Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Magereza Yenye Giza Hadi Milima ya Alps ya Uswisi

Kutoka Magereza Yenye Giza Hadi Milima ya Alps ya Uswisi

Simulizi la Maisha

Kutoka Magereza Yenye Giza Hadi Milima ya Alps ya Uswisi

LIMESIMULIWA NA LOTHAR WALTHER

Baada ya kukaa miaka mitatu iliyoonekana kuwa mirefu katika magereza ya Kikomunisti yenye giza ya Ujerumani Mashariki, nilitamani sana kufurahia uhuru wenye kuburudisha na ushirika mchangamfu wa familia yangu.

HATA hivyo, sikuwa tayari kumtazama mwanangu Johannes, mwenye umri wa miaka sita, aliyeonekana kutatanika. Hakuniona katika miaka yake mitatu ya kwanza. Machoni pake, nilikuwa mgeni kabisa.

Tofauti na mwanangu, nilipokuwa mtoto nilifurahia ushirika wenye upendo wa wazazi wangu. Kulikuwa na hali changamfu katika nyumba yetu huko Chemnitz, Ujerumani, ambako nilizaliwa mwaka wa 1928. Baba yangu alionyesha waziwazi kwamba hakupendezwa na dini. Alikumbuka kwamba wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, askari “Wakristo” wa kila upande waliwatakia wale wa upande mwingine “Heri ya Krismasi” mnamo Desemba 25, kisha wakaanza kuuana tena siku iliyofuata. Aliona dini kuwa aina ya unafiki iliyo mbaya zaidi.

Imani Baada ya Kukatishwa Tamaa

Ninafurahi kwamba sikupatwa na hali hiyo yenye kuvunja moyo. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilimalizika nikiwa na umri wa miaka 17, hivyo nikaponea chupuchupu kuandikishwa jeshini. Hata hivyo, nilisumbuliwa na maswali haya yenye kutatanisha, ‘Kwa nini watu wanauana? Ninaweza kumtumaini nani? Ninaweza kupata wapi usalama wa kweli?’ Ujerumani Mashariki tulikoishi iliwekwa chini ya utawala wa Sovieti. Malengo ya Kikomunisti kuhusu haki, usawa, umoja, na uhusiano wenye amani yaliwavutia wale waliochoshwa na maafa ya vita. Muda si muda, wengi kati ya watu hao wanyoofu wangekatishwa tamaa sana—wakati huu, si na dini, bali na siasa.

Wakati nilipokuwa nikifanya utafiti ili kupata majibu yafaayo, mmoja wa shangazi zangu, ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova, alizungumza nami kuhusu imani yake. Alinipa kichapo kinachozungumzia Biblia ambacho kilinichochea kusoma kwa mara ya kwanza sura yote ya 24 ya kitabu cha Mathayo. Nilivutiwa na maelezo ya akili na yenye kusadikisha ya kitabu hicho, ambayo yaliutambulisha wakati wetu kuwa “umalizio wa mfumo wa mambo” na kuonyesha kisababishi cha msingi cha matatizo ya wanadamu.—Mathayo 24:3; Ufunuo 12:9.

Muda si muda, nilipokea vichapo zaidi vya Mashahidi wa Yehova na nilipovisoma kwa hamu, nilitambua kwamba nilikuwa nimepata ukweli ambao nilikuwa nimeutafuta kwa bidii sana. Nilipendezwa kujua kwamba Yesu Kristo alikuwa ametawazwa mbinguni mwaka wa 1914 na kwamba karibuni angewaadhibu watu wasiomwogopa Mungu ili kuleta baraka kwa wanadamu watiifu. Kwa upande wangu, jambo lingine kuu nililopata kufahamu waziwazi lilihusu fidia. Ufahamu huo ulinisaidia kumkaribia Yehova Mungu kwa moyo mnyoofu katika sala ili kuomba msamaha. Niliguswa moyo na mwaliko wenye fadhili upatikanao katika Yakobo 4:8: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”

