Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yeye Ni Mfano Mzuri au Ni Onyo Kwako?

Je, Yeye Ni Mfano Mzuri au Ni Onyo Kwako?

Je, Yeye Ni Mfano Mzuri au Ni Onyo Kwako?

“Mungu wa Yakobo . . . atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.”—ISA. 2:3.

1, 2. Unaweza kufaidika jinsi gani kutokana na mifano ya Biblia?

JE, HUSADIKI kwamba unaweza kufaidika na yale yaliyoandikwa katika Biblia? Katika Biblia, unaweza kusoma kuhusu mifano ya wanaume na wanawake waaminifu ambao ungetaka kuiga maisha na sifa zao. (Ebr. 11:32-34) Hata hivyo, inaelekea kwamba umeona pia mifano yenye kuonya, yaani, wanaume na wanawake ambao unapaswa kuepuka matendo au mitazamo yao.

2 Kwa kweli, baadhi ya watu wanaotajwa katika Biblia wanaweza kuwa mifano mizuri ya kuigwa na pia kutuonya kuhusu mambo tunayopaswa kuepuka. Mfikirie Daudi, aliyekuwa mchungaji tu na baadaye akawa mfalme mwenye nguvu. Yeye ni mfano mzuri wa mtu aliyependa kweli na aliyemtegemea Yehova. Hata hivyo, Daudi alikuwa na hatia ya kufanya dhambi nzito, kama ile ya uzinzi pamoja na Bath-sheba, kupanga njama ya kumuua Uria, na pia tendo lisilo la hekima la kuwahesabu watu. Hata hivyo, acheni tuzungumze kuhusu mwana wake, yaani, mfalme na pia mwandikaji wa Biblia, Sulemani. Kwanza, tutazungumzia jinsi alivyokuwa mfano mzuri katika njia mbili.

“Hekima ya Sulemani”

3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Sulemani alikuwa mfano mzuri kwetu?

3 Sulemani Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, alisema mambo mazuri kumhusu Mfalme Sulemani, na hivyo akatutia moyo tuige mfano wake mzuri. Yesu aliwaambia hivi Wayahudi fulani waliokuwa na shaka: “Malkia wa kusini atasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki naye atakihukumu kuwa chenye hatia; kwa sababu alikuja kutoka miisho ya dunia kuisikia hekima ya Sulemani, lakini, tazama! mtu mkuu kuliko Sulemani yuko hapa.” (Mt. 12:42) Naam, Sulemani alikuwa maarufu kwa sababu ya hekima yake, na alitutia moyo tuitafute.

4, 5. Sulemani alipataje hekima, lakini kwa nini ni tofauti na jinsi tunavyopata hekima leo?

4 Mwanzoni mwa utawala wa Sulemani, Mungu alimtokea katika ndoto na akamwambia aombe chochote anachotaka. Akijua kwamba hakuwa na uzoefu maishani, Sulemani aliomba hekima. (Soma 1 Wafalme 3:5-9.) Mungu alifurahi kwamba mfalme huyo aliomba hekima badala ya kuomba utajiri na utukufu, hivyo akampa Sulemani “moyo wenye hekima na wenye uelewaji,” na pia utajiri. (1 Fal. 3:10-14) Kama Yesu alivyosema, hekima ya Sulemani ilikuwa ya pekee sana hivi kwamba malkia wa Sheba alisikia kuihusu na hivyo akafunga safari ndefu ili akutane na Sulemani na kuisikia hekima yake.—1 Fal. 10:1, 4-9.

5 Sisi binafsi hatutarajii kupata hekima kimuujiza. Sulemani alisema kwamba “Yehova mwenyewe anatoa hekima,” lakini aliandika kwamba tunapaswa kujitahidi kupata sifa hiyo ya Mungu: “Usikilize hekima kwa makini, ili uelekeze moyo wako kwenye utambuzi.” Alitumia pia maneno kama vile ‘kuiita’ na ‘kuendelea kuitafuta’ hekima. (Met. 2:1-6) Ni wazi kwamba tunaweza kupata hekima.

