Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi Iweni Vielelezo Bora kwa Watoto Wenu

Wazazi Iweni Vielelezo Bora kwa Watoto Wenu

Wazazi Iweni Vielelezo Bora kwa Watoto Wenu

“WATAALAMU wa akili wanaweza kusimamisha utafiti wao wa muda mrefu kuhusu njia bora ya kulea watoto, si kwa sababu wameipata lakini kwa sababu haipo.” Hivyo ndivyo gazeti moja (Time) lilivyosema lilipokuwa likizungumzia kitabu kimoja kuhusu kulea watoto. Kitabu hicho kinasema kwamba watoto huiga maadili ya marika wao wala si ya wazazi wao.

Tunapaswa kukubali kwamba msongo wa marika una uvutano wenye nguvu. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Mwandishi wa gazeti, William Brown, alisema hivi: ‘Vijana hujitahidi juu chini kujipatanisha na marika wao. . . . Vijana huona kwamba ni heri kufa kuliko kuwa tofauti na marika wao.’ Wazazi wanaposhindwa kufanya maisha ya nyumbani kuwa yenye kuchangamsha na kupendeza au wasipotumia wakati wa kutosha pamoja na watoto wao—kama ilivyo kawaida katika ulimwengu wa leo wenye shughuli nyingi—wanaruhusu uvutano wa marika uwadhuru watoto wao.

Isitoshe, katika ‘siku hizi za mwisho,’ familia zinakabili hatari kwa sababu Biblia ilitabiri kwamba watu wangejishughulisha na utafutaji wa pesa, raha, na mambo ya ubinafsi. Je, tunapaswa kushangaa kuona watoto “wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili”?—2 Timotheo 3:1-3.

Maneno “upendo wa asili,” kama yanavyotumiwa katika Biblia, yanafafanua upendo wa familia. Upendo huo ni kifungo cha asili ambacho huwachochea wazazi kuwatunza watoto wao na watoto kushikamana na wazazi wao. Lakini wazazi wanapokosa kuonyesha upendo wa asili, watoto watatafuta kutegemezwa kihisia na watu wengine nje ya familia, hasa marika wao, na yaelekea wataiga viwango na mitazamo ya marika wao. Lakini, mara nyingi hali hiyo inaweza kuepukika ikiwa wazazi wanaruhusu kanuni za Biblia ziongoze maisha ya familia.—Methali 3:5, 6.

Familia—Mpango Ulioanzishwa na Mungu

Baada ya kuwaunganisha Adamu na Hawa kuwa mume na mke, Mungu aliwaagiza hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” Baadaye, familia ikaanzishwa, yaani, baba, mama, na watoto. (Mwanzo 1:28; 5:3, 4; Waefeso 3:14, 15) Ili kuwasaidia wanadamu kulea watoto wao, Yehova alifanya madaraka fulani ya wazazi yaongozwe kisilika. Hata hivyo, tofauti na wanyama, wanadamu wanahitaji msaada wa ziada. Hivyo, Yehova aliandaa miongozo iliyoandikwa kwa ajili yao. Hiyo inatia ndani miongozo kuhusu maadili, mambo yanayohusiana na ibada ya Mungu, na kuwatia watoto nidhamu kwa njia inayofaa.—Methali 4:1-4.

Akizungumza hasa kuhusu akina baba, Mungu alisema hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Methali 1:8, 9) Ona kwamba wazazi walipaswa kuiweka kwanza sheria ya Mungu ndani ya mioyo yao wenyewe. Kwa nini hilo lilikuwa muhimu? Kwa sababu kufundisha hakutegemei tu yale ambayo mtu anasema bali pia mambo ambayo moyo wake unamchochea kutenda. Wazazi wanapofundisha tu mambo yanayotoka moyoni mwao ndipo wanapoweza kugusa mioyo ya watoto wao. Wazazi hao pia watakuwa vielelezo kwa watoto wao kwa kuwa watoto hutambua unafiki kwa urahisi.—Waroma 2:21.

Wazazi Wakristo wanaambiwa wawafundishe watoto wao tangu utotoni kwa ‘kuendelea kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’ (Waefeso 6:4; 2 Timotheo 3:15) Tangu utotoni? Naam! Mama mmoja aliandika hivi: “Wakati mwingine sisi wazazi hupuuza uwezo wa watoto wetu. Wana uwezo mbalimbali. Sisi wazazi tunapaswa kuwasaidia waendelee kuukuza.” Naam, watoto hufurahia kujifunza, na wanapofundishwa na wazazi wanaomwabudu Mungu, wao pia hujifunza kuwa na upendo. Watoto hao watajihisi salama wanapofuata sheria walizowekewa na wazazi wao. Hivyo, wazazi wanaofanikiwa ni wale wanaojitahidi kuwa marafiki wenye upendo, wenye kuwasiliana vizuri na watoto wao, na walimu wenye subira lakini walio thabiti wanaofanyiza mazingira mazuri ambayo huwasaidia watoto wao kusitawi. *

Linda Watoto Wako

Katika barua moja aliyoandikia wazazi, mwalimu mkuu wa shule moja huko Ujerumani alisema hivi: “Tungependa kuwatia moyo ninyi wazazi wapendwa mjitahidi wenyewe kuwalea watoto wenu badala ya kuacha televisheni au mashirika mabaya yatimize daraka lenu la kusitawisha utu wao.”