Licha ya shauku nyingi kwa sababu ya imani yangu mpya, mwanzoni wazazi wangu na dada yangu mkubwa walisita kukubali yale niliyowaambia. Hata hivyo, hilo halikupunguza tamaa yangu ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo iliyofanywa na kikundi kidogo cha Mashahidi karibu na Chemnitz. Nilishangaa, wakati wazazi wangu na dada yangu walipoenda pamoja nami katika mkutano wa kwanza! Hilo lilitendeka wakati wa majira ya baridi kali ya 1945/1946. Baadaye, wakati kikundi cha funzo la Biblia kilipoanzishwa huko Harthau tulikoishi, familia yetu ilianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.

“Mimi Ni Mvulana Tu”

Kujifunza kweli muhimu za Biblia na kushirikiana kwa ukawaida na watu wa Yehova kulinichochea kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mnamo Mei 25, 1946. Nilifurahi sana wakati washiriki wa familia yetu pia walipofanya maendeleo ya kiroho, na mwishowe wote watatu wakawa Mashahidi waaminifu. Bado dada yangu ni mshiriki mwenye bidii wa kutaniko la Chemnitz. Mama na baba yangu walitumikia kwa uaminifu hadi kifo—baba, mwaka wa 1965, naye mama mwaka wa 1986.

Miezi sita baada ya kubatizwa, nilianza kutumikia nikiwa painia wa pekee. Huo ulikuwa ndio mwanzo wa utumishi ‘katika majira yanayofaa, na katika majira yenye taabu.’ (2 Timotheo 4:2) Muda si muda, nafasi mpya za utumishi zilijitokeza. Kulikuwa na uhitaji wa wahubiri wa wakati wote katika sehemu ya mbali huko mashariki mwa Ujerumani. Mimi na Shahidi mwingine tulijaza fomu kwa ajili ya mgawo huo, lakini nilihisi kwamba sikuwa na uzoefu wala ukomavu wa kiroho kwa ajili ya daraka hilo. Kwa kuwa nilikuwa na umri wa miaka 18 tu, nilihisi kama Yeremia: “Ole wangu, . . . Yehova! Tazama, mimi hakika sijui jinsi ya kusema, kwa sababu mimi ni mvulana tu.” (Yeremia 1:6) Licha ya kuwa na shaka, ndugu wenye madaraka waliamua kwa fadhili kutuomba tujaribu kufanya mgawo huo. Hivyo, tukapewa mgawo wa kwenda Belzig, mji mdogo katika wilaya ya Brandenburg.

Ilikuwa vigumu sana kuhubiri katika eneo hilo, lakini hayo yalikuwa mazoezi muhimu kwangu. Wakati huo, wanabiashara wanawake wengi mashuhuri walikubali ujumbe wa Ufalme na kuwa Mashahidi wa Yehova. Lakini msimamo wao ulikuwa kinyume cha desturi za wenyeji zilizokita mizizi na shaka zao kuhusu jambo lolote jipya. Makasisi Wakatoliki na Waprotestanti walitupinga vikali na kufanya mashtaka ya uchongezi dhidi yetu kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. Lakini kwa kuwa tulitumaini uongozi na ulinzi wa Yehova, tuliweza kusaidia watu kadhaa waliopendezwa wajifunze ukweli.

Hali ya Kutovumiliana Yazidi Kuwa Mbaya

Mwaka wa 1948 ulikuwa wenye baraka na pia wenye matatizo yasiyotazamiwa. Kwanza, nilipokea mgawo wa upainia jijini Rudolstadt, Thuringia. Nikiwa huko nilijuana na ndugu na dada wengi waaminifu, nami nilifurahia ushirika wao. Nilipata baraka nyingine muhimu mnamo Julai mwaka huohuo. Nilifunga ndoa na Erika Ullmann, mwanamke kijana Mkristo mwaminifu na mwenye bidii ambaye nilimfahamu tangu nilipoanza kuhudhuria mikutano katika Kutaniko la Chemnitz. Tulianza utumishi wa upainia pamoja huko Harthau, mji wangu wa nyumbani. Hata hivyo, wakati huo, Erika hakuweza kuendelea na utumishi wa wakati wote kwa sababu ya matatizo ya afya na sababu nyingine pia.