6. Tunaweza kuonyesha katika njia zipi kwamba tunafaidika na mfano mzuri wa Sulemani kuhusiana na hekima?

6 Ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, ninachukua kwa uzito mfano wa Sulemani wa kuthamini hekima ya Mungu?’ Matatizo ya kiuchumi yamewafanya wengi wakazie fikira pesa na kazi zao au yameathiri maamuzi yao kuhusu aina na kiwango cha elimu wanachotaka kupata. Namna gani wewe na familia yako? Je, maamuzi yako yanaonyesha kwamba unathamini na kutafuta hekima ya Mungu? Je, unahitaji kubadili njia yako ya kufikiri kuhusu pesa na elimu ili ujitahidi zaidi kupata hekima? Kwa kweli, kupata na kutumia hekima kutatunufaisha milele. Sulemani aliandika hivi: “Ndipo utakapoelewa uadilifu na hukumu na unyoofu, njia yote ya yaliyo mema.”—Met. 2:9.

Kutanguliza Ibada ya Kweli Kulileta Amani

7. Mungu alipataje kuwa na hekalu kubwa?

7 Mwanzoni mwa utawala wake, Sulemani alichukua hatua za kubomoa maskani ambayo ilikuwa ikitumiwa tangu siku za Musa na kujenga hekalu zuri kabisa. (1 Fal. 6:1) Tunaweza kuliita hekalu la Sulemani, lakini hakulijenga ili ajitafutie umaarufu au utajiri na hata hakupendekeza hekalu hilo lijengwe. Kwa kweli, Daudi ndiye aliyependekeza kwanza wazo la kujenga hekalu, halafu Mungu akampa Daudi ramani kamili kwa ajili ya hekalu na vyombo vyake vyote. Na pia Daudi alitoa mchango mkubwa wa kifedha kwa ajili ya mradi huo wa ujenzi. (2 Sam. 7:2, 12, 13; 1 Nya. 22:14-16) Hata hivyo, Sulemani ndiye aliyekuwa na wajibu wa kujenga hekalu hilo ambalo ujenzi wake ulidumu kwa miaka saba na nusu.—1 Fal. 6:37, 38; 7:51.

8, 9. (a) Sulemani anatuwekea mfano gani mzuri wa kudumu katika matendo mema? (b) Kulikuwa na matokeo gani Sulemani alipotanguliza ibada ya kweli?

8 Kwa hiyo, Sulemani alituwekea mfano mzuri wa kudumu katika matendo mema, na akaendelea kukazia fikira mambo mazuri. Ujenzi wa hekalu ulipokamilika na sanduku la agano kuwekwa ndani yake, Sulemani alitoa sala ya hadharani. Kwa sehemu, alisali hivi kwa Yehova: “[Na] macho yako yafunguliwe kuielekea nyumba hii usiku na mchana, kuelekea mahali ambapo ulisema hivi kupahusu, ‘Jina langu litakuwa hapo,’ ili kusikiliza sala ambayo mtumishi wako anatoa kuelekea mahali hapa.” (1 Fal. 8:6, 29) Waisraeli na wageni wangesali kuelekea jengo hilo ambalo liliitwa kwa jina la Mungu.—1 Fal. 8:30, 41-43, 60.

9 Kulikuwa na matokeo gani Sulemani alipotanguliza ibada ya kweli? Baada ya kusherehekea kuzinduliwa kwa hekalu, watu ‘walishangilia na kufurahi moyoni mwao kutokana na wema wote ambao Yehova alikuwa ametenda kwa ajili ya Daudi mtumishi wake na kwa ajili ya Israeli.’ (1 Fal. 8:65, 66) Kwa kweli, utawala wa Sulemani wa miaka 40 ulikuwa wenye amani na ufanisi mwingi. (Soma 1 Wafalme 4:20, 21, 25.) Zaburi ya 72 inatueleza kuhusu hilo na inatusaidia kuelewa vizuri zaidi baraka ambazo tutafurahia chini ya utawala wa Sulemani Mkuu Zaidi, Yesu Kristo.—Zab. 72: 6-8, 16.

