Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unawezaje Kuwatia Nidhamu Watoto Wako?

Unawezaje Kuwatia Nidhamu Watoto Wako?

“Nilisikiliza kila gari lililopita. Hii ilikuwa mara ya tatu Jordan kushindwa kurudi nyumbani muda tuliokubaliana. Nilijiuliza, ‘Yuko wapi? Je, amepatwa na matatizo? Je, anajua jinsi tunavyohangaika?’ Alipowasili, nilikuwa nimekasirika sana.”GEORGE.

“Binti yangu alipiga mayowe, nikashtuka sana. Nilipogeuka nilimwona ameshika kichwa chake huku akilia. Mdogo wake mwenye umri wa miaka minne alikuwa amempiga vibaya.”—NICOLE.

“‘Sikuiba pete hii. Niliiokota!’ alisema Natalie, binti yetu mwenye umri wa miaka sita, huku akiwa na macho ya huruma. Alipoendelea kukataa tuliumia sana hivi kwamba tukatokwa na machozi. Tulijua alikuwa akidanganya.”—STEPHEN.

IKIWA wewe ni mzazi, je, umewahi kukabili hali zilizotajwa hapo juu? Unapokabili hali hiyo, je, wewe hujiuliza jinsi—au ikiwa—unapaswa kumtia nidhamu mtoto wako? Je, ni vibaya kuwatia nidhamu watoto wako?

NIDHAMU NI NINI?

Katika Biblia, neno “nidhamu” linamaanisha mengi zaidi ya kuadhibu. Nidhamu humaanisha kutoa maagizo, elimu, na marekebisho. Nidhamu haihusiani kamwe na ukatili.Methali 4:1, 2.

Nidhamu inayotolewa na wazazi inaweza kufananishwa na kutunza bustani. Mtunza-bustani hutayarisha udongo, humwagilia maji na kuweka mbolea kwenye mmea, pia huzuia wadudu waharibifu na kuondoa magugu. Kadiri mmea unavyokua, ndivyo mtunza-bustani anavyohitaji kupunguza matawi ili mmea ukue vizuri. Anatambua kwamba kutumia mbinu na ujuzi unaofaa kutamsaidia kuwa na mmea wenye afya. Vivyo hivyo, wazazi huwatunza watoto wao kwa njia mbalimbali. Lakini wakati mwingine wanahitaji kutoa nidhamu—kama tu kupunguza matawi ya mmea, ili kuondoa tabia zisizofaa na kuwasaidia watoto kukua vizuri. Hata hivyo, mtunza-bustani akikata matawi ovyoovyo, mti utadhoofika. Vivyo hivyo, nidhamu inapaswa kutolewa kwa upendo.

Yehova Mungu anawawekea wazazi mfano bora kuhusiana na kutoa nidhamu. Anapowatia nidhamu waabudu wake, wananufaika sana hivi kwamba ‘wanaipenda nidhamu.’ (Methali 12:1) Hivyo, ‘wanashikilia nidhamu’ na ‘hawaiachi iende.’ (Methali 4:13) Unaweza kumsaidia mtoto wako kukubali nidhamu kwa kuiga mambo matatu kuhusu jinsi ambavyo Mungu hutoa nidhamu, yaani, (1) kwa upendo, (2) kwa usawaziko, na (3) kwa uthabiti.

NIDHAMU YENYE UPENDO

Mungu hutoa nidhamu kwa upendo. Biblia inasema hivi: “Yeye ambaye Yehova anampenda, humkaripia, kama vile baba anavyomkaripia mwana anayemfurahia.” (Methali 3:12) Isitoshe, Yehova ni “mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Kwa hiyo, Yehova hatoi nidhamu kwa ukatili. Pia hatumii maneno makali, au kuwakosoa-kosoa waabudu wake, au kuwadharau, mambo ambayo yanaweza kuumiza kama “upanga unaochoma.”Methali 12:18.

SIKILIZA

Kwa kweli, wazazi hawawezi kuiga kikamili mfano mkamilifu wa Mungu wa kujizuia. Nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kuwa na subira, hasa wakati huo inafaa kukumbuka kwamba adhabu inayotolewa kwa hasira hupita kiasi na huwa yenye madhara. Zaidi ya hayo, adhabu inayotolewa kwa hasira au kwa kukata tamaa si nidhamu hata kidogo. Hayo ni matokeo ya kukosa kujidhibiti.

Kwa upande mwingine, ukitoa nidhamu kwa upendo na kwa kujizuia, utapata matokeo mazuri. Fikiria jinsi George na Nicole, wazazi walionukuliwa mwanzoni mwa makala hii walivyofanya.

