Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanaomtukuza Mungu Hubarikiwa

Wanaomtukuza Mungu Hubarikiwa

Wanaomtukuza Mungu Hubarikiwa

‘Watainama mbele zako, Ee Yehova, na kulipa utukufu jina lako.’ —Zaburi 86:9.

1. Kwa nini tunaweza kumtukuza Mungu kwa njia zilizo bora kuliko vitu visivyo na uhai?

YEHOVA anastahili kutukuzwa na viumbe wake wote. Ingawa vitu visivyo na uhai humtukuza kimya-kimya, sisi wanadamu tuna uwezo wa kufikiri, kuelewa, kushukuru, na kuabudu. Hivyo, maneno haya ya mtunga-zaburi yanatuhusu: “Mpigieni Mungu kelele za ushindi, enyi nyote watu wa dunia. Upigieni muziki utukufu wa jina lake. Tukuzeni sifa yake.”—Zaburi 66:1, 2.

2. Ni nani ambao wametii amri ya kulitukuza jina la Mungu, na kwa nini?

2 Wanadamu walio wengi hukataa kumtambua Mungu au kumtukuza. Hata hivyo, katika nchi 235, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita huonyesha kwamba wao huona ‘sifa za Mungu zisizoonekana’ kupitia vitu alivyovifanya na kwamba ‘wamesikia’ ushahidi wa kimya-kimya wa uumbaji. (Waroma 1:20; Zaburi 19:2, 3) Kwa kujifunza Biblia, wao pia wamemjua na kumpenda Yehova. Zaburi 86:9, 10 ilitabiri hivi: “Mataifa yote ambayo umeyafanya, yatakuja yenyewe, nayo yatainama mbele zako, Ee Yehova, na kulipa utukufu jina lako. Kwa maana wewe ni mkuu na unafanya mambo ya ajabu; wewe ni Mungu, wewe peke yako.”

3. “Umati mkubwa” hutoaje “utumishi mtakatifu mchana na usiku”?

3 Vivyo hivyo, andiko la Ufunuo 7:9, 15 linataja “umati mkubwa” wa waabudu kuwa “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” Hiyo haimaanishi kwamba Mungu hutaka watumishi wake wamtukuze mfululizo, lakini waabudu wake ni tengenezo la duniani pote. Hivyo, inapokuwa usiku katika nchi fulani, watumishi wa Mungu katika upande mwingine wa dunia huendelea kutoa ushahidi kwa bidii. Kwa hiyo, inaweza kusemwa kwamba kuna wale wanaomtukuza Yehova mchana na usiku. Hivi karibuni, “kila kitu kinachopumua” kitapaaza sauti kumtukuza Yehova. (Zaburi 150:6) Lakini tunaweza kufanya nini sasa ili kumtukuza Mungu? Huenda tukapata matatizo gani? Nao wanaomtukuza Mungu watapata baraka zipi? Ili kupata jibu, acheni tuchunguze masimulizi ya Biblia kuhusu kabila la Israeli la Gadi.

Tatizo la Kale

4. Kabila la Gadi lilikabili magumu gani?

4 Kabla ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, kabila la Israeli la Gadi liliomba liruhusiwe kuishi katika eneo la malisho, mashariki ya Yordani. (Hesabu 32:1-5) Kuishi katika eneo hilo kungemaanisha kwamba wangekabili hali ngumu sana. Makabila yaliyokuwa magharibi yangekingwa na Bonde la Yordani ambalo lilikuwa kizuizi cha asili kwa shambulizi la kijeshi. (Yoshua 3:13-17) Hata hivyo, kichapo The Historical Geography of the Holy Land, cha George Adam Smith, kinasema hivi kuhusu maeneo yaliyo mashariki ya Yordani: ‘Maeneo hayo yote ni tambarare, nayo yamesambaa juu ya uwanda mkubwa wa juu wa Uarabuni. Hivyo, yamekuwa yakishambuliwa kila mara na wahama-hamaji wenye njaa, ambao baadhi yao hufurika katika maeneo hayo kila mwaka wakitafuta malisho.’

