Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wenye Shangwe Katika Mungu wa Wokovu Wetu

Wenye Shangwe Katika Mungu wa Wokovu Wetu

Wenye Shangwe Katika Mungu wa Wokovu Wetu

‘Nitamfurahia BWANA, nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.’—HABAKUKI 3:18.

1. Danieli aliona ono kuhusu nini kabla ya Babiloni kuanguka mwaka wa 539 K.W.K.?

MUDA unaozidi mwongo mmoja kabla ya Babiloni kuanguka mwaka wa 539 K.W.K., nabii Danieli aliyekuwa amezeeka aliona ono lenye kusisimua. Lilitabiri matukio ya ulimwengu yaliyoendelea hadi kwenye vita ya kukata maneno kati ya adui za Yehova na Mfalme wake aliyewekwa rasmi, Yesu Kristo. Danieli aliitikiaje? Alisema hivi: “Nikazimia . . . naliyastajabia yale maono.”—Danieli 8:27.

2. Danieli aliona pambano gani katika ono, na unahisije kuhusu ukaribu wake?

2 Na sisi je? Twaishi muda mrefu sana baadaye! Sisi hutendaje tutambuapo kwamba pambano ambalo Danieli aliona katika ono—vita ya Mungu ya Har–Magedoni—lakaribia sana? Sisi hutendaje tunapotambua kwamba uovu uliofichuliwa katika unabii wa Habakuki umeenea sana hivi kwamba kuharibiwa kwa adui za Mungu hakuepukiki? Yamkini, hisia zetu zafanana na zile za Habakuki mwenyewe, kama zifafanuliwavyo katika sura ya tatu ya kitabu chake cha kiunabii.

Habakuki Asali kwa Ajili ya Rehema ya Mungu

3. Habakuki alisali kwa niaba ya nani, na maneno yake yanaweza kutuathirije leo?

3 Habakuki sura ya 3 ni sala. Kulingana na mstari wa 1, sala hiyo inaonyeshwa kwa wimbo wa huzuni au maombolezo. Nabii huyo atoa sala hiyo kana kwamba ilikuwa yake mwenyewe. Lakini kwa kweli, Habakuki anasema kwa niaba ya taifa teule la Mungu. Leo, sala yake ina maana kubwa sana kwa watu wa Mungu, ambao wanajishughulisha na kazi ya kuhubiri Ufalme. Tusomapo Habakuki sura ya 3 tukiwa na maoni hayo, maneno yake hutuhuzunisha lakini pia hutufanya tuwe wenye shangwe. Sala ya Habakuki, au maombolezo, hutupatia sababu yenye nguvu ya kuwa na shangwe katika Yehova, Mungu wa wokovu wetu.

4. Kwa nini Habakuki aliogopa, na tunaweza kuwa na hakika juu ya matendo gani yenye nguvu ya Mungu?

4 Kama ambavyo tumeona katika makala mbili zilizotangulia, hali zilikuwa mbaya sana katika Yuda wakati wa Habakuki. Lakini Mungu hangeruhusu hali hiyo iendelee. Yehova angechukua hatua, kama alivyokuwa amefanya wakati uliopita. Si ajabu nabii huyo alilia hivi: “Ee BWANA, nimesikia habari zako, nami naogopa; Ee BWANA”! Alimaanisha nini? ‘Habari za Yehova’ zilikuwa historia iliyorekodiwa ya matendo yenye nguvu ya Mungu, kama vile kwenye Bahari Nyekundu, nyikani, na huko Yeriko. Habakuki aliyajua vema matendo hayo, nayo yalimwogofya kwa sababu alijua kwamba Yehova angetumia tena nguvu zake nyingi dhidi ya adui zake. Tuonapo uovu wa wanadamu leo, sisi pia twajua kwamba Yehova atatenda kama alivyofanya nyakati za kale. Je, hilo latufanya tuogope? Bila shaka! Hata hivyo, twasali kama Habakuki alivyosali: “Fufua kazi yako katikati ya miaka; katikati ya miaka tangaza habari yake; katika ghadhabu kumbuka rehema.” (Habakuki 3:2) Wakati barabara wa Mungu, “katikati ya miaka,” na atumie nguvu zake za kimuujiza. Wakati huo, na akumbuke kuwarehemu wampendao!