Hizo zilikuwa nyakati ngumu kwa watu wa Yehova. Katika jitihada za kunilazimisha niache kazi ya kuhubiri na kutafuta kazi ya wakati wote, Idara ya Kazi huko Chemnitz ilifuta kadi yangu ya posho. Ndugu wenye madaraka walitumia kesi yangu kuomba tutambuliwe kisheria na Serikali. Ombi hilo lilikataliwa, na mnamo Juni 23, 1950, nilihukumiwa kulipa faini au kufungwa gerezani siku 30. Tulikata rufani ya uamuzi huo, lakini mahakama kuu ikaitupilia mbali nami nikatupwa gerezani.

Tukio hilo lilionyesha kidogo tu upinzani na magumu yenye kuongezeka yaliyokuwa mbele. Mnamo Septemba 1950, hata kabla ya mwezi mmoja kwisha, utawala wa Kikomunisti ulipiga kazi yetu marufuku baada ya kuanzisha kampeni ya kutushutumu katika vyombo vya habari. Kwa sababu ya ongezeko la haraka na msimamo wetu wa kutokuwamo, tulionekana kuwa kikundi hatari cha ujasusi kutoka nchi za Magharibi ambacho kiliendesha “kazi yenye kutiliwa shaka” huku kikisingizia kuwa kikundi cha kidini. Siku hiyohiyo marufuku ilipotangazwa, mke wangu alimzaa mwana wetu, Johannes, akiwa nyumbani, nami nikiwa gerezani. Licha ya mzalishaji kukataa, maofisa wa Usalama wa Serikali waliingia kwa nguvu nyumbani kwetu na kutafuta ushuhuda ili kuthibitisha mashtaka yao. Bila shaka, hawakupata chochote. Hata hivyo, walifanikiwa kuingiza mpelelezi katika kutaniko letu. Jambo hilo lilifanya ndugu wote wenye madaraka, kutia ndani mimi, wakamatwe mnamo Oktoba 1953.

Katika Magereza Yenye Giza

Baada ya kupatikana na hatia na kufungwa kati ya miaka mitatu hadi sita, tuliungana na ndugu zetu kadhaa katika magereza machafu ya Osterstein Castle, huko Zwickau. Licha ya hali mbaya huko, tulifurahi kwelikweli kushirikiana na ndugu wakomavu. Tulikosa uhuru lakini hatukukosa chakula cha kiroho. Ingawa tulidharauliwa na kupigwa marufuku na serikali, gazeti Mnara wa Mlinzi liliingia gerezani na hata ndani ya vyumba vyetu! Jinsi gani?

Baadhi ya ndugu wafungwa walipewa kazi katika migodi ya makaa, ambako walikutana na Mashahidi kutoka nje ambao waliwapa magazeti. Kisha ndugu hao wafungwa wakayaingiza kisiri-siri gerezani, na hivyo kwa werevu wakafanikiwa kupitisha chakula cha kiroho ambacho wengi wetu walihitaji. Katika njia hiyo, nilifurahi sana na kutiwa moyo kuona mwongozo wa Yehova na jinsi anavyotujali!

Mwishoni mwa mwaka wa 1954, tulihamishwa kwenda gereza la Torgau lililokuwa na sifa mbaya sana. Mashahidi huko walifurahi kutukaribisha. Kufikia hapo, walikuwa wamedumisha nguvu zao za kiroho kwa kukariri yale ambayo wangeweza kukumbuka katika makala za zamani za Mnara wa Mlinzi. Walitamani sana kupata chakula kipya cha kiroho. Sasa tulikuwa na daraka la kuwaeleza mambo muhimu tuliyojifunza huko Zwickau. Lakini tungewezaje kufanya hivyo kwa kuwa tulikuwa tumekatazwa kabisa kuzungumza mtu na mwenzake wakati wa matembezi yetu ya kila siku? Ndugu walitutolea mapendekezo mazuri kuhusu yale ambayo tungefanya, naye Yehova akatulinda kwa mkono wake wenye nguvu. Hilo lilitufunza umuhimu wa kujifunza Biblia kwa bidii na kutafakari tunapokuwa huru na tunapokuwa na nafasi.