5. Yakobo aliwatia moyo wazao wa Gadi wafanye nini wakishambuliwa?

5 Kabila la Gadi lingekabilianaje na tatizo hilo lenye kuendelea? Alipokaribia kufa, babu yao Yakobo alitabiri hivi: “Naye Gadi, atavamiwa na kikundi cha waporaji, lakini yeye atavamia upande wa nyuma kabisa.” (Mwanzo 49:19) Yakichukuliwa kijuujuu huenda maneno hayo yakaonekana kuwa yenye kuhuzunisha. Hata hivyo, ukweli ni kwamba wazao wa Gadi waliamuriwa walipize kisasi. Yakobo aliwahakikishia kwamba kama wangefanya hivyo, wavamizi hao wangerudi nyuma kwa aibu, nao wazao wa Gadi wangewafuatia upande wa nyuma kabisa.

Matatizo Tunayokabili Katika Ibada Yetu Leo

6, 7. Leo hali ya Wakristo inafananaje na ile ya kabila la Gadi?

6 Kama vile kabila la Gadi, leo Wakristo wanakabili hali ngumu na matatizo ya mfumo wa Shetani; hatukingwi kimuujiza tusikabiliane nayo. (Ayubu 1:10-12) Wengi wetu tunakabiliana na magumu shuleni, tunapotafuta riziki, na kulea watoto. Pia kuna magumu ya kibinafsi. Wengine wanalazimika kuvumilia “mwiba katika mwili” ambao ni ulemavu au ugonjwa mbaya. (2 Wakorintho 12:7-10) Wengine wanasumbuliwa na hisia za kujidharau. Huenda “siku zenye msiba” za uzee zikawazuia Wakristo walio wazee wasimtumikie Yehova kwa nguvu kama zamani.—Mhubiri 12:1.

7 Mtume Paulo pia anatukumbusha kwamba “tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Tunakabiliana daima na “roho ya ulimwengu,” roho ya uasi na upotovu wa maadili ambayo Shetani na roho wake waovu huendeleza. (1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2, 3) Kama Loti mwenye kumwogopa Mungu, leo huenda tukahuzunishwa na mambo yasiyo ya adili ambayo watu wanaotuzunguka husema na kufanya. (2 Petro 2:7) Pia tunakabili shambulio la Shetani la moja kwa moja. Shetani anapigana vita na mabaki ya watiwa-mafuta, ‘ambao wanashika amri za Mungu na wana kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.’ (Ufunuo 12:17) Pia “kondoo wengine” wa Yesu hushambuliwa na Shetani kupitia marufuku na mateso.—Yohana 10:16.

Je, Utakubali Kushindwa au Utapambana?

8. Tunapaswa kufanyaje tunaposhambuliwa na Shetani?

8 Tunapaswa kufanyaje tunaposhambuliwa na Shetani? Kama kabila la kale la Gadi, ni lazima tuwe na nguvu kiroho na kupambana kupatana na mwongozo wa Mungu. Inasikitisha kwamba wengine wameanza kushindwa na magumu ya maisha na kupuuza madaraka yao ya kiroho. (Mathayo 13:20-22) Akieleza sababu inayofanya hudhurio la mikutano liwe chini, Shahidi mmoja alisema: “Ndugu wamechoka tu. Wote wana mikazo mikali sana.” Kwa kweli, leo watu wana sababu nyingi zinazowafanya wachoke. Kwa hiyo, ni rahisi kuona ibada ya Mungu kuwa takwa lingine lenye kuchosha. Lakini je, hayo ni maoni yafaayo, au yaliyo sahihi?

9. Kuchukua nira ya Kristo hutuleteaje burudiko?

9 Fikiria yale ambayo Yesu aliuambia umati katika siku zake ambao pia ulikuwa umechoshwa na magumu ya maisha: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” Je, Yesu alimaanisha kwamba mtu angepata burudiko kwa kupunguza utumishi wake kwa Mungu? Kinyume cha hilo, Yesu alisema: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Nira ni kiunzi cha mbao au chuma ambacho humwezesha mwanadamu au mnyama kubeba kitu kizito. Basi, kwa nini mtu atake kuchukua nira kama hiyo? Je, si tayari ‘tumelemewa na mizigo’? Ndiyo, lakini maandishi ya Kigiriki yanaweza pia kusomeka hivi: “Jiwekeni chini ya nira yangu pamoja nami.” Ebu wazia: Yesu anajitoa kutusaidia kuvuta mzigo wetu! Hatuhitaji kufanya hivyo kwa nguvu zetu wenyewe.—Mathayo 9:36; 11:28, 29; 2 Wakorintho 4:7.