Yehova Yu Mwendoni!

5. ‘Mungu alikujaje kutoka Temani,’ na jambo hilo laonyesha nini kuhusu Har–Magedoni?

5 Ni nini kitakachotukia Yehova asikiapo sala yetu ya rehema? Twapata jibu kwenye Habakuki 3:3, 4. Kwanza, nabii huyo asema hivi: “Mungu alikuja kutoka Temani, Yeye aliye mtakatifu kutoka mlima Parani.” Wakati wa nabii Musa, Waisraeli walipitia Temani na Parani walipokuwa nyikani wakielekea Kanaani. Taifa hilo kubwa la Israeli lilipokuwa likisafiri, ilionekana kwamba Yehova mwenyewe alikuwa mwendoni na kwamba hakuna kitu chochote kingeweza kumzuia. Punde kabla ya Musa kufa, alisema hivi: “Mwenyezi-Mungu alikuja kutoka mlima Sinai; alitutokea kutoka mlima Seiri; aliiangaza kutoka mlima Parani. Alitokea kati ya maelfu ya malaika.” (Kumbukumbu la Torati 33:2, BHN) Yehova achukuapo hatua dhidi ya adui zake kwenye Har–Magedoni, kutakuwepo wonyesho kama huo wa uweza usioweza kupingwa.

6. Zaidi ya utukufu wa Mungu, Wakristo wenye utambuzi huona nini?

6 Habakuki asema hivi pia: “Utukufu [wa Yehova] ukazifunika mbingu, nayo dunia ikajaa sifa yake. Mwangaza wake ulikuwa kama nuru.” Ni tamasha tukufu kama nini! Ni kweli kwamba wanadamu hawawezi kumtazama Yehova Mungu wakaishi. (Kutoka 33:20) Hata hivyo, kwa habari ya watumishi waaminifu wa Mungu, macho ya mioyo yao hustaajabu wanapotafakari fahari yake. (Waefeso 1:18) Nao Wakristo wenye utambuzi waona kitu kingine zaidi ya utukufu wa Yehova. Habakuki 3:4 lamalizia hivi: “Alikuwa na mishale ya nuru ubavuni pake; ndipo ulipofichwa uweza wake.” Naam, twaona kwamba Yehova yu tayari kutenda, akiutumia mkono wake wa kuume wenye nguvu na uweza.

7. Mwendo wa Mungu wa shangwe ya ushindi wamaanisha nini kwa wale wanaomwasi?

7 Mwendo wa Mungu wa shangwe ya ushindi humaanisha kuharibiwa kwa wale wanaomwasi. Habakuki 3:5 husema hivi: “Mbele zake ilikwenda tauni, na makaa ya moto yakatoka miguuni pake.” Mwaka wa 1473 K.W.K., Waisraeli walipokuwa karibu na mipaka ya Bara Lililoahidiwa, wengi wao waliasi, wakifanya matendo ya ukosefu wa adili na kuabudu sanamu. Kwa hiyo, zaidi ya watu 20,000 wakafa kutokana na ugonjwa wa kuambukiza uliotoka kwa Mungu. (Hesabu 25:1-9) Hivi karibuni, Yehova apigapo mwendo kuelekea “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” wanaomwasi watakufa vivyo hivyo kutokana na dhambi zao. Huenda hata wengine wakafa kutokana na ugonjwa halisi wenye kuambukiza.—Ufunuo 16:14, 16.

8. Kulingana na Habakuki 3:6, ni nini kitakachowapata adui za Mungu?

8 Sasa sikieni nabii huyo akimfafanua kinaganaga Yehova wa majeshi akitenda. Kwenye Habakuki 3:6, twasoma: “[Yehova Mungu] akasimama, akaitetemesha dunia; akatazama, akawasitusha mataifa; na milima ya zamani ikatawanyika; vilima vya kale vikainama; miendo yake ilikuwa kama siku za kale.” Kwanza, Yehova ‘asimama,’ kama jenerali anayeukagua uwanja wa vita. Adui zake watetemeka kwa woga. Wanaona mpinzani wao ni nani na kushtuka, wakiruka kwa kufadhaika. Yesu alitabiri wakati ambapo “makabila yote ya dunia yatakapojipiga yenyewe kwa maombolezo.” (Mathayo 24:30) Watakuwa wamechelewa mno kutambua kwamba hakuna mtu awaye yote awezaye kusimama dhidi ya Yehova. Mashirika ya kibinadamu—hata yale yaonekanayo kuwa ya kudumu kama “milima ya zamani” na “vilima vya kale”—yataporomoka. Kisha itakuwa kama ‘miendo ya Mungu ya siku za kale,’ kama alivyotenda nyakati za kale.