Onyo Tunalopata Kutokana na Maisha ya Sulemani

10. Ni kosa gani alilofanya Sulemani ambalo tunakumbuka kwa urahisi?

10 Hata hivyo, kwa nini tunaweza kusema kwamba maisha ya Sulemani pia ni onyo kwetu? Huenda ukafikiria kwanza kuhusu masuria na wake zake wageni. Tunasoma hivi: “Ikawa kwamba wakati Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Yehova.” (1 Fal. 11:1-6) Bila shaka, umeazimia kutoiga kamwe mwenendo wake wa kipumbavu. Lakini je, hilo ndilo onyo pekee tunalojifunza kutokana na maisha ya Sulemani? Fikiria mambo mengine katika maisha ya Sulemani ambayo huenda ni rahisi kuyapuuza, na uone ni onyo gani unalojifunza.

11. Tunaweza kujifunza nini kuhusu ndoa ya kwanza ya Sulemani?

11 Sulemani alitawala kwa miaka 40. (2 Nya. 9:30) Hivyo, unaweza kujifunza nini kutokana na andiko la 1 Wafalme 14:21? (Soma.) Kulingana na mstari huo, baada ya kifo cha Sulemani, mwana wake Rehoboamu alianza kutawala kama mfalme akiwa na umri wa miaka 41. Mama yake alikuwa “Naama Mwamoni.” Hilo linamaanisha kwamba kabla ya Sulemani kuwa mfalme, alioa mke mgeni kutoka katika taifa adui ambalo liliabudu miungu ya sanamu. (Amu. 10:6; 2 Sam. 10:6) Je, mwanamke huyo aliabudu miungu hiyo? Hata ikiwa wakati mmoja aliabudu miungu hiyo, huenda aliacha kuabudu sanamu na kuwa mwabudu wa kweli kama walivyofanya Rahabu na Ruthu. (Rut. 1:16; 4:13-17; Mt. 1:5, 6) Hata hivyo, inaelekea Sulemani alikuwa na wakwe na watu wa ukoo Waamoni ambao hawakumtumikia Yehova.

12, 13. Sulemani alifanya uamuzi gani mbaya mapema katika utawala wake, na huenda alifikirije?

12 Na bila shaka mambo yalikuwa mabaya hata zaidi baada ya yeye kuwa mfalme. Sulemani alifanya “mapatano ya ndoa pamoja na Farao mfalme wa Misri, akamchukua binti ya Farao, akamleta katika Jiji la Daudi.” (1 Fal. 3:1) Je, mwanamke huyo Mmisri aliiga mfano wa Ruthu na kuwa mwabudu wa kweli? Hakuna jambo linaloonyesha kwamba alifanya hivyo. Badala yake, baada ya muda Sulemani alimjengea nyumba (na labda wajakazi wake Wamisri) nje ya Jiji la Daudi. Kwa nini? Maandiko yanasema kwamba alifanya hivyo kwa sababu haikufaa kwa mwabudu wa uwongo kuishi karibu na sanduku la agano.—2 Nya. 8:11.

13 Huenda Sulemani alifikiri kwamba kuoa binti ya mfalme wa Misri kungekuwa na faida za kisiasa kwa kuwa hilo lingeimarisha urafiki kati ya Israeli na Misri. Lakini je, hicho kilikuwa kisingizio kinachofaa? Muda mrefu kabla ya hapo, Mungu alikuwa amewakataza watu wake kuoa Wakanaani wapagani, hata alitaja orodha ya mataifa fulani ambayo walipaswa kuyaepuka. (Kut. 34:11-16) Je, Sulemani alifikiri kwamba Misri haikuwa kwenye orodha ya mataifa hayo? Hata ikiwa alifikiri hivyo, je, Mungu angekubali kisingizio hicho? Ni wazi kwamba Sulemani alipuuza onyo la Yehova lililokuwa wazi la kwamba ingekuwa hatari kuoa mtu wa taifa lingine, kwa sababu mtu huyo angemgeuza Mwisraeli aache ibada ya kweli na kuanza kuabudu miungu ya uwongo.—Soma Kumbukumbu la Torati 7:1-4.

