Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa Kikristo

Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa Kikristo

Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa Kikristo

“Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?”—MATENDO 8:36.

1, 2. Filipo alianzishaje mazungumzo pamoja na ofisa mmoja Mwethiopia, na nini kinachoonyesha kwamba mtu huyo alipendezwa na mambo ya kiroho?

MWAKA mmoja au miwili hivi baada ya kifo cha Yesu, ofisa mmoja wa serikali alikuwa akisafiri kuelekea kusini kwenye barabara iliyotoka Yerusalemu mpaka Gaza. Bado alihitaji kusafiri kilometa 1,500 hivi akitumia gari la kukokotwa. Hiyo ilikuwa safari yenye kuchosha kweli! Mtu huyo aliyemwogopa Mungu alikuwa amesafiri mbali sana, kutoka Ethiopia hadi Yerusalemu, ili kumwabudu Yehova. Alipokuwa katika safari ndefu ya kurudi, alitumia vizuri wakati wake kwa kusoma Neno la Mungu. Naam, alikuwa na imani kwelikweli. Yehova alimtambua mtu huyo mnyoofu, na kupitia malaika, Akamwongoza mwanafunzi Filipo amhubirie.—Matendo 8:26-28.

2 Ilikuwa rahisi kwa Filipo kuanzisha mazungumzo kwa kuwa ofisa huyo Mwethiopia alikuwa akisoma kwa sauti kubwa, kama ilivyokuwa desturi wakati huo. Hivyo, Filipo alimsikia akisoma kitabu cha kukunjwa cha Isaya. Filipo aliamsha upendezi wa mtu huyo kwa kuuliza swali moja rahisi: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Kisha, mazungumzo kuhusu Isaya 53:7, 8 yakaanza. Mwishowe, Filipo “akamtangazia habari njema juu ya Yesu.”—Matendo 8:29-35.

3, 4. (a) Kwa nini Filipo alimbatiza Mwethiopia huyo bila kukawia? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Kwa muda mfupi tu, Mwethiopia huyo alielewa daraka la Yesu katika kusudi la Mungu na vilevile uhitaji wa kuwa mwanafunzi aliyebatizwa wa Kristo. Mwethiopia huyo alipoona mahali penye maji karibu, alimuuliza Filipo hivi: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Bila shaka, hizo zilikuwa hali za pekee. Tayari mtu huyo mwenye imani alikuwa akimwabudu Mungu akiwa mgeuzwa-imani. Kama hangebatizwa wakati huo, basi huenda hangepata nafasi nyingine ya kubatizwa kwa muda mrefu sana. Zaidi ya yote, mtu huyo alielewa matakwa ya Mungu, na alitaka kuyatimiza kwa moyo wote. Filipo alikubali ombi lake kwa furaha, naye Mwethiopia huyo alipobatizwa “aliendelea kwenda zake akishangilia.” Inaelekea alienda kuwa mhubiri mwenye bidii wa habari njema katika nchi yao.—Matendo 8:36-39.

4 Ingawa hatua za wakfu na ubatizo hazipaswi kuchukuliwa kimchezo wala haraka-haraka, mfano wa ofisa huyo Mwethiopia unaonyesha kwamba kuna nyakati ambazo watu fulani wamebatizwa muda mfupi tu baada ya kusikia kweli ya Neno la Mungu. * Basi, inafaa kuchunguza maswali haya: Mtu anapaswa kujitayarishaje kwa ajili ya ubatizo? Ni wakati gani ambapo umri unapaswa kufikiriwa? Ni maendeleo gani ya kiroho ambayo yanapaswa kuonekana kabla mtu hajabatizwa? Zaidi ya yote, kwa nini Yehova anataka watumishi wake wachukue hatua hiyo?

Mapatano Mazito

5, 6. (a) Watu wa Mungu wa kale walionyeshaje kwamba wanathamini upendo wa Yehova? (b) Tunaweza kuwa na uhusiano gani wa karibu pamoja na Mungu baada ya kubatizwa?

5 Baada ya kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri, Yehova alikuwa tayari kuwakubali kuwa “mali [yake] ya pekee,” kuwapenda na kuwalinda na kuwafanya kuwa “taifa takatifu.” Hata hivyo, ili wapate baraka hizo, iliwabidi watu hao waonyeshe waziwazi kwamba wanathamini upendo wa Mungu. Walifanya hivyo kwa kukubali kufanya ‘yote ambayo Yehova alisema’ na kufanya agano pamoja naye. (Kutoka 19:4-9) Katika karne ya kwanza, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na wale waliokubali mafundisho yake wakabatizwa. Uhusiano mzuri pamoja na Mungu ulitegemea kumwamini Yesu Kristo kisha kubatizwa.—Mathayo 28:19, 20; Matendo 2:38, 41.

