Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shauri la Mama Lenye Hekima

Shauri la Mama Lenye Hekima

Shauri la Mama Lenye Hekima

“Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” —Mithali 1:8.

WAZAZI wetu—baba na mama—wanaweza kuwa chanzo chenye thamani cha kitia-moyo, utegemezo, na shauri. Kitabu cha Biblia cha Mithali humtaja mfalme fulani kijana, Lemueli, ambaye alipokea “mausia aliyofundishwa” na mama yake. Maneno hayo yameandikwa katika Mithali sura ya 31, nasi pia twaweza kunufaika na shauri lenye hekima la mama huyo.—Mithali 31:1.

Shauri Lifaalo Mfalme

Mama ya Lemueli aanza kwa maswali ambayo yachochea upendezi wetu: “Ni nini, mwanangu? Tena ni nini, mwana wa tumbo langu? Tena, ni nini mwana wa nadhiri zangu?” Kwa kumsihi mara tatu, yeye aonyesha hangaiko lake la kutaka mwana wake ayazingatie maneno yake. (Mithali 31:2) Hangaiko lake kwa hali njema ya kiroho ya mtoto wake yawawekea kielelezo kizuri wazazi Wakristo leo.

Kuhusu hali njema ya mwana wake, ni nini ambacho kingemtia mama wasiwasi zaidi kuliko sherehe zenye kelele na ufasiki zinazohusisha mvinyo, wanawake, na nyimbo zinazotajwa sana? Mama ya Lemueli aeleza mambo waziwazi: “Usiwape wanawake nguvu zako.” Yeye aonyesha kwamba mwenendo wa kufanya ngono ovyo-ovyo ‘unawaharibu wafalme.’— Mithali 31:3.

Kunywa kupita kiasi hakupaswi kupuuzwa. “Kunywa mvinyo hakuwafai wafalme, hakuwafai wafalme,” yeye aonya. Mfalme atahukumuje ifaavyo na kwa utimamu wa akili bila ‘kuisahau sheria, na kuipotosha hukumu ya mtu aliye taabuni’ ikiwa yeye hulewa daima?—Mithali 31:4-7.

Lakini, akijiepusha na maovu hayo, mfalme ataweza ‘kuhukumu kwa haki; kuwapatia maskini na wahitaji haki yao.’—Mithali 31:8, 9.

Ingawa huenda vijana Wakristo wasiwe “wafalme” leo, shauri lenye hekima la mama ya Lemueli lafaa hata zaidi wakati huu. Matumizi mabaya ya kileo, kutumia tumbaku, na ukosefu wa adili katika ngono umeenea sana miongoni mwa vijana siku hizi, na ni muhimu kwa vijana Wakristo kuwasikiliza wazazi wao wanapowafundisha “mausia.”

Mke Mwema

Mama wengi huhangaikia kwa kufaa mataraja ya ndoa ya wana wao wanaokaribia utu uzima. Kisha mama ya Lemueli azungumzia sifa za mke mwema. Yaelekea, kijana mwanamume angenufaika sana kwa kufikiria maoni ya mwanamke juu ya jambo hilo muhimu.

Katika mstari wa 10, “mke mwema” anafananishwa na marijani haba yenye thamani, ambayo wakati wa Biblia ilipatikana tu kwa jitihada kubwa sana. Hali kadhalika, kumpata mke mwema kwahitaji jitihada. Badala ya kukimbilia ndoa haraka-haraka, ingekuwa vema kwa mwanamume kijana kufanya uchaguzi wake bila haraka. Ndipo, yaelekea atamthamini sana mke wake mwenye thamani.

Kuhusu mke mwema, Lemueli aambiwa: “Moyo wa mumewe humwamini.” (Mstari wa 11) Yaani, hapaswi kusisitiza kwamba mke wake amwombe kibali katika kila jambo. Bila shaka, mume na mke wanapaswa kushauriana kabla ya kufanya maamuzi makubwa, kama yale yanayohusisha kununua vitu vya bei kubwa au kulea watoto wao. Kuwasiliana katika mambo hayo hufanya mume na mke wawe na ukaribu zaidi.

