, walitenga wakati wa kuwa pamoja kwa kuhakikisha kwamba kufikia saa fulani binti zao watakuwa wamelala. Joan anasema: “Sikuzote binti zetu walipaswa kuwa wamelala kufikia saa fulani hususa. Hilo lilinipa mimi na Darren wakati wa kutulia na kuzungumza.”

Kwa kuwawekea watoto wakati hususa wa kulala, wazazi hawatakuwa tu na wakati wa kuwa pamoja bali pia watamsaidia mtoto “asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” (Waroma 12:3) Mwishowe, watoto waliozoezwa kuheshimu wakati wa kulala wanatambua kwamba wao ni sehemu muhimu ya familia lakini wao si sehemu pekee ya familia, hivyo, lazima wafuate ratiba ya familia badala ya kutazamia ratiba ya familia ibadilishwe kulingana na mapendezi yao.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Wawekee watoto wakati hususa wa kulala na uhakikishe unafuatwa kila siku. Mtoto wako akitoa sababu ya kutolala kama vile kwa sababu anataka maji, kubali ombi hilo moja tu. Lakini usimruhusu mtoto aahirishe wakati wake wa kulala kwa kutoa visababu vingine vingi. Mtoto wako akiomba akae macho kwa dakika nyingine tano na unataka kumruhusu, pima wakati huo kwa saa yenye kengele. Kengele inapolia, hakikisha kwamba mtoto analala bila kumruhusu atoe visababu vingine. Acha ‘Ndiyo yako imaanishe Ndiyo, Siyo yako, Siyo.”—Mathayo 5:37.

Onyesheni Kuwa Mna Muungano

“Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako,” inasema methali moja yenye hekima. (Methali 1:8) Mstari huo unaonyesha kwamba baba na mama wana haki ya kuwawekea watoto wao sheria. Hata hivyo, hata wenzi wa ndoa wenye malezi yaleyale, wanaweza kubishana juu ya kuwatia watoto wao nidhamu na jinsi sheria za familia zinavyopaswa kufuatwa katika hali fulani. Wazazi wanaweza kushughulikia tatizo hilo jinsi gani?

John, aliyetajwa mapema, anasema, “Ninahisi kwamba ni muhimu kutobishana mbele ya watoto.” Hata hivyo, anakubali kwamba si rahisi kuonyesha kwamba wazazi wana muungano. “Watoto huwa makini sana,” anasema John. “Hata ikiwa hatubishani mbele yao, binti yetu anaweza kujua kuna jambo.”

John na Alison wanashughulikia tatizo hilo jinsi gani? Alison anasema: “Hata nisipokubaliana na jinsi mume wangu anavyomtia nidhamu binti yetu, mimi ninasubiri hadi aondoke kabla ya kuzungumzia jambo hilo na mume wangu. Sitaki afikiri kwamba anaweza kutugonganisha kwa kutumia maoni yetu yanayotofautiana. Anapotambua kwamba hatujakubaliana, ninamwambia kuwa kila mshiriki wa familia anapaswa kufuata mpango wa Yehova na kwamba mimi ninajitiisha kwa hiari chini ya ukichwa wa baba yake kama yeye anavyopaswa kujitiisha chini yetu tukiwa wazazi.” (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 6:1-3) John anasema: “Tunapokuwa pamoja kama familia, mimi ndiye ninawatia binti zetu nidhamu. Lakini ikiwa Alison anaelewa hali hiyo vizuri zaidi, ninamwacha awatie nidhamu nami ninamuunga mkono. Ikiwa sikubaliani naye kuhusu jambo fulani, ninalizungumzia baadaye pamoja naye.”

Unaweza kuzuia jinsi gani maoni yanayotofautiana kuhusu kuwazoeza watoto yasitokeze uhasama kati yako na mwenzi wako, na hivyo kuwafanya watoto wasiwaheshimu?

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Tengeni wakati hususa kila juma wa kuzungumzia mambo yanayohusu kuwalea watoto, na mzungumzie waziwazi tofauti zozote mnazoweza kuwa nazo. Jaribu kuelewa maoni ya mwenzi wako na ukubali kwamba mwenzi wako ana uhusiano wa pekee na mtoto.

Boresheni Uhusiano Wenu Mnapowalea Watoto

Bila shaka, kuwazoeza watoto ni kazi ngumu. Nyakati nyingine, jukumu hilo linaweza kunyonya nguvu za mzazi. Hata hivyo, punde si punde, watoto wenu wataondoka nyumbani, nanyi mtabaki mkiwa wawili tena. Je, ndoa yenu itakuwa imeimarishwa au kudhoofishwa na kazi ya kuwalea watoto? Jibu litategemea jinsi mnavyofuata kanuni inayopatikana katika Mhubiri 4:9, 10: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.”

Wazazi wanapofanya kazi pamoja, wanaweza kupata matokeo yenye kuridhisha sana. Carol, aliyenukuliwa mapema, anasema hivi: “Nilijua kwamba mume wangu alikuwa na sifa nyingi nzuri, lakini kuwalea watoto pamoja kumenifanya nione sifa zake nyingine nzuri. Nimemheshimu na kumpenda zaidi kwa sababu nimeona jinsi alivyowatunza binti zetu kwa upendo.” John anasema hivi kumhusu Alison, “Kuona jinsi mke wangu amekuwa mama mwenye upendo kumenifanya nimpende na kumheshimu sana.”

Ukitenga wakati wa kuwa na mwenzi wako na kuwalea watoto wenu pamoja, ndoa yenu itaimarika kadiri watoto wenu wanavyoendelea kuwa watu wazima. Huo ndio mfano mzuri zaidi mnaoweza kuwawekea watoto wenu.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

JIULIZE . . .

▪ Ninatumia muda gani kila juma pamoja na mwenzi wangu bila watoto kuwepo?

▪ Ni jinsi gani ninavyomuunga mkono mwenzi wangu anapowatia nidhamu watoto wetu?