6 Masimulizi hayo ya Biblia yanaonyesha kwamba Yehova huwabariki wale wanaofanya na kutimiza mapatano mazito ya kumtumikia. Kwa Wakristo, wakfu na ubatizo ni hatua ambazo mtu anapaswa kuchukua ili apate baraka za Yehova. Tunaazimia kufuata njia zake na kutafuta mwongozo wake. (Zaburi 48:14) Tunapofanya hivyo, Yehova hushika mkono wetu na kutuongoza katika njia tunayopaswa kutembea ndani yake.—Zaburi 73:23; Isaya 30:21; 41:10, 13.

7. Kwa nini wakfu na ubatizo unapaswa kuwa uamuzi wa kibinafsi?

7 Nia yetu ya kuchukua hatua hizo inapaswa kuwa upendo kwa Yehova na tamaa ya kumtumikia. Mtu hapaswi kubatizwa eti kwa sababu mwingine amemwambia kwamba amejifunza kwa muda mrefu au kwa sababu rafiki zake wanabatizwa. Ni kweli kwamba wazazi na Wakristo wengine waliokomaa wanaweza kumhimiza mtu afikirie wakfu na ubatizo. Hata mtume Petro aliwasihi wale waliomsikiliza wakati wa Pentekoste ‘wabatizwe.’ (Matendo 2:38) Hata hivyo, kujiweka wakfu ni jambo la kibinafsi, na hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yetu. Sisi wenyewe ndio tunaopaswa kujiamulia kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 40:8.

Kujitayarisha Vizuri kwa Ajili ya Ubatizo

8, 9. (a) Kwa nini ubatizo wa watoto wachanga haupatani na Maandiko? (b) Kabla ya kubatizwa, vijana wanapaswa kufanya maendeleo gani ya kiroho?

8 Je, watoto wanaweza kuwa na hekima ya kufanya uamuzi wa kujiweka wakfu? Maandiko hayataji umri hususa wa kubatizwa. Lakini, ni wazi kwamba watoto wachanga hawawezi kuwa waamini, hawawezi kuwa na imani, wala hawawezi kujiweka wakfu kwa Mungu. (Matendo 8:12) Kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza, mwanahistoria Augustus Neander alisema hivi katika kitabu chake (General History of the Christian Religion and Church): “Mwanzoni ni watu wazima tu waliokuwa wakibatizwa, kwa kuwa kwa kawaida watu walielewa kwamba ubatizo unahusiana sana na imani.”

9 Vijana wengine husitawisha hali ya kiroho wakiwa na umri mdogo, huku wengine hufanya hivyo baada ya muda mrefu. Hata hivyo, kabla ya kubatizwa, kijana anapaswa kuwa na uhusiano pamoja na Yehova, kuelewa kwa usahihi mafundisho ya msingi ya Maandiko, na kufahamu kabisa maana ya wakfu, kama ilivyo kwa watu wazima pia.

10. Ni hatua gani zinazopaswa kutangulia wakfu na ubatizo?

10 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake kuwafundisha wapya mambo yote aliyoamuru. (Mathayo 28:20) Kwa hiyo, kwanza kabisa, wapya wanahitaji kupata ujuzi sahihi kuhusu kweli, kisha ujuzi huo utawawezesha kumwamini Yehova na Neno lake. (Waroma 10:17; 1 Timotheo 2:4; Waebrania 11:6) Halafu, kweli ya Biblia inapogusa moyo wa mtu, inamchochea kutubu na kugeuka kwa kuacha maisha yake ya zamani. (Matendo 3:19) Mwishowe, mtu huyo hutamani kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, kama vile Yesu alivyoamuru.

11. Kwa nini ni muhimu tushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri kabla ya ubatizo?

11 Hatua nyingine muhimu ya kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo ni kuhubiri habari njema ya Ufalme. Hiyo ndiyo kazi muhimu zaidi ambayo Yehova amewapa watu wake katika siku hizi za mwisho. (Mathayo 24:14) Hivyo, wahubiri ambao hawajabatizwa wanaweza kupata shangwe kwa kuwaeleza wengine yale wanayoamini. Kufanya kazi hiyo huwatayarisha pia kushiriki kwa ukawaida na kwa bidii katika huduma ya shambani baada ya ubatizo.—Waroma 10:9, 10, 14, 15.

Je, Kuna Jambo Linalokuzuia Usibatizwe?

