Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, ukoma unaotajwa katika Biblia ni sawa na ukoma wa leo?

Ukoma unaojulikana leo unaambukizwa kupitia bakteria. Bakteria hiyo (Mycobacterium leprae) iligunduliwa na Dakt. G.A. Hansen mnamo 1873. Wachunguzi wamegundua kwamba bakteria hiyo inaweza kuishi nje ya mwili wa mwanadamu katika kamasi kwa siku tisa hivi. Pia wamegundua kwamba watu wanaoshirikiana kwa ukaribu na wagonjwa wa ukoma wana uwezekano mkubwa wa kuambukizwa ugonjwa huo na pia mtu anaweza kuambukizwa na nguo za mtu mwenye ukoma. Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, zaidi ya visa vipya 220,000 vya ukoma viliripotiwa katika mwaka wa 2007.

Hakuna shaka kwamba watu walioishi Mashariki ya Kati katika nyakati za Biblia walipatwa na ukoma, na Sheria ya Musa ilisema kwamba mkoma atengwe na watu wengine. (Mambo ya Walawi 13:4, 5) Hata hivyo, neno la Kiebrania tsa·raʹʽath linalotafsiriwa “ukoma” halikutumiwa tu kwa ukoma uliowapata wanadamu. Tsa·raʹʽath pia ulipata mavazi na nyumba. Aina hiyo ya ukoma ingepatikana katika vitambaa vya sufu au kitani au kitu chochote kilichotengenezwa kwa ngozi. Katika visa fulani, ukoma huo ungeweza kuondolewa kwa kusafisha, lakini ikiwa “pigo la rangi ya kijani-manjano au la rangi nyekundu-nyekundu” lingeendelea, kitambaa au ngozi hiyo ingeteketezwa. (Mambo ya Walawi 13:47-52) Kwenye kuta za nyumba ukoma huo ulionekana kama “mibonyeo ya rangi ya kijani-manjano au ya rangi nyekundu-nyekundu.” Mawe na saruji iliyoathiriwa ingetolewa na kutupwa mbali na makao ya wanadamu. Ikiwa ukoma huo ungerudi, jengo hilo lingebomolewa na vifaa hivyo kutupwa. (Mambo ya Walawi 14:33-45) Watu fulani wanasema kwamba ukoma uliokuwa katika mavazi au nyumba ni kile ambacho leo kinaitwa ukungu au kuvu. Hata hivyo, hilo haliwezi kuthibitishwa.

Kwa nini mahubiri ya mtume Paulo huko Efeso yalitokeza mvurugo kati ya mafundi wa fedha?

Mafundi wa fedha wa Efeso walisitawi kwa kutengeneza “vihekalu vya fedha vya Artemi,” mlinzi wa Efeso, mungu wa kike wa uwindaji, nguvu za uzazi, na kuzaa. (Matendo 19:24) Sanamu yake ilisemekana kuwa ilianguka “kutoka mbinguni” na iliwekwa katika hekalu la Artemi huko Efeso. (Matendo 19:35) Hekalu hilo lilionwa kuwa moja kati ya maajabu saba ya ulimwengu wa kale. Waabudu wengi sana walienda Efeso kila mwaka katika mwezi wa Machi/Aprili (Mwezi wa 3/4) ili kuhudhuria sherehe za kumtukuza Artemi. Wageni hao wengi walifanya sanamu nyingi sana ziuzwe, ambazo zilitumiwa kama zawadi, hirizi, matoleo kwa mungu huyo wa kike, au ili zitumiwe na familia katika ibada. Maandishi ya kale kutoka Efeso yanataja kuhusu utengenezaji wa sanamu za dhahabu na fedha za Artemi, na maandishi mengine yanataja kihususa kuhusu mafundi wa fedha.

Paulo alifundisha kwamba sanamu ‘zilizofanywa kwa mikono si miungu.’ (Matendo 19:26) Hivyo, mafundi wa fedha waliona kwamba biashara yao inahatarishwa na hivyo wakachochea ghasia ili kupinga kazi ya Paulo ya kuhubiri. Demetrio, mmoja wa mafundi hao wa fedha, alieleza wasiwasi wao kwa kusema: “Kuna hatari si kwamba tu kazi hii yetu itapata sifa mbaya bali pia hekalu la Artemi, mungu mkuu wa kike, litaonwa kuwa si kitu na hata utukufu wake ambao wilaya yote ya Asia na dunia inayokaliwa huuabudu utashushwa uwe si kitu hivi karibuni.”—Matendo 19:27.