Wakati wa Maamuzi Muhimu

Kwa msaada wa Yehova, tulibaki imara. Tulishangaa sana wakati baadhi yetu tuliposamehewa mwishoni mwa mwaka wa 1956. Ni vigumu kueleza furaha tuliyohisi tulipoachiliwa! Wakati huo, mwanangu alikuwa na umri wa miaka sita, na ilikuwa shangwe kubwa kwangu kujiunga tena na mke wangu na kusaidiana naye kumlea mtoto wetu. Kwa muda fulani Johannes aliniona kama mgeni, lakini muda si muda tukawa na uhusiano mchangamfu.

Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani Mashariki walikabili wakati mgumu sana. Kuongezeka kwa upinzani kuelekea huduma yetu ya Kikristo na msimamo wetu wa kutokuwamo ni mambo yaliyomaanisha kwamba tulipaswa kuishi chini ya vitisho daima, yaani, maisha yenye hatari, hangaiko, na kukatisha tamaa. Hivyo, ilitubidi mimi na Erika tuchunguze hali yetu kwa makini na katika sala, na ili tusilemewe na hangaiko, tuliona tunahitaji kuhamia eneo lingine ambako tungeishi katika hali nzuri. Tulitaka kuwa huru ili kumtumikia Yehova na kufuatia miradi ya kiroho.

Mapema mwaka wa 1957, nafasi ilijitokeza kwetu kuhamia Stuttgart, Ujerumani Magharibi. Huko kazi ya kuhubiri haikuwa imepigwa marufuku, nasi tungeweza kushirikiana kwa uhuru na ndugu zetu. Upendo wao ulitutegemeza sana. Tulishirikiana kwa miaka saba na kutaniko la Hedelfingen. Wakati huo, mtoto wetu alianza shule na alifanya maendeleo katika ukweli. Mnamo Septemba 1962, nilipata nafasi ya pekee ya kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme huko Wiesbaden. Nikiwa huko nilitiwa moyo kuhama pamoja na familia yangu ili kutumikia katika eneo ambako walimu wa Biblia wanaozungumza Kijerumani walihitajiwa. Hilo lilitia ndani maeneo fulani ya Ujerumani na Uswisi.

Kwenye Milima ya Alps ya Uswisi

Hivyo, tulihamia Uswisi mwaka wa 1963. Tuliambiwa tutumikie pamoja na kutaniko dogo huko Brunnen, karibu na ziwa maridadi la Lucerne, katika sehemu ya kati ya milima ya Alps ya Uswisi. Eneo hilo lilikuwa kama paradiso kwetu. Ilitubidi tujizoeze Kijerumani kinachozungumzwa Uswisi, hali ya maisha, na mtazamo wa watu. Hata hivyo, tulifurahia kutumika na kuhubiri kati ya watu wenye amani na upendo. Tulikaa miaka 14 huko Brunnen, na mwana wetu alikulia huko.

Mnamo 1977, nilipokuwa na umri wa miaka 50 hivi, tulipokea mwaliko wa kutumika katika Betheli ya Uswisi huko Thun. Tuliliona kuwa pendeleo lisilotarajiwa, nasi tukalikubali kwa uthamini mkubwa. Mimi na mke wangu tulitumika Betheli kwa muda wa miaka tisa, ambao tunaukumbuka kama hatua muhimu na ya kipekee katika maisha yetu ya Kikristo na ukuzi wetu wa kiroho. Pia tulifurahi kuhubiri pamoja na wahubiri wenyeji huko Thun na katika maeneo ya karibu, tukifurahia sikuzote kuona “kazi za ajabu” za Yehova, yaani, milima maridadi ya Alps ya Bernese yenye vilele vilivyofunikwa na barafu.—Zaburi 9:1.

