Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu Kristo alipowatuma wale mitume 12 kuhubiri, je, waliambiwa wabebe fimbo na kuvaa viatu?

Watu fulani wanadai kwamba masimulizi matatu ya Injili yanayoripoti kuhusu Yesu kuwatuma mitume hao yanapingana. Hata hivyo, tunapolinganisha masimulizi hayo, tunaweza kufikia uamuzi mzuri. Kwanza, linganisha mambo ambayo Marko na Luka waliandika. Simulizi la Marko linasema hivi: “[Yesu] akawaagiza wasichukue kitu chochote kwa ajili ya safari, wala mkate, wala mfuko wa chakula, wala pesa za shaba katika mikoba kwenye mishipi yao ila fimbo tu, lakini wafunge viatu, na wasivae mavazi mawili ya ndani.” (Marko 6:7-9) Luka aliandika hivi: “Msichukue kitu chochote kwa ajili ya safari, wala fimbo wala mfuko wa chakula, wala mkate wala fedha; wala msiwe na mavazi mawili ya ndani.” (Luka 9:1-3) Katika maandiko hayo tunaona habari ambayo inaonekana kwamba inapingana. Marko anasema kwamba mitume waliambiwa wabebe fimbo na kufunga viatu, lakini simulizi la Luka linasema kwamba hawakupaswa kubeba kitu chochote, hata fimbo. Tofauti na Marko, Luka hakutaja viatu.

Ili kuelewa maagizo ambayo Yesu alikuwa akitoa wakati huo, ona maneno ambayo yanapatikana katika Injili zote tatu. Katika masimulizi ambayo tayari yametajwa na pia katika Mathayo 10:5-10, mitume waliambiwa wasivae au wasiwe na “mavazi mawili ya ndani.” Inaelekea kwamba kila mtume alikuwa amevaa vazi moja la ndani. Basi hawakupaswa kubeba vazi lingine kwa ajili ya safari. Pia, walikuwa wamevaa viatu. Marko alikazia kwamba walihitaji ‘kufunga viatu’ ambavyo walikuwa tayari wamevaa. Namna gani fimbo? Kitabu kimoja (The Jewish Encyclopedia) kinasema hivi: “Inaonekana kwamba kwa ujumla Waebrania wa kale walikuwa pia na desturi ya kubeba fimbo.” (Mwa. 32:10) Marko alitaja kwamba mitume hawakupaswa ‘kuchukua kitu chochote kwa ajili ya safari’ isipokuwa fimbo waliyokuwa nayo wakati Yesu alipowapa amri hiyo. Hivyo, waandikaji wa Injili walikuwa wakikazia maagizo ya Yesu ya kutojishughulisha sana kutafuta vitu vya ziada kwa ajili ya safari.

Jambo hilo linakaziwa zaidi na Mathayo, ambaye alisikia amri ya Yesu wakati huo na kuiandika. Yesu alisema hivi: “Msichukue dhahabu wala fedha wala shaba kwa ajili ya mikoba yenu ya mshipi, wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi mawili ya ndani, wala viatu wala fimbo; kwa maana mfanyakazi anastahili chakula chake.” (Mt. 10:9, 10) Namna gani viatu ambavyo mitume walikuwa wamevaa na fimbo ambazo walikuwa nazo mikononi? Yesu hakuwaambia watupe vitu ambavyo tayari walikuwa navyo, lakini alikuwa akiwaambia wasichukue vitu kama hivyo. Kwa nini alitoa amri hiyo? Kwa sababu “mfanyakazi anastahili chakula chake.” Hivyo ndivyo Yesu alivyomaanisha alipotoa amri hiyo, na hilo lilipatana na himizo alilotoa katika Mahubiri ya Mlimani kwamba wasihangaike kuhusu kile ambacho watakula, kunywa, au kuvaa.—Mt. 6:25-32.

Ingawa masimulizi hayo ya Injili yanaweza kuonekana yanapingana, yote yalikazia jambo lilelile. Mitume walipaswa kwenda jinsi walivyokuwa na hawakupaswa kukengeushwa fikira wakitafuta kitu chochote cha ziada. Kwa nini? Kwa sababu Yehova angewatimizia mahitaji yao.

“Bibi, naam mabibi” ambao Sulemani alitaja walikuwa nani?—Mhu. 2:8.

Hatuwezi kuwa na hakika wao ni nani, lakini inawezekana kwamba walikuwa wanawake mashuhuri ambao Sulemani alikutana nao katika makao yake ya kifalme.

Katika kitabu cha Mhubiri sura ya 2, Sulemani alitaja mambo mbalimbali ambayo alikuwa ametimiza, kutia ndani miradi yake mikubwa ya ujenzi. Aliongezea hivi: “Pia nikajikusanyia fedha na dhahabu, na mali iliyo ya pekee kwa wafalme na wilaya za utawala. Nikajifanyia waimbaji wa kiume na wa kike na wale walio furaha tele ya wana wa binadamu, bibi, naam mabibi.”—Mhu. 2:8.

Wasomi wengi wanadai kwamba “mabibi” ambao Sulemani alitaja walikuwa masuria na wake wengi wa kigeni ambao alipata katika miaka yake ya baadaye, wanawake ambao walimfanya aingie katika ibada ya uwongo. (1 Fal. 11:1-4) Hata hivyo, ni vigumu kuelewa maelezo hayo. Sulemani alipoandika maneno hayo, tayari aliwafahamu “bibi, naam mabibi.” Na wakati huo, bado alikuwa na kibali cha Yehova, kwa kuwa Mungu alikuwa akimwongoza kwa roho yake kuandika vitabu vya Biblia. Hali hiyo ni tofauti kabisa na miaka mingi baadaye alipokuwa na mamia ya wake wa kigeni na masuria na alipojiingiza katika ibada ya uwongo.

Katika kitabu cha Mhubiri, Sulemani alisema kwamba “alijitahidi kutafuta maneno yenye kupendeza na kuandika maneno sahihi ya kweli.” (Mhu. 12:10) Bila shaka alijua maneno “mke,” “malkia,” na “suria,” kwa kuwa aliyatumia maneno hayo katika maandishi yake yaliyoongozwa na roho ya Mungu. (Met. 5:18; 12:4; 18:22; Mhu. 9:9; Wim. 6:8, 9) Lakini katika Mhubiri 2:8, maneno hayo yanayojulikana hayajatumiwa.

Maneno “bibi, naam mabibi,” ni mfano pekee (umoja na wingi) katika Biblia wa neno la Kiebrania lisilo la kawaida. Wasomi wanakubali kwamba maana yake haijulikani. Watafsiri wengi wa Biblia wanaamini kwamba maneno yaliyo katika Mhubiri 2:8 yanamaanisha wanawake, yakitajwa katika umoja na kisha katika wingi au cheo cha juu zaidi. Usemi “bibi, naam mabibi” unatokeza wazo hilo.

Sulemani alijulikana sana hivi kwamba malkia mmoja kutoka ufalme wenye utajiri wa Sheba alisikia kumhusu, akamtembelea, na alivutiwa na mambo aliyoona. (1 Fal. 10:1, 2) Hilo linaonyesha uwezekano mmoja wa maana ya maneno yaliyotajwa na Sulemani, “bibi, naam mabibi.” Huenda alikuwa akizungumza kuhusu wanawake mashuhuri ambao alikutana nao kwenye makao yake kwa miaka mingi alipokuwa bado na kibali cha Mungu.