Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fikiria Unapaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani

Fikiria Unapaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani

“Ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu!”2 PET. 3:11.

1, 2. ‘Tunapaswa kuwa watu wa namna gani’ ili tupate kibali cha Mungu?

NI KAWAIDA kuhangaikia maoni ya wengine kutuhusu. Hata hivyo, tukiwa Wakristo, je, hatupaswi kuhangaikia zaidi maoni ya Yehova kutuhusu? Kwa kweli yeye ndiye Mkuu zaidi katika ulimwengu mzima na ndiye “chemchemi ya uzima.”Zab. 36:9.

2 Akikazia ‘namna ya watu tunaopaswa kuwa’ kulingana na maoni ya Yehova, mtume Petro anatuhimiza tutende “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (Soma 2 Petro 3:11.) Ili kupata kibali cha Mungu, ni lazima ‘matendo yetu ya mwenendo’ yawe matakatifu, yaani, safi kiadili, kiakili, na kiroho. Zaidi ya hayo, tunahitaji kutenda “vitendo vya ujitoaji-kimungu,” tukimheshimu Mungu na kuwa washikamanifu kwake. Hivyo, kutafuta kibali chake hakuhusishi tu mwenendo wetu bali pia utu wetu wa ndani. Kwa kuwa Yehova ndiye “mchunguzaji wa moyo,” anajua ikiwa tuna mwenendo mtakatifu na tumejitoa kabisa kwake au ikiwa hatufanyi hivyo.1 Nya. 29:17.

3. Kuhusu uhusiano wetu na Mungu, ni maswali gani tunayopaswa kufikiria?

3 Shetani Ibilisi hataki tupate kibali cha Mungu. Kwa kweli, anafanya yote awezayo ili tupoteze uhusiano wetu na Yehova. Shetani hutumia uwongo na udanganyifu ili kutushawishi na kutuvuta mbali kutoka kwa Mungu tunayemwabudu. (Yoh. 8:44; 2 Kor. 11:13-15) Kwa hiyo, ni jambo la hekima tujiulize hivi: ‘Shetani huwadanganya watu jinsi gani? Ninaweza kufanya nini ili kulinda uhusiano wangu na Yehova?’

SHETANI HUWADANGANYA WATU JINSI GANI?

4. Shetani hujaribu kuvunja ushikamanifu wetu kwa Mungu akitumia nini, na kwa nini?

4 Mwanafunzi Yakobo anaandika hivi: “Kila mtu  hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” (Yak. 1:14, 15) Shetani hujaribu kuvunja ushikamanifu wetu kwa Mungu akitumia chanzo cha tamaa zetu—moyo wetu.

5, 6. (a) Shetani hutumia njia gani kutushawishi? (b) Ni mambo gani yenye kushawishi anayotumia Shetani kujaribu kupotosha tamaa za moyo wetu, naye ana uzoefu mwingi kadiri gani katika kutumia njia hizo?

5 Shetani hujaribu kuushawishi moyo wetu akitumia nini? Biblia inasema hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Silaha za Shetani zinatia ndani “vitu vilivyo katika ulimwengu.” (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Kwa maelfu ya miaka, Ibilisi ameufinyanga ulimwengu kwa hila ili kutushawishi. Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu huu, tunahitaji kujilinda dhidi ya mbinu zake zenye hila.Yoh. 17:15.

6 Shetani hutumia njia zinazokusudiwa kupotosha tamaa za moyo. Mtume Yohana anataja mambo matatu anayotumia Shetani kutushawishi: (1) “tamaa ya mwili,” (2) “tamaa ya macho,” na (3) “mtu kujionyesha mali yake maishani.” Shetani alitumia mambo hayo kumshawishi Yesu nyikani. Kwa kuwa Shetani ametumia mitego hiyo kwa miaka mingi, anaitumia kwa mafanikio leo, akibadili mbinu zake kulingana na mielekeo ya kila mtu. Kabla ya kuchunguza hatua tunazoweza kuchukua ili kujilinda na mitego hiyo, acheni tuone jinsi Ibilisi alivyofanikiwa kumshawishi Hawa akitumia mambo hayo lakini akashindwa kumshawishi Mwana wa Mungu.