Kuiachia televisheni au mashirika mabaya mtoto wako, ni kuacha roho ya ulimwengu iwe na uvutano juu ya malezi ya mtoto huyo. (Waefeso 2:1, 2) Roho hiyo ya ulimwengu hupinga roho ya Mungu, na kama upepo mkali, roho hiyo hubeba mbegu za mtazamo wa ‘kidunia, wa kinyama, na wa roho waovu’ nayo hutia mbegu hizo katika akili na mioyo ya wasio na uzoefu au wapumbavu. (Yakobo 3:15) Mwishowe, mtazamo huo ulio kama magugu huharibu moyo. Yesu alieleza hivi kuhusu matokeo ya mambo yanayopandwa ndani ya moyo: “Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutokeza maovu katika hazina yake mbovu; kwa maana kutokana na wingi wa moyo kinywa chake husema.” (Luka 6:45) Hivyo, Biblia inatuhimiza hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.”—Methali 4:23.

Bila shaka, watoto ni watoto, na wengine wao wana mwelekeo wa ukaidi, na hata wa kuasi. (Mwanzo 8:21) Wazazi wanaweza kufanya nini? Biblia inasema hivi: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana; fimbo ya nidhamu ndiyo itakayouondolea mbali.” (Methali 22:15) Wengine wana maoni ya kwamba kutumia fimbo ni kumnyanyasa mtoto na kwamba jambo hilo limepitwa na wakati. Ni kweli kwamba Biblia inapinga jeuri ya aina yoyote. Ingawa wakati mwingine “fimbo” hiyo humaanisha mamlaka ya wazazi ya kutia adhabu kwa uthabiti, adhabu hiyo inapaswa kutolewa kwa upendo na kwa njia inayofaa kwa kufikiria faida za milele za watoto.—Waebrania 12:7-11.

Furahia Tafrija Pamoja na Watoto Wako

Ni kweli kwamba ili watoto wakue vizuri, wanahitaji kucheza na kujiburudisha. Wazazi wenye hekima hutumia kila nafasi ili kuimarisha uhusiano wao pamoja na watoto wao kwa kufurahia tafrija pamoja nao inapowezekana. Hivyo, zaidi ya kuwaelekeza watoto wao kuchagua tafrija zinazofaa, wazazi wanaweza pia kuwaonyesha watoto kwamba wanathamini kuwa pamoja nao.

Baba mmoja ambaye ni Shahidi anasema kwamba mara nyingi aliporudi nyumbani kutoka kazini alicheza mpira pamoja na mvulana wake. Mama mmoja anasema kwamba watoto wake walipenda sana michezo fulani inayochezwa juu ya ubao. Mwanamke mmoja anakumbuka kwamba familia yao ilifurahia kuendesha baiskeli pamoja. Watoto wote hao sasa ni watu wazima, lakini bado upendo wao kwa wazazi wao na kwa Yehova ni wenye nguvu na unaendelea kukua.

Kwa kweli, wazazi wanaoonyesha kwa maneno na kwa matendo kwamba wanawapenda watoto wao na wanafurahia kuwa pamoja nao, hugusa mioyo ya watoto wao sana hivi kwamba watoto hawawezi kusahau jambo hilo hata wanapokuwa watu wazima. Kwa mfano, wengi wa wahitimu katika darasa moja la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) walieleza kwamba walianza kuwa na tamaa ya kufuatia huduma ya wakati wote kwa sababu wazazi wao waliwawekea kielelezo na kuwatia moyo. Huo ni urithi mzuri kama nini kwa watoto, na baraka iliyoje kwa wazazi! Ni kweli kwamba si watoto wote wanaoweza kufanya huduma ya wakati wote wanapokuwa watu wazima. Hata hivyo, watoto wote wanaweza kufaidika kutokana na wazazi wanaomwogopa na kumheshimu Mungu, ambao ni marafiki wao wa karibu zaidi na vielelezo bora kwao.—Methali 22:6; Waefeso 6:2, 3.