Twahama Tena

Tulihama tena mwanzoni mwa mwaka wa 1986. Tuliombwa kutumikia kama mapainia wa pekee katika eneo kubwa sana lililogawiwa Kutaniko la Buchs mashariki mwa Uswisi. Kwa mara nyingine, ilitubidi kuzoea maisha tofauti. Hata hivyo, kwa kuchochewa na tamaa yetu ya kumtumikia Yehova kokote ambako tungetumiwa vizuri zaidi, tulianza mgawo huo mpya, naye akatubariki. Mara kwa mara, nimesaidia waangalizi wasafirio kutembelea na kuimarisha makutaniko. Miaka kumi na minane imepita sasa, nasi tumejionea mambo mengi yenye kufurahisha tunapohubiri katika eneo hili. Kutaniko la Buchs limekua, nasi hufurahia kufanya mikutano katika Jumba la Ufalme maridadi, lililowekwa wakfu miaka mitano iliyopita.

Yehova ametujali sana. Tumetumia sehemu kubwa ya maisha yetu katika huduma ya wakati wote, lakini hatukuwahi kamwe kukosa chochote. Tuna shangwe na uradhi wa kuona mwana wetu, mke wake, watoto wao, na pia familia za wajukuu wetu, wakitembea kwa uaminifu katika njia ya Yehova.

Ninapokumbuka miaka ya nyuma, kwa kweli ninahisi kwamba tumemtumikia Yehova ‘katika majira yanayofaa, na katika majira yenye taabu.’ Kufuatia huduma ya Kikristo kumenitoa katika magereza yenye giza ya Kikomunisti hadi kwenye milima maridadi ya Alps ya Uswisi. Mimi na familia yangu hatujawahi kujuta.

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

“Waathiriwa Maradufu,” Wabaki Imara Chini ya Mateso

Katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani (GDR), ambayo pia iliitwa Ujerumani Mashariki, Mashahidi wa Yehova walikandamizwa kikatili. Ripoti zinaonyesha kwamba Mashahidi zaidi ya 5,000 walipelekwa kufanya kazi ngumu katika kambi mbalimbali na kwenye vituo vya wafungwa kwa sababu ya huduma yao ya Kikristo na msimamo wao wa kutokuwamo.—Isaya 2:4.

Baadhi ya Mashahidi hao wameitwa “waathiriwa maradufu.” Mashahidi 325 hivi kati yao walikuwa wamefungwa katika kambi za mateso za Nazi na katika magereza. Kisha, miaka ya 1950, walisakwa na kufungwa na Stasi, Shirika la Usalama la Kitaifa la GDR. Hata baadhi ya magereza yalitumiwa na maofisa wa Nazi, kisha yakatumiwa na maofisa wa Stasi.

Katika miaka kumi ya kwanza ya upinzani mkali, toka 1950 hadi 1961, jumla ya Mashahidi 60—wanaume kwa wanawake—walikufa gerezani kutokana na dhuluma, ukosefu wa chakula kinachofaa, magonjwa, na uzee. Mashahidi kumi na wawili walihukumiwa kifungo cha maisha ambacho baadaye kilipunguzwa kuwa miaka 15 gerezani.

Leo, katika makao makuu ya Stasi ya zamani huko Berlin, kuna uthibitisho wenye kudumu unaoonyesha jinsi Mashahidi wa Yehova walivyoteswa kwa miaka 40 kwa kibali cha serikali ya Ujerumani Mashariki. Picha na masimulizi ya watu binafsi yanayoonyeshwa huko, yanatoa ushuhuda wa kimya-kimya kuhusu uhodari na nguvu za kiroho za Mashahidi hao ambao walibaki waaminifu chini ya mateso.

[Ramani katika ukurasa wa 24, 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

UJERUMANI MASHARIKI

Rudolstadt

Belzig

Torgau

Chemnitz

Zwickau

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ngome ya Osterstein, huko Zwickau

[Hisani]

Fotosammlung des Stadtarchiv Zwickau, Deutschland

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa pamoja na mke wangu, Erika