Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Ngome na Nguvu Yangu

Yehova Ni Ngome na Nguvu Yangu

Simulizi la Maisha

Yehova Ni Ngome na Nguvu Yangu

KAMA LILIVYOSIMULIWA NA MARCEL FILTEAU

“Ukiolewa na yeye, hakika utafungwa gerezani.” Ndivyo watu walivyomwambia mwanamke niliyekuwa nikipanga kumwoa. Ebu niwaeleze sababu iliyofanya waseme hivyo.

NILIPOZALIWA mwaka wa 1927, Ukatoliki ulikuwa umekolea katika mkoa wa Quebec, Kanada. Miaka minne hivi baadaye, Cécile Dufour, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, akaanza kututembelea nyumbani katika jiji la Montreal. Mara nyingi alikuwa akitishwa na jirani zetu kwa kufanya hivyo. Hata alikamatwa na kutendwa vibaya mara nyingi kwa sababu ya kuhubiri ujumbe wa Biblia. Basi punde si punde tulipata kujua ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mtakuwa vitu vya kuchukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.”—Mathayo 24:9.

Wakati huo, wengi waliona kwamba haiwezekani kwa familia ya Wakanada wenye asili ya Kifaransa kuacha dini yao ya Katoliki. Ijapokuwa wazazi wangu hawakupata kuwa Mashahidi waliobatizwa, mara moja walikata kauli ya kwamba mafundisho ya Kanisa Katoliki hayapatani na Biblia. Basi wakawatia moyo watoto wao wanane wasome vichapo vilivyochapishwa na Mashahidi, na waliunga mkono baadhi yetu tuliochukua msimamo kwa ajili ya kweli ya Biblia.

Kuchukua Msimamo Katika Nyakati Ngumu

Mwaka wa 1942, nilipokuwa ningali shuleni, nilianza kupenda sana kusoma Biblia. Wakati huo utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa umepigwa marufuku nchini Kanada kwa sababu walifuata mfano wa Wakristo wa mapema na hawakujihusisha na vita vya mataifa. (Isaya 2:4; Mathayo 26:52) Ndugu yangu mkubwa zaidi, Roland, alifungwa katika kambi ya kazi ngumu kwa sababu alikataa kupigana wakati vita ya ulimwengu ilipokuwa imepamba moto wakati huo.

Karibu na wakati huo, Baba akanipa kitabu kimoja cha Kifaransa kinachozungumzia mateseko ya Mashahidi wa Ujerumani kwa kukataa kuunga mkono harakati za vita za Adolph Hitler. * Nilichochewa kujiunga na watu kama hawa wenye mifano mizuri ya moyo mkuu ya kushika uaminifu wa maadili, nikaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika nyumba fulani. Punde si punde nikaalikwa nishiriki katika kazi ya kuhubiri. Nikakubali mwaliko huo nikijua wazi kwamba ningekamatwa na kufungwa.

Baada ya kusali ili nipate nguvu, nikabisha mlango kwa mara ya kwanza. Bibi mmoja mwenye fadhili alitokea, na baada ya kujitambulisha, nikamsomea maneno ya 2 Timotheo 3:16: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa.”

“Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia?” nikauliza.

“Ndiyo,” akajibu.

Basi nikamwambia ningeleta rafiki mwingine anayefahamu Biblia vizuri kuliko mimi, nikafanya hivyo juma lililofuata. Baada ya tukio hilo la kwanza, nikawa mwenye hakika zaidi, nikajifunza kwamba hatutekelezi kazi hii ya huduma kwa nguvu zetu. Kama mtume Paulo alivyosema, twafanya hivyo kwa msaada wa Yehova. Kwa kweli, ni muhimu tutambue kwamba “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida [ni] ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.”—2 Wakorintho 4:7.

Baadaye, kazi ya kuhubiri ikawa kawaida ya maisha yangu na ndivyo na kukamatwa-kamatwa na kufungwa. Si ajabu kwamba yule niliyetazamia kumwoa aliambiwa, “Ukiolewa na yeye, hakika utafungwa gerezani”! Lakini, mambo kama hayo hayakuwa magumu sana. Baada ya kukaa jela siku moja, mara nyingi Shahidi mwingine alitutoa kwa dhamana.

Maamuzi Muhimu

Mnamo Aprili 1943, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa ubatizo wa maji. Kisha, mnamo Agosti 1944, nikahudhuria mkusanyiko mkubwa kwa mara ya kwanza kule Buffalo, New York, Marekani, karibu na mpaka wa Kanada. Watu 25,000 walihudhuria, na programu hiyo ikachochea tamaa yangu ya kuwa painia, kama wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Marufuku juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kanada iliondolewa Mei 1945, nikaanza kufanya upainia mwezi uliofuata.