Wazazi Wasio na Wenzi Wanaweza Kufanikiwa

Leo, watoto wengi wanalelewa na mzazi mmoja. Ingawa ni vigumu sana kulea watoto bila mwenzi wa ndoa, mtu anaweza kufaulu. Wazazi wasio na wenzi wanaweza kutiwa moyo na mfano wa Eunike, Mkristo Myahudi wa karne ya kwanza. Akiwa na mume asiyeamini, yaelekea Eunike hakutegemezwa kiroho na mume wake. Hata hivyo, Eunike alikuwa mfano mzuri katika kumfundisha Timotheo. Kielelezo kizuri ambacho Eunike alimwekea Timotheo tangu utotoni pamoja na kielelezo cha Loisi nyanya ya Timotheo, kilikuwa na nguvu nyingi kuliko uvutano wowote wenye kudhuru ambao huenda ungetokana na marika wa Timotheo.—Matendo 16:1, 2; 2 Timotheo 1:5; 3:15.

Leo, vijana wengi wanaolelewa na mzazi asiyeamini au mzazi mmoja wanaonyesha sifa nzuri kama zile za kijana Timotheo. Kwa mfano, Ryan, ambaye sasa ana umri wa miaka 22 na ni mhudumu wa wakati wote, alilelewa na mzazi mmoja pamoja na ndugu yake mkubwa na dada yake. Baba yao alikuwa mlevi na aliacha familia yake Ryan alipokuwa na umri wa miaka minne. Ryan alisema hivi: “Mama aliazimia kwamba familia yetu ingeendelea kumtumikia Yehova, naye alitenda kulingana na azimio hilo kwa moyo wake wote.”

Pia, Ryan alisema hivi: “Kwa mfano, mama alituruhusu kushirikiana tu na watoto ambao walikuwa na uvutano mzuri. Hakuturuhusu tushirikiane na wale ambao Biblia husema kuwa mashirika mabaya, iwe nje au ndani ya kutaniko. Pia, alitufunza kuwa na maoni mazuri kuhusu elimu.” Hata ingawa mama ya Ryan alikuwa mara nyingi mwenye shughuli na alichoka kwa sababu ya kazi, hilo halikumzuia asiwaonyeshe watoto wake upendo. Ryan alisema hivi: “Sikuzote mama alitaka kuwa pamoja nasi na kuzungumza nasi. Alikuwa mwalimu mwenye subira lakini thabiti aliyefanya yote awezayo ili kuhakikisha kwamba tulikuwa na funzo la familia la Biblia kwa ukawaida. Kamwe, hangevunja kanuni za Biblia.”

Ryan anapokumbuka maisha yake ya utotoni, anatambua kwamba mtu aliyekuwa na uvutano mkubwa zaidi katika maisha yake ni mama yake ambaye alimpenda Mungu sana na watoto wake. Hivyo, enyi wazazi Wakristo, waliofunga ndoa au wajane, walio na wenzi wa ndoa Wakristo au la, msikate tamaa mnapokabili mambo yenye kuvunja moyo au matatizo ya muda mnapojitahidi kuwafundisha watoto wenu. Nyakati nyingine, huenda vijana wengine, kama yule mwana mpotevu, wakakengeuka na kuacha ukweli. Lakini watarudi wanapotambua jinsi ulimwengu ulivyo wenye ubaridi. Naam, “mwadilifu anatembea kwa utimilifu wake. Wanawe watakuwa na furaha baada yake.”—Methali 20:7; 23:24, 25; Luka 15:11-24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kuhusu mambo hayo hususa, ona ukurasa wa 55-59 wa kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Wazazi wa Yesu Walichaguliwa na Mungu

Alipomtuma Mwana wake azaliwe akiwa binadamu, Yehova alichagua kwa uangalifu wazazi wa Yesu. Inapendeza kwamba Yehova alichagua wenzi wa ndoa wanyenyekevu waliomwogopa Mungu, ambao hawakumwendekeza Yesu bali walimfundisha Neno la Mungu na umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii na kuchukua madaraka kwa uzito. (Methali 29:21; Maombolezo 3:27) Yosefu alimfunza Yesu useremala, na bila shaka, Yosefu na Maria walimpa jukumu la kuwatunza wale watoto wengine wapatao sita.—Marko 6:3.

Wakati wa Pasaka, unaweza kuwazia jinsi familia ya Yosefu ilivyofanya kazi pamoja ili kutayarisha safari yao ya kila mwaka ya kwenda Yerusalemu umbali wa kilometa 200 kwenda na kurudi bila usafiri wa kisasa. Ni kweli kwamba mpango mzuri ulihitajiwa ili familia ya watu tisa au zaidi ifunge safari ndefu kama hiyo. (Luka 2:39, 41) Licha ya matatizo hayo, bila shaka, Yosefu na Maria walithamini pindi hizo, na huenda walichukua nafasi hiyo ili kuwafundisha watoto wao kuhusu matukio ya kale ya Biblia.

Alipokuwa akikua, Yesu ‘aliendelea kujitiisha’ kwa wazazi wake, nyakati zote ‘akizidi kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.’ (Luka 2:51, 52) Naam, Yosefu na Maria walithibitika kuwa wenye kustahili kutumainiwa na Yehova. Wao ni vielelezo vizuri sana kwa wazazi leo!—Zaburi 127:3.