14. Mfano wa Sulemani unawezaje kuwa onyo kwetu?

14 Je, maisha ya Sulemani yatakuwa onyo kwetu? Huenda dada akajaribu kutoa kisingizio cha kuwa na uhusiano wa kimapenzi na kupuuza amri ya Mungu ya kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Au tunaweza kutoa visingizio katika mambo mengine. Kwa mfano, huenda mtu akatoa visingizio ili kujiunga na klabu mbalimbali shuleni au kushiriki katika michezo baada ya masomo, au kutotoa ripoti kamili ya ushuru, au kutosema ukweli anapoulizwa kuhusu mambo fulani aliyofanya yanayoweza kumwaibisha. Somo ni kwamba bila shaka Sulemani alitoa visingizio ili asitii amri za Mungu, nasi pia tunakabili hatari hiyohiyo.

15. Yehova alionyeshaje rehema katika kushughulika na Sulemani, lakini tunapaswa kukumbuka nini kuhusu hilo?

15 Ona kwamba baada ya kutaja ndoa ya Sulemani pamoja na binti ya mfalme wa Misri, Biblia inasema kwamba Mungu alimpa Sulemani hekima kama alivyoomba, na pia Akamwongezea utajiri. (1 Fal. 3:10-13) Sulemani alikuwa amepuuza maagizo ya Mungu, hata hivyo hakuna jambo linaloonyesha kwamba Yehova alimkataa mara moja asiwe mfalme au kwamba alimwadhibu vikali. Sababu ni kwamba Mungu anajua kuwa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu waliofanywa kutokana na mavumbi. (Zab. 103:10, 13, 14) Hata hivyo, kumbuka kwamba matendo yetu yanaweza kuwa na matokeo mabaya sasa au labda baadaye katika maisha yetu.

Wake Wengi Sana!

16. Kwa kuchukua wake wengi, Sulemani alikuwa akipuuza amri gani?

16 Katika kitabu cha Wimbo wa Sulemani, mfalme alimsifu msichana mmoja bikira akisema kwamba alikuwa mrembo zaidi kuliko malkia 60 na masuria 80. (Wim. 6:1, 8-10) Ikiwa hali hiyo inamhusu Sulemani, hilo linamaanisha kwamba wakati huo katika utawala wake, Sulemani alikuwa tayari na idadi hiyo ya wanawake. Hata ikiwa wengi wao au wote walikuwa waabudu wa kweli, mwongozo wa Mungu kupitia Musa ulikuwa kwamba mfalme wa Israeli asingepaswa ‘kuzidisha wake kwa ajili yake, ili moyo wake usigeuke kando.’ (Kum. 17:17) Hata hivyo, kwa mara nyingine tena, Yehova hakumkataa Sulemani. Kwa kweli, bado Mungu alimbariki Sulemani, huku akimtumia kuandika kitabu cha Biblia cha Wimbo wa Sulemani.

17. Ni ukweli gani ambao hatupaswi kupuuza?

17 Je, hilo linamaanisha kwamba Sulemani angepuuza mwongozo wa Mungu bila kupata madhara au kwamba sisi pia tunaweza kufanya hivyo? Hapana. Badala yake, hilo linaonyesha kwamba subira ya Mungu inaweza kuendelea kwa wakati fulani. Ukweli ni kwamba mtu anaweza kupuuza mwongozo wa Mungu na asipatwe papo hapo na matokeo mabaya, lakini hilo halimaanishi kwamba mwishowe hatapatwa na matokeo yenye kuhuzunisha. Kumbuka yale ambayo Sulemani aliandika: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.” Akaongeza hivi: “Ninajua pia kwamba mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli, kwa sababu walimwogopa.”—Mhu. 8:11, 12.

