Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Lazima Uwe Mfuasi wa Kanisa Fulani?

Je, Ni Lazima Uwe Mfuasi wa Kanisa Fulani?

Je, Ni Lazima Uwe Mfuasi wa Kanisa Fulani?

‘SI LAZIMA niwe mfuasi wa kanisa fulani au niende kanisani kwa ukawaida ili nimwamini Mungu!’ Hivyo ndivyo watu wengi huhisi kuhusu kuwa wafuasi wa kanisa au tengenezo fulani la kidini. Kwa kweli, wengine huhisi kuwa karibu zaidi na Mungu wanapokuwa nje wakifurahia uumbaji kuliko wanapohudhuria ibada za kidini. Leo, watu wengi wana maoni kwamba si lazima mtu awe mfuasi wa dini au tengenezo fulani ili amwamini Mungu.

Hata hivyo, wengine wana maoni tofauti kabisa. Wanasisitiza kwamba ili mtu apate kibali cha Mungu, ni lazima awe mfuasi na pia mhudhuriaji wa kanisa fulani. Kwa hiyo, kuwa mfuasi wa dini fulani ni jambo muhimu kwa kila mtu wala si kwa wale tu wanaochunguza dini ili kupata takwimu fulani au habari nyingine. Vyovyote vile, kwa kuwa uhusiano wetu pamoja na Mungu unahusika, je, si jambo linalopatana na akili kuchunguza maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo? Kwa hiyo, tunaweza kujifunza nini katika Neno lake, Biblia, kuhusu habari hiyo?

Jinsi Mungu Alivyoshughulika na Watu Zamani

Yapata miaka 4,400 iliyopita, gharika yenye kuleta maafa iliikumba dunia nzima. Tukio hilo halingeweza kusahaulika kwa urahisi, na watu duniani pote wana hekaya kuhusu gharika hiyo katika historia yao ya mapema. Ingawa hekaya hizo zinatofautiana katika mambo madogo-madogo, zinataja mambo mengi yanayofanana, kutia ndani jambo linaloonyesha kwamba ni wanadamu wachache na wanyama waliookoka.

Je, waokokaji wa Gharika waliokoka uharibifu tu bila mpango maalumu? Biblia inaonyesha kwamba haikuwa hivyo. Ni jambo muhimu kuona kwamba, Mungu hakueleza kila mtu kuhusu Gharika hiyo. Badala yake, alimwambia Noa, ambaye aliwaonya watu walioishi wakati mmoja naye kuhusu Gharika iliyokuwa ikikaribia.—Mwanzo 6:13-16; 2 Petro 2:5.

Ili kuokoka, mtu alihitaji kujiunga na kikundi hicho chenye kutegemezana na kuwa tayari kukubali mwongozo ambao Mungu alimpa Noa. Hata wanyama waliokuwa ndani ya safina waliokoka Gharika hiyo kwa sababu ya kuwa pamoja na kikundi hicho. Noa alipewa maagizo hususa ya kufanya mipango inayofaa ili kuhifadhi wanyama.—Mwanzo 6:17–7:8.

Karne kadhaa baadaye, wazao wa Noa kupitia mwana wake Shemu walikuwa watumwa huko Misri. Hata hivyo, Mungu alikusudia kuwakomboa na kuwapeleka kwenye nchi ambayo alimwahidi babu yao Abrahamu. Kwa mara nyingine tena, si kila mtu aliyeelezwa jambo hilo, bali kwanza lilifunuliwa wale waliochaguliwa kuwa viongozi, yaani, Musa na ndugu yake, Haruni. (Kutoka 3:7-10; 4:27-31) Baada ya watu hao waliokuwa watumwa kukombolewa kutoka Misri wakiwa kikundi, walipewa Sheria ya Mungu kwenye Mlima Sinai na kufanywa kuwa taifa la Israeli.—Kutoka 19:1-6.

Waisraeli mmoja-mmoja waliweza kuokoka tu kwa sababu ya kushirikiana na kikundi hiki kilichoanzishwa na Mungu na kufuata maagizo ya viongozi wake waliowekwa rasmi. Hata mipango ilifanywa ili Wamisri mmoja-mmoja waweze kujiunga na kikundi hicho ambacho bila shaka kilikuwa na kibali cha Mungu. Waisraeli walipotoka Misri, watu hao waliandamana nao, na hivyo wakawa na tarajio la kupokea baraka za Mungu.—Kutoka 12:37, 38.

Kisha katika karne ya kwanza, Yesu alianza kazi yake ya kuhubiri na kukusanya watu pamoja wawe wanafunzi wake. Alishughulika nao wakiwa kikundi, ingawa pia alishughulika na watu mmoja-mmoja kulingana na mahitaji yao. Yesu aliwaambia hivi mitume waaminifu 11: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:28, 29) Baadaye, wanafunzi walipokuwa pamoja kama kikundi, walipokea roho takatifu ya Mungu.—Matendo 2:1-4.

Mifano hiyo inaonyesha wazi kwamba tangu zamani Mungu amekuwa akishughulika na watu wake wakiwa kikundi kilichopangwa kitengenezo. Watu wachache ambao Mungu alishughulika nao kibinafsi—Noa, Musa, Yesu, na wengine—kwa kweli walitumiwa Naye ili kuwasiliana na kikundi kilichoshirikiana kwa ukaribu. Ni wazi kwamba, Mungu hushughulika na watu wake kwa njia iyo hiyo leo. Bila shaka, swali lingine linazuka: Je, inatosha tu kushirikiana na kikundi chochote cha kidini? Tutazungumzia swali hilo muhimu katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Tangu zamani, Mungu ameshughulika na watu wake wakiwa wamepangwa kitengenezo