12. Ni mambo gani ambayo huenda yakawazuia wengine wasibatizwe?

12 Huenda wengine wakasita kubatizwa kwa sababu hawataki madaraka yanayoambatana na hatua hiyo. Wanatambua kwamba ili watimize viwango vya Yehova, itawabidi wafanye mabadiliko makubwa maishani mwao. Au huenda wakaogopa kwamba itakuwa vigumu kwao kutimiza matakwa ya Mungu baada ya ubatizo. Huenda wengine wakafikiri hivi, “Labda siku moja nitafanya kosa na kutengwa na ushirika wa kutaniko.”

13. Katika siku za Yesu, ni nini kilichowazuia watu fulani wasiwe wafuasi wake?

13 Katika siku za Yesu, watu fulani waliruhusu mapendezi yao wenyewe na uhusiano wa kifamilia uwazuie wasiwe wanafunzi wake. Mwandishi fulani alisema kwamba angemfuata Yesu popote ambapo Yesu angeenda. Lakini Yesu akamwambia kwamba mara nyingi hata hana mahali pa kulala usiku. Yesu alipomwalika mtu mwingine amfuate, mtu huyo alijibu kwamba anahitaji kwanza ‘kumzika’ baba yake. Labda, alitaka kukaa nyumbani na kungoja mpaka wakati ambapo baba yake angekufa badala ya kumfuata Yesu na kushughulikia daraka hilo la kifamilia wakati ambapo lingetokea. Mwishowe, mtu wa tatu alisema kwamba kabla ya kumfuata Yesu, anahitaji kwanza ‘kuwaaga’ watu wa nyumbani mwake. Yesu alisema kwamba kuahirisha mambo kwa njia hiyo ni “kutazama mambo yaliyo nyuma.” Hivyo, inaonekana kwamba wale wanaosita kuamua hawatakosa visingizio vya kuepuka daraka lao la Kikristo.—Luka 9:57-62.

14. (a) Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana walitendaje wakati Yesu alipowaalika wawe wavuvi wa watu? (b) Kwa nini hatupaswi kusita-sita kukubali nira ya Yesu?

14 Mfano wa Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana ni tofauti sana. Yesu alipowaalika wamfuate na kuwa wavuvi wa watu, Biblia inasema hivi: “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” (Mathayo 4:19-22) Kwa kufanya uamuzi huo bila kusitasita, walijionea ukweli wa maneno ambayo Yesu aliwaambia baadaye: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:29, 30) Ingawa ubatizo huleta nira ya daraka, Yesu anatuhakikishia kwamba hiyo ni nira laini inayoweza kubebwa ambayo itatuburudisha sana.

15. Mfano wa Musa na Yeremia unaonyeshaje kwamba tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatutegemeza?

15 Bila shaka, si ajabu kwa mtu kuhisi kwamba hawezi kutimiza madaraka yanayotokana na ubatizo. Mwanzoni, Musa na Yeremia walihisi kwamba hawawezi kushughulikia migawo ambayo Yehova alikuwa amewapa. (Kutoka 3:11; Yeremia 1:6) Mungu aliwapa uhakikisho gani? Alimwambia Musa hivi: “Nitakuwa pamoja nawe.” Pia, alimwahidi Yeremia hivi: “Mimi niko pamoja nawe ili kukukomboa.” (Kutoka 3:12; Yeremia 1:8) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutegemeza. Kumpenda Mungu na kumtegemea kunaweza kutusaidia kuondoa shaka kwamba hatuwezi kutimiza wakfu wetu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Hakuna woga katika upendo, lakini upendo mkamilifu hutupa woga nje.” (1 Yohana 4:18) Mvulana mdogo anaweza kuogopa anapotembea peke yake, lakini anakuwa na uhakika anapotembea akiwa ameushika mkono wa baba yake. Vivyo hivyo, tukimtegemea Yehova kwa moyo wetu wote, anatuahidi kwamba ‘atanyoosha mapito yetu’ tunapoendelea kutembea pamoja naye.—Methali 3:5, 6.

Pindi Inayostahili Heshima

16. Kwa nini ubatizo unahusisha kumzamisha mtu kabisa ndani ya maji?

16 Kwa kawaida, hotuba ya Kimaandiko inayoeleza maana ya ubatizo wa Kikristo hutolewa kabla ya ubatizo. Mwishoni mwa hotuba hiyo, wale wanaotaka kubatizwa huombwa wafanye tangazo la hadharani la imani yao kwa kujibu yale maswali mawili ya ubatizo. (Waroma 10:10; ona sanduku kwenye ukurasa wa 22.) Kisha, wale wanaotaka kubatizwa huzamishwa ndani ya maji, kwa kufuata mfano uliowekwa na Yesu. Biblia inasema kwamba baada ya Yesu kubatizwa, ‘alipanda kutoka katika maji’ au “kutoka majini.” (Mathayo 3:16; Marko 1:10) Ni wazi kwamba Yohana Mbatizaji alimzamisha Yesu kabisa. * Kuzamishwa kabisa huonyesha badiliko kubwa ambalo tumefanya maishani, yaani, ni kana kwamba tunakufa kuhusiana na maisha yetu ya zamani na kuanza maisha mapya ya kumtumikia Mungu.

