Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutenda Mema Nyakati za Uhitaji

Kutenda Mema Nyakati za Uhitaji

Kutenda Mema Nyakati za Uhitaji

MTUME Paulo alihimiza hivi: “Tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hujitahidi kufuata kanuni hiyo maishani mwao, wakiwatendea wote mema, hasa waamini wenzao. Wao hufanya hivyo tena na tena nyakati za uhitaji. Na tuchunguze mifano ya hivi karibuni kutoka nchi tatu.

Mnamo Desemba 2002, kimbunga kikali kilichokuwa kikisafiri kwa mwendo wa kilometa zaidi ya 300 kwa saa kilikumba Guam. Nyumba nyingi zilibomolewa, nazo nyingine zikaharibiwa kabisa. Mara moja makutaniko ya huko yalipanga kuwe na vikundi vya kuondoa uchafu ili kusaidia familia za Mashahidi zilizoathiriwa zaidi. Ofisi ya tawi ya Guam ilituma vifaa na wafanyakazi wa kurekebisha nyumba zilizoharibiwa, nayo ofisi ya tawi ya Hawaii ikaunga mkono kazi hiyo. Baada ya majuma machache, kikundi cha maseremala kiliwasili kutoka Hawaii ili kusaidia kazi ya kujenga nyumba upya. Nao ndugu kadhaa wenyeji wakachukua likizo ili kuwasaidia ndugu hao wa Hawaii. Roho ya ushirikiano ilitoa ushahidi katika eneo hilo lote.

Katika kitongoji kimoja cha jiji la Mandalay, Myanmar, moto ulizuka karibu na Jumba la Ufalme. Dada mmoja asiyetenda na familia yake waliishi katika nyumba iliyokuwa karibu na jumba hilo. Upepo ulikuwa ukivuma kuelekea nyumba yake, kwa hiyo akakimbia kwenye jumba hilo ili kuomba msaada. Wakati huo, jumba lilikuwa likirekebishwa, hivyo kulikuwa na ndugu wengi. Walishangaa kumwona dada huyo kwa sababu hawakujua kwamba aliishi katika eneo hilo. Upesi ndugu walisaidia kuhamisha familia hiyo pamoja na vitu vyao hadi mahali salama. Wakati mume, asiyekuwa Shahidi, aliposikia kuhusu moto huo, alikimbia nyumbani na kuwapata akina ndugu wakishughulikia familia yake. Alivutiwa sana na kushukuru, na pia akapata kitulizo kwa kuwa mara nyingi wezi hutumia hali kama hizo kupora. Tendo hilo la fadhili la akina ndugu lilimchochea dada huyo pamoja na mwana wake waanze kushirikiana tena na kutaniko la Kikristo, na sasa wanahudhuria mikutano yote.

Katika mwaka wa utumishi uliopita, watu wengi nchini Msumbiji walikabiliwa na njaa kwa sababu ya ukame na kuharibika kwa mazao. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo ilichukua hatua mara moja ya kuwapa chakula wenye uhitaji. Chakula kiligawanywa katika Majumba ya Ufalme, nyakati nyingine baada ya mikutano ya kutaniko. Dada mmoja ambaye ni mzazi asiye na mwenzi alisema: “Nilikuja mikutanoni nikiwa nimevunjika moyo bila kujua watoto wangu wangekula nini baada ya kurudi nyumbani.” Alitiwa moyo mara moja na msaada wa upendo aliopata kutoka kwa akina ndugu. “Kwangu huo ulikuwa kama ufufuo!” akasema.

Pia Mashahidi ‘hutenda mema’ kwa njia ya kiroho kwa kuwaeleza wengine ujumbe wa Biblia wenye faraja na tumaini. Sawa na mtu wa kale mwenye hekima, wao wanaamini hivi: ‘Kwa habari yake mtu anayesikiliza hekima ya kimungu, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.’—Methali 1:33.

[Picha katika ukurasa wa 31]

1, 2. Wenye uhitaji wagawiwa chakula huko Msumbiji

3, 4. Kimbunga kilichokumba Guam kiliharibu nyumba nyingi

[Hisani]

Child, left: Andrea Booher/FEMA News Photo; woman, above: AP Photo/Pacific Daily News, Masako Watanabe