“TAMAA YA MWILI”

Hawa alinaswa na “tamaa ya mwili” (Tazama fungu la 7)

7. Shetani alitumiaje “tamaa ya mwili” kumshawishi Hawa?

7 Wanadamu wanahitaji kutimiza takwa la msingi ili kuendeleza uhai wao, yaani, wanahitaji kula chakula. Muumba aliiumba dunia ikiwa na uwezo wa kuzalisha chakula kingi. Huenda Shetani akatumia tamaa yetu ya kiasili ya kula chakula kujaribu kutushawishi tuache kufanya mapenzi ya Mungu. Fikiria jinsi alivyotumia tamaa hiyo kumshawishi Hawa. (Soma Mwanzo 3:1-6.) Shetani alimwambia Hawa kwamba angeweza kula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” naye hangekufa, kisha akamwambia kwamba siku ambayo angekula matunda ya mti huo, angekuwa kama Mungu. (Mwa. 2:9) Hivyo, Ibilisi alidokeza kwamba Hawa hakuhitaji kumtii Mungu ili kuendelea kuishi. Huo ulikuwa uwongo wa wazi kabisa! Baada tu ya wazo hilo kuingia katika akili ya Hawa, alihitaji kuchagua jambo moja kati ya mambo haya mawili: Angeondoa kabisa wazo hilo akilini, au angeendelea kulifikiria, na kuruhusu tamaa yake ya kula tunda iendelee kusitawi. Licha ya uhakika wa kwamba angeweza kula matunda ya miti mingine  yote katika bustani hiyo, aliamua kuendelea kufikiria mambo aliyosema Shetani kuhusu mti uliokuwa katikati ya bustani, naye “akaanza kuchukua kati ya matunda yake akala.” Hivyo, Shetani alisitawisha ndani ya Hawa tamaa ya kuchukua kilichokatazwa na Muumba.

Yesu hakuruhusu chochote kimpotoshe (Tazama fungu la 8)

8. Shetani alijaribu kumshawishi Yesu jinsi gani akitumia “tamaa ya mwili,” na kwa nini hakufanikiwa kumshawishi?

8 Shetani alitumia mbinu hiyohiyo alipojaribu kumshawishi Yesu nyikani. Baada ya Yesu kufunga kwa siku 40 mchana na usiku, Shetani alijaribu kumshawishi Yesu akitumia tamaa yake ya kula chakula. Shetani akasema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate.” (Luka 4:1-3) Yesu angefanya mojawapo ya mambo haya mawili: Angeamua kutumia nguvu zake za kufanya miujiza kutosheleza uhitaji wake wa chakula, au angeamua kutozitumia. Yesu alijua kwamba hapaswi kutumia nguvu hizo kwa makusudi ya kichoyo. Ingawa alihisi njaa, jambo muhimu kwake halikuwa kutosheleza njaa bali kudumisha uhusiano wake pamoja na Yehova. Yesu akajibu, “Imeandikwa, ‘mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’”Mt. 4:4.

“TAMAA YA MACHO”

9. Maneno “tamaa ya macho” yanadokeza nini, na Shetani alimshawishije Hawa akitumia tamaa hiyo?

9 Yohana alitaja pia kishawishi cha “tamaa ya macho.” Maneno hayo yanadokeza kwamba mtu anaweza kuanza kutamani kitu kwa kukitazama tu. Shetani alitumia tamaa hiyo kumshawishi Hawa aliposema hivi: “Macho yenu yatafunguliwa.” Kadiri Hawa alivyozidi kutazama matunda yaliyokatazwa ndivyo yalivyomvutia zaidi. Hawa akaona kwamba mti huo “ulikuwa kitu cha kutamanika kwa macho.”