9, 10. Andiko la Habakuki 3:7-11 latukumbusha nini?

9 ‘Hasira ya Yehova imekuwa juu’ dhidi ya adui zake. Lakini atatumia silaha gani katika vita yake kuu? Sikiliza nabii huyo azifafanuapo, akisema: “Uta wako ukafanywa wazi kabisa; viapo walivyopewa kabila vilikuwa neno thabiti; ukaipasua nchi kwa mito. Milima ilikuona, ikaogopa; gharika ya maji ikapita; vilindi vikatoa sauti yake, vikainua juu mikono yake. Jua na mwezi vikasimama makaoni mwao; mbele ya nuru ya mishale yako ilipotapakaa, mbele ya mwangaza wa mkuki wako umeremetao.”—Habakuki 3:7-11.

10 Siku za Yoshua, Yehova alifanya jua na mwezi visimame tuli akionyesha nguvu zenye kutokeza. (Yoshua 10:12-14) Maneno ya Habakuki yatukumbusha kwamba Yehova atatumia nguvu hizohizo kwenye Har–Magedoni. Mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alionyesha ukuu wake juu ya vilindi vya maji vya dunia alipoitumia Bahari Nyekundu ili kuyaharibu majeshi ya Farao. Miaka 40 baadaye, mto Yordani uliokuwa umefurika kabisa haukuwazuia kwa njia yoyote ile Waisraeli waliokuwa wakipiga mwendo wa ushindi kuingia Bara Lililoahidiwa. (Yoshua 3:15-17) Siku za nabii wa kike Debora, mvua nyingi sana ilifagilia mbali magari ya vita ya adui wa Israeli, Sisera. (Waamuzi 5:21) Yehova aweza kutumia nguvu hizohizo za mafuriko, mvua nyingi sana, na vilindi vya maji kwenye Har–Magedoni. Angeweza pia kutumia ngurumo na umeme, kama vile mkuki au podo lililojaa mishale.

11. Ni nini kitakachotokea Yehova aachiliapo nguvu zake kuu?

11 Kwa kweli, litakuwa jambo lenye kutia kicho Yehova atakapoachilia nguvu zake kuu. Maneno ya Habakuki yadokeza kwamba usiku utakuwa mchana na mchana utakuwa mwangavu kuliko vile jua liwezavyo kuufanya uwe. Iwe ufafanuzi huo wa kiunabii wa Har–Magedoni ni halisi au ni wa kitamathali, jambo moja ni hakika—Yehova atashinda, wala hataruhusu adui yeyote aponyoke.

Wokovu Ni Hakika kwa Watu wa Mungu!

12. Mungu atawafanya nini adui zake, lakini ni nani atakayeokolewa?

12 Nabii huyo aendelea kufafanua matendo ya Yehova anapowaharibu adui Zake. Kwenye Habakuki 3:12, twasoma: “Ulikwenda katikati ya nchi kwa ghadhabu; ukawapura mataifa kwa hasira.” Hata hivyo, Yehova hataharibu ovyoovyo. Wanadamu fulani wataokolewa. “Ukatokea kwa ajili ya wokovu wa watu wako, kwa ajili ya wokovu wa masihi wako,” lasema andiko la Habakuki 3:13. Naam, Yehova atawaokoa watumishi wake watiwa-mafuta waaminifu. Kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, kutakuwa kumemalizika. Hata hivyo, leo mataifa yanajaribu kufutilia mbali ibada safi. Karibuni, watumishi wa Yehova watashambuliwa na majeshi ya Gogu wa Magogu. (Ezekieli 38:1–39:13; Ufunuo 17:1-5, 16-18) Je, mashambulizi hayo ya kishetani yatafaulu? La! Wakati huo Yehova atawaponda adui zake kwa hasira, akiwakanyaga kama nafaka kwenye sakafu ya kupuria. Lakini atawaokoa wale wamwabuduo kwa roho na kweli.—Yohana 4:24.