18. Kisa cha Sulemani kinaonyeshaje ukweli wa maneno ya Wagalatia 6:7?

18 Inasikitisha kwamba Sulemani hakuendelea kutii kweli hiyo ya Neno la Mungu! Naam, alikuwa ametimiza mengi na kufurahia baraka za Mungu kwa muda mrefu. Lakini alianza kufanya makosa hatua kwa hatua kadiri muda ulivyopita, na hivyo akazoea kutotii amri za Yehova. Baadaye, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika ukweli huu: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia”! (Gal. 6:7) Baadaye, Sulemani alipatwa na matokeo yenye kuhuzunisha ya kupuuza mwongozo wa Mungu. Tunasoma hivi: “Mfalme Sulemani akawapenda wake wengi wageni pamoja na binti ya Farao, wanawake Wamoabu, Waamoni, Waedomu, Wasidoni na Wahiti.” (1 Fal. 11:1) Inaelekea wengi wa wanawake hao waliendelea kushikamana na miungu ya uwongo, na bila shaka Sulemani hangeweza kuepuka mtego huo. Alipotoshwa na akapoteza kibali cha Mungu wetu mwenye subira.—Soma 1 Wafalme 11:4-8.

Jifunze Kutokana na Mambo Mazuri na Mabaya Aliyofanya

19. Kwa nini unaweza kusema kwamba Biblia ina mifano mingi mizuri?

19 Kwa fadhili, Yehova, kupitia roho yake takatifu, alimwongoza Paulo kuandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Rom. 15:4) Mambo hayo yaliyoandikwa yanatia ndani mifano mingi mizuri ya wanaume na wanawake wenye imani ya pekee. Paulo alisema hivi: “Nitasema nini zaidi? Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia juu ya Gideoni, Baraka, Samsoni, Yeftha, Daudi na vilevile Samweli na wale manabii wengine, ambao kupitia imani walishinda falme katika mapambano, wakatenda uadilifu, wakapata ahadi . . . kutoka hali ya udhaifu wakafanywa kuwa wenye nguvu.” (Ebr. 11:32-34) Tunaweza na tunapaswa kufaidika kutokana na mifano mizuri iliyo katika Maandiko, na kufuata au kuiga mambo yanayoonyeshwa katika masimulizi hayo mazuri ya Biblia.

20, 21. Kwa nini umeazimia kufaidika kutokana na maonyo yaliyo katika Neno la Mungu?

20 Hata hivyo, masimulizi fulani ya Biblia yanatia ndani maonyo. Tunaweza kuyapata baadhi ya maonyo hayo tukichunguza maisha ya wanaume na wanawake ambao Yehova aliwakubali na kuwatumia wakiwa watumishi wake wakati fulani. Tunaposoma Biblia, tunaweza kujifunza kuhusu makosa ambayo baadhi ya watu wa Mungu walifanya, jinsi walivyokosea na hivyo kuyaepuka. Tunaweza kutambua kwamba baadhi yao walisitawisha mitazamo au mielekeo mibaya hatua kwa hatua, mielekeo ambayo mwishowe ilisababisha matokeo yenye kuhuzunisha. Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi kama hayo? Huenda tukajiuliza maswali kama haya: ‘Hali hiyo ilianzaje kusitawi? Je, ninaweza kusitawisha mwelekeo kama huo? Ninaweza kufanya nini ili kuepuka hali hiyo na badala yake kufaidika kutokana na onyo hilo?’

21 Bila shaka, tunapaswa kufikiria kwa uzito mifano hiyo kwa sababu Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.”—1 Kor. 10:11.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini unaweza kupata mifano mizuri na maonyo katika Biblia?

• Sulemani aliruhusu jinsi gani mazoea mabaya yasitawi katika maisha yake?

• Unaweza kufaidikaje kutokana na mfano mbaya wa Sulemani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sulemani alitumia hekima aliyopewa na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je, unafaidika kutokana na onyo kumhusu Sulemani?