17. Watazamaji na wale wanaotaka kubatizwa wanaweza kuonyeshaje heshima wakati wa ubatizo?

17 Ubatizo ni pindi nzito na ya shangwe. Biblia inaonyesha kwamba Yesu alikuwa akisali wakati Yohana alipombatiza katika Mto Yordani. (Luka 3:21, 22) Kupatana na mfano huo, wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa kujiendesha kwa njia inayofaa wakati wa ubatizo. Kwa kuwa Biblia inatuhimiza tuvalie kwa kiasi kila siku, tunapaswa kutii shauri hilo hata zaidi siku ya ubatizo wetu! (1 Timotheo 2:9) Pia, watazamaji wanaweza kuonyesha heshima kwa kusikiliza kwa makini hotuba ya ubatizo na kutazama ubatizo kwa utaratibu.—1 Wakorintho 14:40.

Baraka Ambazo Wanafunzi Waliobatizwa Hupata

18, 19. Ubatizo huleta mapendeleo na baraka gani?

18 Tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, tunakuwa sehemu ya familia ya pekee. Kwanza kabisa, Yehova anakuwa Baba yetu na Rafiki yetu. Kabla ya ubatizo, tulikuwa tumetenganishwa na Mungu, lakini baada ya ubatizo tunapatanishwa naye. (2 Wakorintho 5:19; Wakolosai 1:20) Kupitia dhabihu ya Kristo, tumemkaribia Mungu naye anatukaribia. (Yakobo 4:8) Nabii Malaki anaeleza jinsi Yehova anavyowasikiliza wale wanaolitumia jina lake na kutambulishwa kwa jina hilo, naye anaingiza majina yao katika kitabu chake cha kumbukumbu. Mungu anasema hivi: “Nao watakuwa wangu, . . . Nami nitawaonyesha huruma, kama vile mwanamume anavyomwonyesha huruma mwana wake ambaye anamtumikia.”—Malaki 3:16-18.

19 Pia, ubatizo hutuwezesha kuwa sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote. Mtume Petro alipouliza baraka ambazo wanafunzi wa Kristo watapata kwa sababu ya kujidhabihu, Yesu aliahidi hivi: “Kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.” (Mathayo 19:29) Miaka mingi baadaye, Petro aliandika kuhusu “ushirika mzima wa akina ndugu” ambao ulikuwa umesitawi “ulimwenguni.” Petro mwenyewe alijionea utegemezo na baraka zinazotokana na undugu wenye upendo, nasi pia tunaweza kujionea mambo hayo.—1 Petro 2:17; 5:9.

20. Tunapobatizwa tunapata tumaini gani zuri?

20 Isitoshe, Yesu alionyesha kwamba wale wanaomfuata ‘watarithi uzima wa milele.’ Naam, wakfu na ubatizo hutupa tumaini la ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli,’ yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Hakuna msingi mwingine bora kuliko huo ambao tunaweza kujiwekea sisi wenyewe pamoja na familia zetu kwa ajili ya wakati ujao! Tumaini hilo zuri litatuwezesha ‘kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.’—Mika 4:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Vivyo hivyo, Wayahudi na wageuzwa-imani 3,000 waliosikiliza hotuba ya Petro wakati wa Pentekoste, walibatizwa bila kukawia. Bila shaka, kama yule towashi Mwethiopia, tayari walijua mafundisho ya msingi na kanuni za Neno la Mungu.—Matendo 2:37-41.

^ fu. 16 Kulingana na kitabu kimoja (Expository Dictionary of New Testament Words cha Vine), neno la Kigiriki baʹpti·sma (ubatizo) linamaanisha “hatua ya kuingizwa ndani ya maji, kuzamishwa na kuinuliwa.”

Je, Unaweza Kueleza?

• Tunaweza kuitikiaje upendo wa Yehova, na kwa nini tufanye hivyo?

• Mtu anapaswa kufanya maendeleo gani ya kiroho kabla ya kubatizwa?

• Kwa nini hatupaswi kusita kubatizwa kwa sababu tu ya kuogopa kwamba tutafanya kosa au kwa sababu ya kuepuka kutimiza madaraka yanayotokana na ubatizo?

• Wanafunzi waliobatizwa wa Yesu Kristo wanaweza kupata baraka gani za pekee?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ubatizo ni pindi nzito na ya shangwe