13. Andiko la Habakuki 3:13 litatimizwaje?

13 Kuangamizwa kabisa kwa waovu kulitabiriwa kwa maneno haya: “[Wewe Yehova] ukakiponda kichwa cha nyumba ya waovu, ukiuweka wazi msingi hata mwambani.” (Habakuki 3:13) “Nyumba” hiyo ni mfumo mwovu uliotokezwa na uvutano wa Shetani Ibilisi. Itavunjwavunjwa. “Kichwa,” au viongozi wampingao Mungu, kitapondwa. Jengo lote litabomolewa, hadi kwenye msingi wake. Halitakuwepo tena kamwe. Hicho kitakuwa kitulizo kilichoje!

14-16. Kulingana na Habakuki 3:14, 15, ni nini kitakachowapata watu wa Yehova na vilevile adui zao?

14 Kwenye Har–Magedoni, wale wanaojaribu kumwangamiza “masihi” wa Yehova watavurugwa. Kulingana na Habakuki 3:14, 15, nabii huyo asema na Mungu, akimwambia: “Ukakichoma kichwa cha mashujaa wake kwa fimbo zao wenyewe; wakaja kama kisulisuli ili kunitawanya; kama wakifurahi kuwameza maskini kwa siri. Ukaikanyaga bahari kwa farasi zako, chungu ya maji yenye nguvu.”

15 Habakuki asemapo “mashujaa . . . wakaja kama kisulisuli ili kunitawanya,” nabii huyo asema kwa niaba ya watumishi watiwa-mafuta wa Yehova. Kama maharamia wanaootea, mataifa yatawarukia waabudu wa Yehova ili kuwaangamiza. Adui hao wa Mungu na wa watu wake watakuwa “wakifurahi,” wakiwa na uhakika wa kufanikiwa. Wakristo waaminifu wataonekana kuwa dhaifu, kama “maskini.” Lakini majeshi yampingayo Mungu yashambuliapo, Yehova atayafanya yatumie silaha zao kuangamizana. Watatumia mikono, au “fimbo” zao, dhidi ya mashujaa wao wenyewe.

16 Na kuna mengi zaidi yatakayotokea. Yehova atatumia majeshi ya roho yenye nguvu zinazozidi zile za kibinadamu ili kukamilisha uharibifu huo. Akitumia “farasi” za majeshi yake ya kimbingu wakiwa chini ya Yesu Kristo, atasonga mbele akishinda kupitia “bahari” na “chungu ya maji yenye nguvu,” yaani, tungamo lenye kusukasuka la wanadamu adui. (Ufunuo 19:11-21) Kisha waovu wataondolewa duniani. Ni wonyesho wenye nguvu kama nini wa uweza na haki ya kimungu!

Siku ya Yehova Inakuja!

17. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika katika utimizo wa maneno ya Habakuki? (b) Tunawezaje kuwa kama Habakuki tungojeapo siku kuu ya Yehova?

17 Twaweza kuwa na uhakika kwamba maneno ya Habakuki yatatimizwa hivi karibuni. Hayatakawia. Kujua hivyo kimbele kwakuathirije wewe? Kumbuka kwamba Habakuki alikuwa akiandika mambo yaliyopuliziwa na Mungu. Yehova atatenda, na kutakuwa na uharibifu mkubwa duniani hilo litukiapo. Si ajabu kwamba nabii huyo aliandika hivi: “Nikasikia, na tumbo langu likatetemeka, midomo yangu ikatikisika kwa sauti ile; ubovu ukaingia mifupani mwangu, nikatetemeka katika mahali pangu; ili nipate kuingoja ile siku ya dhiki, kundi lao washambuliao wakweapo juu ya watu.” (Habakuki 3:16) Habakuki alifadhaika sana—na yaeleweka ni kwa nini. Lakini je, imani yake ilitikiswa? La hasha! Alikuwa tayari kungojea siku kuu ya Yehova kwa utulivu. (2 Petro 3:11, 12) Sisi pia tuna mtazamo huohuo, sivyo? Bila shaka ndivyo! Tuna imani kamili kwamba unabii wa Habakuki utatimizwa. Lakini tutangoja kwa saburi hadi utakapotimizwa.