10. Shetani alitumiaje “tamaa ya macho” kumshawishi Yesu, naye Yesu alimjibuje?

10 Namna gani Yesu? Shetani ‘alimwonyesha Yesu mara moja falme zote za dunia inayokaliwa; naye Ibilisi akamwambia: ‘Hakika nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake.’” (Luka 4:5, 6) Yesu hangeweza kuona falme zote mara moja kwa macho yake halisi, lakini inawezekana kwamba Shetani alihisi kuwa Yesu angevutiwa ikiwa angeona utukufu wa falme hizo katika maono. Bila aibu yoyote, Shetani akapendekeza hivi: “Ukifanya tendo la ibada mbele yangu, yote itakuwa yako.” (Luka 4:7) Yesu hakutaka kamwe kuwa mtu ambaye Shetani alitaka awe. Alimjibu papo hapo. Alisema hivi: “Imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’”Luka 4:8.

“MTU KUJIONYESHA MALI YAKE MAISHANI”

11. Shetani alimshawishi Hawa jinsi gani?

11 Yohana alipozungumzia vitu vilivyo  katika ulimwengu, alitaja “mtu kujionyesha mali yake maishani.” Hakukuwa na wanadamu wengine duniani isipokuwa Adamu na Hawa, basi hawangeweza ‘kuwaonyesha watu wengine mali yao maishani.’ Lakini walionyesha kiburi. Alipomshawishi Hawa, Shetani alidokeza kwamba Mungu alimnyima Hawa kitu fulani kizuri ajabu. Ibilisi alimwambia kwamba siku ileile ambayo angekula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya,” Hawa ‘angekuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ (Mwa. 2:17; 3:5) Hivyo, Shetani alidokeza kwamba Hawa angeweza kuwa huru bila kumtegemea Yehova. Inaonekana kwamba kiburi ndicho kilichomfanya akubali uwongo huo. Alikula matunda ya mti uliokatazwa, akiamini kwamba kwa hakika hangekufa. Alikosea kama nini!

12. Shetani alitumia njia gani nyingine kujaribu kumshawishi Yesu, na Yesu aliitikiaje?

12 Tofauti na Hawa, Yesu aliweka mfano mzuri kama nini wa unyenyekevu! Shetani alijaribu kumshawishi kwa njia nyingine, lakini Yesu hata hakuwazia kamwe kufanya jambo la kustaajabisha ambalo lingemjaribu Mungu. Hilo lingekuwa tendo la kiburi! Badala yake, Yesu alimjibu waziwazi na moja kwa moja: “Imesemwa, ‘Usimjaribu Yehova Mungu wako.’”Soma Luka 4:9-12.

TUNAWEZAJE KUULINDA UHUSIANO WETU NA YEHOVA?

13, 14. Eleza jinsi Shetani anavyotumia vishawishi fulani leo.

13 Leo, Shetani hutumia mambo kama yale aliyotumia kumshawishi Hawa na Yesu. Ili kuchochea “tamaa ya mwili,” Ibilisi hutumia ulimwengu wake kuendeleza upotovu wa maadili na kuwachochea watu kula na kunywa kupita kiasi. Akitumia ponografia, hasa katika Intaneti, anaweza kuvutia uangalifu wa mtu asiyejali na kuvutia “tamaa ya macho.” Watu wenye kiburi na wale walio na mwelekeo wa ‘kuonyesha mali yao maishani’ hushawishiwa kama nini na tamaa ya vitu vya kimwili, mamlaka, na umashuhuri!

Unapaswa kukumbuka kanuni gani za Kimaandiko unapokabili hali zifuatazo? (Tazama fungu la 13 na 14)

14 “Vitu vilivyo katika ulimwengu” ni kama vyambo vinavyotumiwa na mvuvi. Vinavutia, lakini vimefungwa kwenye ndoana. Shetani hutumia mahitaji ya kila siku ambayo huenda watu wakayaona kuwa ya kawaida ili kuwafanya watende kinyume cha sheria za Mungu. Hata hivyo, vishawishi kama hivyo vyenye hila vimekusudiwa kuongoza tamaa zetu na kuuchafua  moyo wetu. Kwa kweli Shetani hutumia vishawishi hivyo kujaribu kutufanya tuamini kwamba kutanguliza starehe na mahitaji yetu ya kibinafsi ni muhimu zaidi kuliko kufanya mapenzi ya Mungu. Je, tutanaswa na vishawishi hivyo?