Hata hivyo, kadiri nilivyozidi kushiriki katika huduma ndivyo nilivyozidi kutiwa korokoroni. Pindi moja niliwekwa kwenye seli moja na Mike Miller, mtumishi mwaminifu wa Yehova aliyekuwa ametumikia kwa muda mrefu. Tuliketi kwenye sakafu ya sementi na kuzungumza. Mazungumzo yetu yenye kujenga kiroho yaliniimarisha sana. Lakini, baadaye nikawaza, ‘Ingalikuwaje kama hatukuwa tukisikilizana na kuzungumziana?’ Wakati niliotumia pamoja na ndugu huyo mpendwa korokoroni ulinifundisha mojawapo ya masomo mazuri zaidi maishani—twahitaji ndugu zetu na basi twapaswa kuwa wenye kusameheana na wenye fadhili mtu na mwenzake. La sivyo, kama mtume Paulo alivyoandika: “Ikiwa mnafuliza kuumana na kunyafuana, jihadharini kwamba msipate kuangamizana mtu na mwenzake.”—Wagalatia 5:15.

Mnamo Septemba 1945, nilialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society, Toronto, Kanada, ambayo tunaiita Betheli. Kwa kweli ratiba ya kiroho huko ilikuwa yenye kujenga na yenye kuimarisha imani. Mwaka uliofuata, nilipewa mgawo wa kufanya kazi katika shamba la Betheli, kilometa zipatazo 40 kaskazini mwa ofisi ya tawi. Nilipokuwa nikichuma zabibubua na msichana aitwaye Anne Wolynec, niliona urembo wake na kuona pia upendo wake na bidii yake kwa Yehova. Basi uhusiano ukaanza, tukafunga ndoa Januari 1947.

Kwa miaka miwili na nusu iliyofuata, tulifanya upainia London, Ontario, na baada ya hapo katika Cape Breton Island, ambako tulisaidia kuanzisha kutaniko. Kisha, mwaka wa 1949, tukaalikwa kuhudhuria darasa la 14 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, ambako tulizoezwa kuwa mishonari.

Kazi ya Mishonari Katika Mkoa wa Quebec

Wahitimu kutoka Kanada wa madarasa yaliyotangulia ya Gileadi walipewa mgawo wa kuanzisha kazi ya kuhubiri katika mkoa wa Quebec. Mwaka wa 1950, sisi pamoja na wengine 25 katika darasa letu la 14 tulijiunga nao. Utendaji zaidi wa mishonari ulileta mnyanyaso mkali na ghasia za umati zilizochochewa na viongozi wa Kanisa Katoliki.

Siku mbili baada ya kufika katika mgawo wetu wa kwanza wa mishonari katika jiji la Rouyn, Anne alikamatwa na kuwekwa nyuma ya gari la polisi. Hakuwa amewahi kukamatwa, kwa kuwa alilelewa katika kijiji kidogo katika mkoa wa Manitoba, Kanada, ambako ilikuwa nadra kumwona polisi. Kama kawaida aliogopa sana akakumbuka maneno aliyoambiwa, “Ukiolewa na yeye, hakika utafungwa gerezani.” Hata hivyo, kabla ya kuondoka, polisi walinipata pia na kuniweka pamoja na Anne. “Nimefurahi kukuona!” akasema. Lakini, ajabu ni kwamba alikuwa mtulivu, akisema, “Mambo haya yaliwapata mitume kwa sababu ya kuhubiri kuhusu Yesu.” (Matendo 4:1-3; 5:17, 18) Baadaye siku hiyo takaachiliwa kwa dhamana.

Mwaka mmoja hivi baada ya kisa hicho, tulipokuwa tukifanya huduma ya nyumba hadi nyumba katika mgawo wetu mpya jijini Montreal, nilisikia msukosuko barabarani nikaona umati wenye ghasia ukitupa mawe. Nilipoenda kumsaidia Anne na mwenzake, polisi wakafika. Badala ya kuwakamata watu wenye kufanya ghasia, polisi walimkamata Anne na mwenzake! Walipokuwa korokoroni, Anne alimkumbusha Shahidi huyo mpya kwamba walikuwa wakiona ukweli wa maneno ya Yesu: “Mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.”—Mathayo 10:22.