18. Ingawa Habakuki alitazamia magumu, alikuwa na mtazamo gani?

18 Nyakati zote vita hutokeza magumu, hata kwa wale wanaoibuka wakiwa washindi. Huenda chakula kikapungua. Huenda mali zikapotezwa. Huenda viwango vya maisha vikashuka. Iwapo hayo yatupata, tutatendaje? Habakuki alikuwa na mtazamo unaofaa kuigwa, kwani alisema hivi: “Maana mtini hautachanua maua, wala mizabibuni hamtakuwa na matunda; taabu ya mzeituni itakuwa bure, na mashamba hayatatoa chakula; zizini hamtakuwa na kundi, wala vibandani hamtakuwa na kundi la ng’ombe; walakini nitamfurahia BWANA nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.” (Habakuki 3:17, 18) Habakuki alitarajia magumu, huenda alitarajia njaa kuu. Hata hivyo, hakupoteza kamwe shangwe yake katika Yehova, aliye chanzo cha wokovu wake.

19. Wakristo wengi hupatwa na magumu gani, lakini twaweza kuwa na hakika gani tukimtanguliza Yehova katika maisha zetu?

19 Leo, hata kabla ya vita ya Yehova dhidi ya waovu, watu wengi hutaabika sana. Yesu alitabiri kwamba vita, njaa kuu, matetemeko ya dunia, na magonjwa yangekuwa sehemu ya ‘ishara ya kuwapo kwake’ akiwa na nguvu za kifalme. (Mathayo 24:3-14; Luka 21:10, 11) Wengi wa waamini wenzetu huishi katika nchi ambazo zimekumbwa vibaya na utimizo wa maneno ya Yesu, nao wanapata magumu mengi kwa sababu ya utimizo huo. Huenda Wakristo wengine wakapatwa na mambo hayohayo siku za usoni. Kwa walio wengi kati yetu, yawezekana kabisa kwamba “mtini hautachanua maua” kabla ya mwisho kuja. Hata hivyo, twajua ni kwa nini mambo hayo yanatokea, na hilo hutupatia nguvu. Isitoshe, twategemezwa. Yesu aliahidi hivi: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu], na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Hilo halituhakikishii kupata maisha ya starehe, lakini latuhakikishia kwamba tukimtanguliza Yehova, atatulinda.—Zaburi 37:25.

20. Japo magumu ya muda, twapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Kwa hiyo, ijapokuwa magumu yoyote ya muda ambayo ni lazima tuyakabili, hatutapoteza imani katika nguvu ya kuokoa ya Yehova. Wengi wa ndugu na dada zetu katika Afrika, Ulaya Mashariki, na sehemu nyinginezo hulazimika kukabili magumu mazito, lakini wao hufuliza ‘kushangilia katika Yehova.’ Sisi nasi, kama wao, tusikome kamwe kufanya vivyo hivyo. Kumbuka Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ndiye Chanzo cha ‘nguvu zetu.’ (Habakuki 3:19) Hawezi kututamausha kamwe. Har–Magedoni itakuja hakika, na pasipo shaka ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu utafuata. (2 Petro 3:13) Kisha “dunia itajazwa maarifa ya utukufu wa BWANA, kama maji yaifunikavyo bahari.” (Habakuki 2:14) Hadi wakati huo mzuri ajabu, na tufuate kielelezo kizuri cha Habakuki. Na sikuzote ‘tumfurahie Yehova na kumshangilia Mungu wa wokovu wetu.’

Je, Wakumbuka?

• Sala ya Habakuki inaweza kutuathirije?

• Kwa nini Yehova yu mwendoni?

• Unabii wa Habakuki wasema nini kuhusu wokovu?

• Twapaswa kungoja siku kuu ya Yehova tukiwa na mtazamo gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, wajua Mungu atatumia majeshi gani dhidi ya waovu kwenye Har–Magedoni?