10. Jitihada zetu za kumtukuza Mungu zina matokeo gani?

10 Tunapochukua nira ya kuwa wanafunzi wa Yesu, tunapigana na Shetani. “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi,” linaahidi andiko la Yakobo 4:7. Hiyo haimaanishi kwamba ni rahisi kufanya hivyo. Jitihada nyingi zinahitajiwa ili kumtumikia Mungu. (Luka 13:24) Lakini Biblia inatoa ahadi hii kwenye Zaburi 126:5: “Wale wanaopanda mbegu kwa machozi watavuna kwa vigelegele vya shangwe.” Naam, sisi huabudu Mungu mwenye shukrani. Yeye “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii,” naye huwabariki wale wanaomtukuza.—Waebrania 11:6.

Kumtukuza Mungu Tukiwa Wahubiri wa Ufalme

11. Huduma ya shambani hutukingaje na mashambulizi ya Shetani?

11 Yesu aliamuru: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Kazi ya kuhubiri ndiyo njia kuu ya kumtolea Mungu “dhabihu ya sifa.” (Mathayo 28:19; Waebrania 13:15) ‘Kuvaa miguuni mwetu viatu vya habari njema ya amani’ ni sehemu muhimu sana ya “mavazi kamili ya silaha,” yaani, kinga yetu dhidi ya mashambulizi ya Shetani. (Waefeso 6:11-15) Kumtukuza Mungu katika huduma ya shambani ni njia nzuri ya kuimarisha imani yetu. (2 Wakorintho 4:13) Huduma hiyo hutusaidia tusifikirie mambo yasiyofaa. (Wafilipi 4:8) Kushiriki katika huduma ya shambani hutuwezesha kufurahia ushirika wenye kujenga pamoja na waabudu wenzetu.

12, 13. Kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani kunawezaje kunufaisha familia? Toa mfano.

12 Kazi ya kuhubiri inaweza pia kuwa utendaji unaojenga familia. Ni kweli kwamba vijana wanahitaji tafrija yenye usawaziko. Hata hivyo, wakati ambao familia inatumia katika huduma ya shambani haupaswi kuwa wenye kuchosha. Wazazi wanaweza kufanya wakati huo uwe wenye kufurahisha zaidi kwa kuwazoeza watoto wao wawe wenye matokeo katika huduma. Vijana hufurahia mambo wanayoweza kufanya vizuri. Wazazi wanaweza kuwasaidia vijana wapate furaha katika huduma kwa kuwa na usawaziko, na kutowasukuma kupita uwezo wao.—Mwanzo 33:13, 14.

13 Pia, familia inayomtukuza Mungu pamoja huwa na uhusiano wa karibu. Fikiria dada mmoja ambaye mume wake asiyeamini alimwacha na watoto watano. Alikabili tatizo la kufanya kazi ya kuajiriwa na la kuwaandalia kimwili watoto wake watano. Je, alichoka sana hivi kwamba alipuuza masilahi ya kiroho ya watoto wake? Yeye anakumbuka: “Nilijifunza kwa bidii Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia na kujitahidi kutumia yale niliyojifunza. Nilienda na watoto mikutanoni na katika huduma ya nyumba kwa nyumba kwa ukawaida. Matokeo ya jitihada zangu yalikuwaje? Watoto wote watano wamebatizwa.” Kushiriki kikamili katika huduma kunaweza kukusaidia pia katika jitihada zako za kulea watoto wako “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

14. (a) Vijana wanawezaje kumtukuza Mungu shuleni? (b) Ni nini kinachoweza kuwasaidia vijana ‘wasiionee aibu habari njema’?

14 Enyi vijana, ikiwa mnaishi katika nchi ambako sheria inaruhusu kuhubiri hadharani, je, mnamtukuza Mungu kwa kuhubiri shuleni, au kuogopa wanadamu kunawazuia? (Methali 29:25) Msichana mmoja Shahidi mwenye umri wa miaka 13 huko Puerto Riko anaandika: “Sijawahi kamwe kuona aibu kuhubiri shuleni kwa kuwa ninajua huu ndio ukweli. Sikuzote mimi huinua mkono darasani na kueleza mambo niliyojifunza katika Biblia. Ninapokuwa na wakati, mimi huenda kwenye maktaba kusoma kitabu Vijana Huuliza.” * Je, Yehova amebariki jitihada zake? Yeye anasema: “Wakati mwingine wanadarasa wenzangu huniuliza maswali na hata huniomba nakala ya kitabu hicho.” Ikiwa umekuwa ukisita kufanya hivyo, labda unahitaji kujihakikishia “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Unapokuwa na hakika kwamba yale ambayo umejifunza ni ukweli, basi ‘hutaionea aibu kamwe habari njema.’—Waroma 1:16.