15. Tunawezaje kumwiga Yesu katika kupinga vishawishi vya Shetani?

15 Hawa alidanganywa na vishawishi vya Shetani, lakini Yesu alivipinga kwa mafanikio. Kila mara, alitoa jibu la Kimaandiko, akisema: “Imeandikwa” au, “Imesemwa.” Ikiwa sisi ni wanafunzi wenye bidii wa Biblia, tutayaelewa vizuri zaidi Maandiko na tutakumbuka mistari inayoweza kutusaidia kufikiria kwa utimamu tunaposhawishiwa. (Zab. 1:1, 2) Kukumbuka mifano ya Kimaandiko ya watu waaminifu waliokuwa washikamanifu kwa Mungu kutatusaidia kuwaiga. (Rom. 15:4) Kumheshimu na kumwogopa Yehova kikweli, kupenda mambo anayopenda na kuchukia anayochukia, kutatulinda.Zab. 97:10.

16, 17. ‘Nguvu zetu za kufikiri’ zinaweza kuamuaje namna tulivyo?

16 Mtume Paulo anatutia moyo tutumie ‘nguvu zetu za kufikiri’ ili tuwe watu ambao wanafinyangwa na fikira za Mungu, wala si ulimwengu. (Rom. 12:1, 2) Akikazia uhitaji wa kudhibiti kabisa mambo tunayofikiria, Paulo alisema hivi: “Tunapindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu; nasi tunaiteka kila fikira ili kuifanya imtii Kristo.” (2 Kor. 10:5) Mambo tunayofikiria yana nguvu za kuamua tutakuwa watu wa namna gani, hivyo tunahitaji ‘kuendelea kufikiria’ mambo yanayojenga.Flp. 4:8.

17 Hatuwezi kutarajia kuwa watakatifu ikiwa tunaendelea kukazia fikira tamaa na mambo yasiyofaa. Ni lazima tumpende Yehova kwa “moyo safi.” (1 Tim. 1:5) Lakini moyo ni wenye hila, na huenda hata tusitambue jinsi tunavyoathiriwa sana na “vitu vilivyo katika ulimwengu.” (Yer. 17:9) Hivyo basi, je, hatupaswi ‘kuendelea kujijaribu kama sisi tuko katika imani, kuendelea kuthibitisha sisi wenyewe jinsi tulivyo’ kwa kujichunguza kwa unyoofu tukitumia mambo tunayojifunza katika Biblia?2 Kor. 13:5.

18, 19. Kwa nini tunapaswa kuazimia kuwa namna ya watu ambao Yehova anataka tuwe?

18 Jambo lingine linaloweza kutusaidia kupinga “vitu vilivyo katika ulimwengu” ni kuendelea kukumbuka maneno aliyosema Yohana kwa mwongozo wa roho takatifu: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yoh. 2:17) Mfumo wa Shetani unaonekana kuwa wa kudumu na halisi. Hata hivyo, siku moja utafikia mwisho wake. Hakuna kitu chochote katika ulimwengu wa Shetani kitakachodumu. Kukumbuka jambo hilo kutatusaidia kutovutiwa na vishawishi vya Ibilisi.

19 Mtume Petro anatuhimiza tuwe namna ya watu wanaokubaliwa na Mungu huku ‘tukingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo kupitia hiyo mbingu zikiwa zimewaka moto zitayeyushwa na vitu vya msingi vikiwa moto sana vitayeyuka!’ (2 Pet. 3:12) Hivi karibuni, siku hiyo itafika na Yehova ataharibu kila sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Kabla ya wakati huo, Shetani ataendelea kutumia “vitu vilivyo katika ulimwengu” ili kutushawishi kama alivyomshawishi Hawa na Yesu. Hatupaswi kuwa kama Hawa na kutafuta kutosheleza tamaa zetu wenyewe. Tukifanya hivyo tutakuwa tukionyesha kwamba Shetani ni mungu wetu. Tunahitaji kupinga vishawishi hivyo kama Yesu alivyofanya, hata viwe vinapendeza au vinavutia kadiri gani. Kila mmoja wetu na aazimie kuwa namna ya watu ambao Yehova anataka tuwe.