Pindi moja, kesi zipatazo 1,700 dhidi ya Mashahidi wa Yehova zilikuwa zikingojea kusikilizwa katika mkoa wa Quebec. Kwa ujumla, tulishtakiwa kwa kuwapa watu fasihi yenye uchochezi au kwa kuwapa fasihi bila leseni. Basi, Idara ya Sheria ya Watch Tower Society ikachukua hatua dhidi ya serikali ya Quebec. Baada ya miaka mingi ya mapambano ya kisheria, Yehova alitupa ushindi mkubwa mara mbili katika Mahakama Kuu Zaidi ya Kanada. Mnamo Desemba 1950, tuliondolewa shtaka la kwamba fasihi yetu ni yenye uchochezi, na Oktoba 1953, haki yetu ya kutoa fasihi ya Biblia bila leseni ikatetewa. Basi tukajionea dhahiri shahiri jinsi Yehova alivyo kwa kweli mahali pa ‘kimbilio na nguvu, msaada unaoonekana tele wakati wa mateso.’—Zaburi 46:1.

Ni jambo la kutokeza kwamba idadi ya Mashahidi katika mkoa wa Quebec imeongezeka kutoka 356 mwaka wa 1945 nilipoanza kufanya upainia hadi zaidi ya 24,000 leo! Kwa kweli, imekuwa tu kama unabii wa Biblia ulivyotabiri: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa.”—Isaya 54:17.

Kazi Yetu Nchini Ufaransa

Mnamo Septemba 1959, tulialikwa pamoja na Anne kutumikia katika Betheli ya Paris, Ufaransa, ambako nilipewa mgawo wa kusimamia kazi ya uchapaji. Kabla hatujawasili Januari 1960, uchapaji ulikuwa ukifanywa na kampuni moja ya kibiashara. Kwa kuwa Mnara wa Mlinzi lilikuwa limepigwa marufuku Ufaransa, tulichapa gazeti hilo kila mwezi likifanana na kijitabu chenye kurasa 64. Kijitabu hicho kiliitwa The Interior Bulletin of Jehovah’s Witnesses, na kilikuwa na makala za kusoma katika makutaniko kwa mwezi mzima. Tokea 1960 hadi 1967, idadi ya wale walioshiriki katika kazi ya kuhubiri nchini Ufaransa iliongezeka kutoka 15,439 hadi 26,250.

Hatimaye, mishonari wengi walipewa tena mgawo wa kwenda kwingineko, wengine wakaenda kwenye nchi za Afrika zinazozungumza Kifaransa na wengine wakarudi Quebec. Kwa kuwa Anne alikuwa mgonjwa na alihitaji kufanyiwa upasuaji, tulirudi Quebec. Baada ya kutibiwa kwa miaka mitatu, Anne alipona. Kisha nikapewa mgawo wa kazi ya mzunguko, nikizuru kutaniko tofauti kila juma ili kutia wengine moyo kiroho.

Kazi ya Mishonari Katika Afrika

Miaka michache baadaye, mwaka wa 1981, tulifurahi kupokea mgawo mpya wa kutumikia tukiwa mishonari nchini Zaire, ambayo sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Watu walikuwa maskini na walikuwa na magumu mengi. Tulipofika, kulikuwa na Mashahidi 25,753, lakini leo wameongezeka kupita 113,000, na 446,362 walihudhuria Ukumbusho wa Kifo cha Kristo mwaka wa 1999!

Mwaka wa 1984 tulipokea kutoka kwa serikali ekari 500 za ardhi za kujengea ofisi mpya ya tawi. Kisha, Desemba 1985, mkusanyiko wa kimataifa ukafanywa katika jiji kuu, Kinshasa, kukiwa na wahudhuriaji 32,000 waliotoka sehemu nyingi za ulimwengu. Baadaye, upinzani uliochochewa na makasisi ukavuruga kazi yetu nchini Zaire. Mnamo Machi 12, 1986, ndugu wenye madaraka walipewa barua iliyotangaza kwamba shirika la Mashahidi wa Yehova la Zaire si halali. Marufuku juu ya utendaji wetu wote ilitiwa sahihi na aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Mobutu Sese Seko.

Kwa sababu ya matukio hayo ya ghafula, ilitubidi tutumie shauri la Biblia: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha.” (Mithali 22:3) Hivyo, tukatafuta njia ya kupata karatasi, wino, film, mabamba ya kuchapia, na kemikali kutoka nje ya nchi ili kuchapisha vichapo vyetu Kinshasa. Pia tulianzisha njia yetu wenyewe ya kusafirisha vitu. Mara tu ilipopangwa vizuri, njia yetu ya kusafirisha vitu ilikuwa bora kuliko huduma za posta ya serikali!

Maelfu ya Mashahidi walikamatwa, na wengi wakateswa kikatili. Lakini, isipokuwa wachache tu, wao walistahimili kutendwa vibaya na kudumisha uaminifu wao. Hata mimi nilikamatwa, nikaona hali mbaya sana ambazo ndugu walizikabili gerezani. Mara nyingi tulisongwa sana na polisi wa siri na wenye mamlaka, lakini sikuzote Yehova alitutokezea njia.—2 Wakorintho 4:8.