‘Mlango Uliofunguliwa’ wa Utendaji

15, 16. Wakristo fulani wameingia katika ‘mlango gani mkubwa unaoongoza kwenye utendaji,’ nao wamepata baraka gani?

15 Mtume Paulo aliandika kwamba alikuwa amefunguliwa “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.” (1 Wakorintho 16:9) Je, hali zako zinakuwezesha kupanua utendaji wako? Kwa mfano, ili kufanya upainia wa kawaida au upainia msaidizi unahitaji kuhubiri muda wa saa 70 au 50 kwa mwezi. Kwa kawaida, mapainia huthaminiwa na Wakristo wenzao kwa utumishi wao wa uaminifu. Lakini wao hawahisi kuwa bora kuliko ndugu na dada zao eti kwa sababu wanatumia muda mwingi zaidi katika huduma. Bali, wao husitawisha mtazamo huu ambao Yesu alitutia moyo tuwe nao: “Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Jambo ambalo tumefanya ndilo tulilopaswa kufanya.”—Luka 17:10.

16 Ili kupainia mtu anahitaji kujitia nidhamu, kuwa na mpango mzuri, na kuwa tayari kujidhabihu. Hata hivyo, baraka tunazopata hufanya jitihada hizo zifae. “Ni baraka kwelikweli kuwa na uwezo wa kulitumia sawasawa Neno la Mungu la kweli,” akasema painia mmoja kijana aitwaye Tamika. “Unapofanya upainia, unatumia Biblia sana. Sasa ninapoenda nyumba kwa nyumba, ninaweza kufikiria maandiko yanayomfaa kila mwenye nyumba.” (2 Timotheo 2:15) Painia aitwaye Mica anasema: “Kuona jinsi ukweli unavyoathiri maisha ya watu ni baraka nyingine yenye kutokeza.” Pia kijana aitwaye Matthew anataja furaha ya “kuona mtu akiukubali ukweli. Hakuna jambo lingine linaloweza kukuletea furaha kama hiyo.”

17. Mkristo mmoja alishindaje hisia zisizofaa kuhusu upainia?

17 Je, unaweza kufikiria kuanza upainia? Labda ungependa kufanya hivyo lakini unahisi kuwa hufai. “Nilikuwa na hisia zisizofaa kuhusu upainia,” anakiri dada mmoja kijana aitwaye Kenyatte. “Nilihisi kwamba siwezi kufanya upainia. Sikujua jinsi ya kutayarisha matangulizi wala kutoa sababu kwa kutumia Maandiko.” Hata hivyo, wazee walimpa dada painia mkomavu mgawo wa kuhubiri naye. “Nilifurahia kuhubiri naye,” Kenyatte anasema. “Jambo hilo lilinichochea nitake kufanya upainia.” Labda ukitiwa moyo na kuzoezwa, wewe pia utataka kufanya upainia.

18. Huenda wale wanaojiunga na utumishi wa umishonari wakapata baraka gani?

18 Kufanya upainia kunaweza kukusaidia ufikie mapendeleo mengine ya utumishi. Kwa mfano, huenda wenzi fulani wa ndoa wakastahili kuzoezwa kazi ya umishonari ili watumwe kuhubiri katika nchi za kigeni. Lazima mishonari wazoeleane na maisha na labda lugha, utamaduni, na vyakula vya nchi ambako wametumwa. Lakini baraka wanazopata hufanya magumu hayo yawe si kitu. Mildred, ambaye amefanya umishonari kwa muda mrefu huko Mexico anasema: “Sijawahi kujuta kwamba nilifanya uamuzi wa kuwa mishonari. Nilitamani kuwa mishonari tangu nilipokuwa msichana mdogo.” Amefurahia baraka gani? “Katika nchi ninakotoka, ilikuwa vigumu kupata funzo la Biblia. Hapa Mexico, nyakati nyingine nimekuwa na wanafunzi wanne hivi wa Biblia ambao wameanza kuhubiri wakati uleule!”

19, 20. Wengi wamenufaikaje na utumishi wa Betheli, utumishi wa kimataifa, na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma?