SALI

“Jordan alipowasili, mke wangu na mimi tulikuwa tumekasirika sana, lakini tulijizuia tulipokuwa tukimsikiliza akijieleza. Kwa sababu ilikuwa usiku sana, tuliamua kujadili jambo hilo asubuhi. Tulisali pamoja na kwenda kulala. Siku iliyofuata, tulikuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kuzungumza na kijana wetu kwa utulivu na kumgusa moyo. Alikubali kutii sheria tulizoweka na akakiri makosa yake. Tuligundua kwamba kama tungesuluhisha jambo hilo haraka-haraka tukiwa na hasira hatungepata matokeo mazuri. Tulipojitahidi kusikiliza kwanza kwa makini matokeo yalikuwa mazuri.”—George.

ZUNGUMZA

“Nilikasirika sana nilipoona jinsi mwanangu alivyokuwa amemjeruhi dadake. Badala ya kumwadhibu papo hapo, nilimwambia aende chumbani kwa sababu nilikuwa na hasira sana na nisingeweza kutoa nidhamu inayofaa. Baadaye, nilipokuwa nimetulia, nilimwambia kwamba ujeuri haufai na kumwonyesha jinsi dada yake alivyokuwa ameumia. Njia hiyo ilimsaidia. Alimwomba msamaha dadake na kumkumbatia.”Nicole.

Kwa kweli, nidhamu inayofaa, hata kama itatia ndani kutoa adhabu, sikuzote inapaswa kuchochewa na upendo.

NIDHAMU YENYE USAWAZIKO

Sikuzote nidhamu ya Yehova hutolewa “kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 30:11; 46:28) Kabla ya kutoa nidhamu Yehova huzingatia mambo yote, kutia ndani sababu ambazo hazionekani wazi. Wazazi wanawezaje kuiga mfano wake? Stephen, aliyetajwa mwanzoni, anasema hivi: “Ingawa tulihisi uchungu na hatukuelewa kwa nini Natalie alikataa kukiri kosa lake, tulijaribu kuzingatia umri na ukomavu wake.”

Robert, mume wa Nicole, pia hujaribu kuzingatia mambo yote yanayohusika. Watoto wanapokosea, yeye hujiuliza hivi: ‘Je, hii ni mara ya kwanza au ni tabia inayoendelea? Je, mtoto amechoka au ni mgonjwa? Je, tabia hii ni dalili ya tatizo lingine?’

Wazazi wenye usawaziko pia huelewa kwamba watoto si watu wazima. Mtume Paulo alitambua jambo hilo alipoandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Robert anasema hivi: “Jambo ambalo hunisaidia nisikasirike kupita kiasi ni kukumbuka jinsi nilivyotenda nilipokuwa na umri kama wa mtoto wangu.”

Inafaa uwe na usawaziko kuhusu yale unayotarajia kutoka kwa mtoto wako, na wakati huohuo, usipuuze tabia mbaya za mtoto wako. Kwa kuzingatia uwezo wa mtoto, upungufu wake, na hali nyingine, utakuwa na hakika kwamba nidhamu utakayotoa itakuwa yenye usawaziko.

KUTOA NIDHAMU KWA UTHABITI

Andiko la Malaki 3:6, linasema hivi: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” Watumishi wa Mungu wanatambua ukweli huo na hivyo kuhisi wako salama. Watoto pia wanahitaji nidhamu thabiti ili wahisi salama. Ikiwa sheria zako zinabadilika-badilika kwa kutegemea hisia zako, huenda mtoto wako akachanganyikiwa na kukata tamaa.

Kumbuka maneno ya Yesu: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” Maneno hayo yanawahusu pia wazazi. (Mathayo 5:37) Fikiria kwa makini kabla ya kutaja adhabu ambayo hukusudii kutekeleza. Ukimwonya mtoto wako kwamba utamtia nidhamu fulani akikosea, hakikisha kwamba unatekeleza nidhamu hiyo.

Mawasiliano mazuri kati ya mzazi na mtoto ni muhimu sana inapohusu nidhamu thabiti. Robert anasema: “Watoto wangu wakinishawishi niwaruhusu kufanya jambo ambalo mama yao aliwakataza, ninapojua kwamba wamekatazwa, mimi hubadili uamuzi wangu ili ufanane na wa mke wangu.” Wazazi wasipokubaliana jinsi ya kutoa nidhamu, inafaa wajadili jambo hilo faraghani na kufikia makubaliano.

NIDHAMU NI MUHIMU

Ukiiga jinsi Yehova anavyotoa nidhamu kwa upendo, kwa usawaziko, na kwa uthabiti, unaweza kuwa na hakika kwamba jitihada zako zitawasaidia sana watoto wako. Mwongozo wako wa upendo utawasaidia watoto wako kukomaa na kuwa watu wazima wenye usawaziko na wanaotegemeka. Kama Biblia inavyosema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.”Methali 22:6.