Tulificha katoni 3,000 hivi za fasihi katika bohari ya mfanya-biashara mmoja. Hata hivyo, hatimaye mmojawapo wa wafanyakazi wake aliwajulisha polisi wa siri, wakamkamata mfanya-biashara huyo. Wakiwa njiani kwenda korokoroni, kwa ghafula tukakutana nao nikiwa katika gari langu. Huyo mfanya-biashara akawaambia kwamba ni mimi niliyefanya mipango pamoja naye ya kuweka fasihi hapo. Polisi wakasimama na kunihoji kuhusu jambo hilo, wakinishtaki kwamba niliweka fasihi haramu katika bohari ya mtu huyo.

“Mna kimojawapo cha vitabu hivyo?” nikauliza.

“Ndiyo, tunacho,” wakajibu.

“Naweza kukiona?” nikauliza.

Wakaniletea kitabu kimoja, nikawaonyesha ukurasa wa ndani, usemao hivi: “Kimechapwa Marekani na Watch Tower Bible & Tract Society.”

“Hiki kitabu ni mali ya Marekani wala si mali ya Zaire,” nikawakumbusha. “Serikali yenu imepiga marufuku shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova la Zaire wala si Watch Tower Bible & Tract Society la Marekani. Mwe waangalifu sana na kile mnachofanya na vichapo hivi.”

Niliachiliwa niende nyumbani kwa sababu hawakuwa na amri ya mahakama ya kunikamata. Usiku huo tulipeleka lori mbili kwenye bohari hiyo na kuchukua fasihi yote. Wenye mamlaka walipokuja siku iliyofuata, walikasirika sana kupata mahali hapo pakiwa patupu. Kufikia wakati huo walikuwa wakinitafuta, kwa kuwa sasa walikuwa na amri ya mahakama ya kunikamata. Wakanipata, lakini kwa sababu hawakuwa na gari, nikajipeleka korokoroni kwa gari langu! Shahidi mwingine aliandamana nami ili aweze kuchukua gari langu kabla ya hao kulinyakua.

Baada ya kunihoji kwa muda wa saa nane, waliamua kunihamisha. Lakini nikawaonyesha nakala ya barua ya serikali iliyothibitisha kwamba nimechaguliwa kufunga hesabu ya mali za shirika la Mashahidi wa Yehova la Zaire ambalo sasa lilikuwa limepigwa marufuku. Basi nikaruhusiwa kuendelea na utendaji wangu Betheli.

Baada ya miaka minne ya kufanya kazi chini ya mkazo tukiwa tumepigwa marufuku nchini Zaire, nilipata kidonda cha tumbo chenye kutoa damu ambacho kingeweza kusababisha kifo. Ikaamuliwa kwamba niondoke nipate tiba nchini Afrika Kusini, ambako ofisi ya tawi ilinitunza vizuri, nikapona. Baada ya kutumikia kwa miaka minane nchini Zaire, iliyokuwa yenye kufurahisha sana na nisiyoweza kusahau, tulihamia ofisi ya tawi ya Afrika Kusini mwaka wa 1989. Mwaka wa 1998 tulirudi kwetu na tangu wakati huo tumekuwa tukitumikia tena katika Betheli ya Kanada.

Nashukuru Kutumikia

Ninapotazama miaka 54 ya utumishi wa wakati wote, ninashukuru sana kwamba nilitumia nguvu zangu za ujana katika utumishi wenye thamani wa Yehova. Japo Anne amelazimika kuvumilia hali nyingi ngumu, hajalalamika bali ameniunga mkono katika utendaji wetu wote. Tukiwa pamoja tumepata pendeleo la kuwasaidia wengi wapate kumjua Yehova, na kadhaa kati yao sasa ni wahudumu wa wakati wote. Ni shangwe sana kuona kwamba baadhi ya watoto wao na hata wajukuu wao wanamtumikia Mungu wetu mkuu, Yehova!

Nasadiki kabisa kwamba hakuna kitu ambacho ulimwengu huu unaweza kutupa kinachoweza kulinganishwa na mapendeleo na baraka ambazo Yehova ametupa. Ni kweli kwamba tumevumilia majaribu mengi, lakini hayo yote yameimarisha imani yetu na uhakika wetu katika Yehova. Kwa kweli amekuwa nguzo, na mahali pa usalama, na msaada ambao hupatikana kwa urahisi wakati wa mikazo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kitabu hicho kilichapishwa kwanza katika Kijerumani kikiitwa Kreuzzug gegen das Christentum (Krusedi Dhidi ya Ukristo). Kilitafsiriwa katika Kifaransa na Kipoland lakini hakikutafsiriwa katika Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tukifanya upainia pamoja mwaka wa 1947; na tukiwa na Anne leo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Watu tuliowapata Zaire walipenda kweli ya Biblia