19 Walio katika utumishi wa Betheli kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova hupata baraka nyingi. Sven, ndugu kijana anayetumikia huko Ujerumani anasema hivi kuhusu kazi anayofanya Betheli: “Ninahisi kwamba ninafanya kazi yenye thamani ya kudumu. Ningeweza kutumia ustadi wangu katika ulimwengu. Lakini hiyo ingekuwa kama kuweka pesa katika benki ambayo iko karibu kufilisika.” Ni kweli kwamba kutumikia kama mjitoleaji asiyelipwa huhusisha kujidhabihu. Lakini Sven anasema: “Unapoenda nyumbani, unajua kwamba kila kitu ulichofanya siku hiyo ulimfanyia Yehova. Na hilo hukufanya uhisi vizuri sana.”

20 Ndugu fulani wamefurahia baraka za utumishi wa kimataifa, wakifanya kazi ya ujenzi katika nchi mbalimbali za kigeni. Ndugu mmoja na mke wake ambao wametumika katika migawo minane mbalimbali katika nchi za kigeni waliandika: “Ndugu hapa ni wazuri sana. Tunahuzunika sana kuondoka na hii ndiyo mara ya nane tumehuzunika. Tumefurahia sana sana kazi yetu!” Halafu kuna Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Shule hiyo hutoa mazoezi ya kiroho kwa ndugu waseja wanaostahili. Mhitimu mmoja wa shule hiyo aliandika: “Sijui nisemeje ili kuwashukuru kwa shule hiyo nzuri. Ni tengenezo gani lingine linaloweza kujitahidi hivyo ili kuzoeza watu?”

21. Wakristo wote hukabili tatizo gani katika kumtumikia Mungu?

21 Naam, kuna milango mingi ya utendaji ambayo imefunguliwa. Ni kweli kwamba wengi wetu hatuwezi kutumika Betheli au katika nchi ya kigeni. Yesu mwenyewe alisema kwamba Wakristo wangetokeza “matunda” kwa viwango tofauti-tofauti kwa sababu hali zao ni tofauti. (Mathayo 13:23) Basi, tukiwa Wakristo tunakabili tatizo la kutumia hali zetu vizuri tuwezavyo, yaani, kumtumikia Yehova kadiri tuwezavyo kulingana na hali zetu. Tunapofanya hivyo, tunamtukuza Yehova, na tunaweza kuwa na hakika kwamba anafurahi sana. Fikiria Ethel, dada mzee katika hospitali ndogo ya binafsi. Yeye huwahubiria kwa ukawaida watu anaokaa nao katika hospitali hiyo na pia huhubiri kupitia simu. Licha ya kupungukiwa kwake, yeye hutumikia kwa nafsi yote.—Mathayo 22:37.

22. (a) Tunaweza kumletea Mungu utukufu katika njia nyingine zipi? (b) Tunatazamia wakati gani mzuri?

22 Hata hivyo, kumbuka kwamba kuhubiri ni mojawapo tu ya njia tunazoweza kumtukuza Yehova. Kwa kujiendesha na kujipamba vizuri tunapokuwa kazini, shuleni, na nyumbani, tunamfurahisha Yehova. (Methali 27:11) Methali 28:20 inaahidi: “Mtu mwenye matendo ya uaminifu atapata baraka nyingi.” Kwa hiyo, tunapaswa ‘kupanda kwa wingi’ katika utumishi wetu kwa Mungu, tukijua kwamba tutavuna baraka nyingi. (2 Wakorintho 9:6) Kwa kufanya hivyo, tutakuwa na pendeleo la kuwa hai wakati huo mzuri ambapo “kila kitu kinachopumua” kitampa Yehova utukufu ambao anastahili sana kupewa!—Zaburi 150:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi huchapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Watu wa Yehova humtumikiaje “mchana na usiku”?

• Kabila la Gadi lilikabili magumu gani, na leo jambo hilo huwafunza Wakristo nini?

• Huduma ya shambani hutukingaje na mashambulizi ya Shetani?

• Wengine wameingia ‘mlango gani uliofunguliwa,’ nao wamepata baraka gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama vile wazao wa Gadi walivyopigana na vikundi vya waporaji, Wakristo wanapaswa kupambana na mashambulizi ya Shetani

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tunafurahia ushirika wenye kujenga katika huduma ya shambani

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kufanya upainia kunaweza kukusaidia ufikie mapendeleo mengine ya utumishi, kutia ndani:

1. Utumishi wa kimataifa

2. Utumishi wa Betheli

3. Utumishi wa mishonari