Bila shaka, mke mwema ana mengi ya kufanya. Katika mstari wa 13 hadi 27 kuna mashauri na kanuni zilizoorodheshwa ambazo wake wa enzi yoyote ile wanaweza kutumia kwa manufaa ya familia zao. Kwa mfano, huku bei za mavazi na fanicha zikizidi kuongezeka, mke mwema hujifunza kujifanyia mambo na kutumia fedha kwa uangalifu ili familia yake iweze kuvalia ifaavyo na iwe yenye kupendeza. (Mstari wa 13, 19, 21, 22) Ili kupunguza fedha ambazo familia hutumia kununulia chakula, yeye hupanda anachoweza na kununua vitu kwa uangalifu.—Mstari wa 14, 16.

Ni wazi kwamba mwanamke huyu hali “chakula cha uvivu.” Yeye hufanya kazi kwa bidii na husimamia shughuli za nyumba yake ifaavyo. (Mstari wa 27) Yeye hujifunga “nguvu viunoni,” ikimaanisha kwamba yeye hujiandaa kufanya kazi ngumu. (Mstari wa 17) Yeye huamka kabla ya mapambazuko ili kuanza kazi, naye hufanya kazi kwa bidii hadi usiku. Ni kana kwamba taa ambayo huangaza anapofanya kazi haizimiki kamwe.—Mstari wa 15, 18.

Zaidi ya yote, mke mwema ni wa kiroho. Yeye humcha Mungu na kumwabudu kwa staha nyingi na hofu yenye kicho. (Mstari wa 30) Yeye pia humsaidia mume wake katika kuzoeza watoto wao wamche Mungu vilevile. Mstari wa 26 wasema: “Kwa hekima,” yeye huwafundisha watoto wake, na “sheria ya wema i katika ulimi wake.”

Mume Mwema

Ili kumvutia mke mwema, Lemueli angehitaji kutimiza wajibu mbalimbali wa mume mwema. Mama ya Lemueli amkumbusha mambo kadhaa kuhusiana na wajibu huo.

Mume mwema angesifiwa na “wazee wa nchi.” (Mithali 31:23) Hilo lamaanisha kwamba angekuwa mwanamume mwenye uwezo, mnyofu, mwenye kutumainika, na mcha-Mungu. (Kutoka 18:21; Kumbukumbu la Torati 16:18-20) Hivyo, yeye ‘angejulikana malangoni,’ ambapo watu mashuhuri hukusanyika kuendesha shughuli za jiji. Ili ‘ajulikane’ kuwa mcha-Mungu, ni lazima awe mwenye kusababu na kufanya kazi kwa kushirikiana na wazee wa “nchi,” labda ikimaanisha wilaya au eneo.

Yaelekea akizungumza kutokana na mambo aliyokuwa amejionea, mama ya Lemueli anamkumbusha mwana wake umuhimu wa kumthamini yule atakayekuwa mke wake. Angempenda mke wake zaidi ya mtu mwingine yeyote duniani. Hivyo, wazia jinsi anavyozungumza kwa hisia zenye nguvu anapokiri hadharani: “Binti za watu wengi wamefanya mema, lakini wewe umewapita wote.”— Mithali 31:29.

Yaonekana kwamba Lemueli alithamini shauri lenye hekima la mama yake. Kwa mfano, twaona kwamba katika mstari wa 1, yeye anarejezea maneno ya mama yake kana kwamba ni yake mwenyewe. Hivyo, alizingatia moyoni ‘fundisho’ la mama yake na kunufaika na shauri lake. Sisi pia na tunufaike na “mausia” hayo kwa kutumia kanuni zake maishani mwetu.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mke mwema hali “chakula cha uvivu”