Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | MASSIMO TISTARELLI

Mbuni wa Roboti Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Mbuni wa Roboti Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Profesa Massimo Tistarelli ni mwanasayansi katika Chuo Kikuu cha Sassari nchini Italia. Yeye ni mhariri-mshiriki wa magazeti matatu ya kimataifa kuhusu sayansi na ameandika tasnifu zaidi ya mia moja za kisayansi. Yeye huchunguza jinsi wanadamu wanavyoweza kutambua nyuso tofauti-tofauti na kufanya mambo madogo-madogo kama kudaka mpira. Kisha yeye hubuni mifumo ya kuona ya roboti—mifumo inayoiga uwezo wa kuona wa mwanadamu. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji kuhusu imani yake katika Mungu na kazi yake ya kisayansi.

Ulilelewa katika dini gani?

Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki lakini hawakuenda kanisani. Nilipokuwa kijana, sikuamini kwamba kuna Mungu. Nilifundishwa kwamba uhai ulitokana na mageuzi, na nikakubali jambo hilo kuwa ni kweli. Hata hivyo, ingawa sikuamini kwamba kuna Muumba, nilihisi kwamba lazima kuwe na mtu fulani aliye juu yetu. Ili nijichunguzie jambo hilo, nilijifunza mafundisho ya Wabudha, Wahindu, na Watao, lakini mafundisho hayo hayakuniridhisha.

Ni nini kilichochochea upendezi wako katika sayansi?

Tangu utotoni nilipendezwa sana na mashine. Hata nilikuwa nikifungua vifaa vyangu vya kuchezea vilivyoendeshwa kwa umeme na kuviunganisha tena. Na ningemuuliza baba yangu maswali mengi kuhusu vile redio na simu hufanya kazi, kwa kuwa yeye alikuwa injinia wa vyombo vya mawasiliano.

Umefanya kazi gani mbalimbali ukiwa mwanasayansi?

Nilijifunza mambo ya kielektroniki katika Chuo Kikuu cha Genoa, kisha nikafanya utafiti na kuandika tasnifu kuhusu ubuni wa roboti. Nilishughulikia hasa kujifunza kuhusu uwezo wa kuona wa mwanadamu na kubuni njia za kuiga mfumo huo katika roboti.

Kwa nini ulipendezwa na uwezo wetu wa kuona?

Kwa kweli uwezo wetu wa kuona ni mfumo tata sana, na unahusisha mengi zaidi ya macho yetu tu—unatia ndani uwezo  wa kuchanganua yale tunayoona. Kwa mfano, fikiria kinachotendeka unapodaka mpira. Unapokimbia ili kuudaka, lenzi ya jicho lako huelekeza picha ya mpira huo kwenye retina. Picha hiyo itasonga kwenye retina yako kwa kutegemea jinsi mpira na macho yako yanavyosonga. Bila shaka, utakazia macho yako kwenye mpira. Basi picha ya mpira husimama tuli kwenye retina yako lakini mazingira ndiyo huonekana kana kwamba yanasonga.

Wakati huohuo, mfumo wako wa kuona hupima mwendo wa mpira na upande unaoelekea. Kwa kustaajabisha, hesabu hizo huanza hapohapo ndani ya retina kwani jicho lako hukadiria mwendo wa mpira kwa kutegemea mazingira yake. Neva kuu ya jicho hupitisha ishara zilizotolewa na retina hadi kwenye ubongo, ambao huchanganua habari hiyo na kukuelekeza uudake mpira huo. Jambo hilo lote hutendeka kwa njia yenye kustaajabisha na yenye kutatanisha sana.

Ni nini kilichokusadikisha kwamba kuna Muumba?

Katika mwaka wa 1990, nilikaa kwa miezi michache huko Dublin, Ireland, nikifanya utafiti katika Chuo Kikuu cha Trinity. Nilipokuwa nikisafiri kurudi nyumbani pamoja na mke wangu, Barbara, tulifikiria kuhusu wakati ujao wa watoto wetu. Pia tuliamua kumtembelea dada yangu ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova. Dada yangu alinipa kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kilichochapishwa na Mashahidi. Utafiti wenye kina uliokuwa katika kitabu hicho ulinivutia sana. Kisha nikaanza kutambua kwamba nilikuwa nimekubali fundisho la mageuzi bila kuchunguza ikiwa kuna uthibitisho wa kuliunga mkono. Kwa mfano, nilikuwa ninaamini kwamba mageuzi yanaweza kuthibitishwa na rekodi ya vitu vya kale vilivyochimbuliwa. Lakini hilo si kweli. Kwa kweli, kadiri nilivyochunguza fundisho la mageuzi ndivyo nilivyokuja kuona kwamba nadharia hiyo ni maneno matupu tu na hakuna mambo hakika ya kuiunga mkono.

Nilifikiria kuhusu kazi yangu ya kubuni roboti. Nilikuwa nikiiga ubuni wa nani?

Kisha nilifikiria kuhusu kazi yangu ya kubuni roboti. Nilikuwa nikiiga ubuni wa nani? Siwezi kubuni roboti inayoweza kudaka mpira kama mwanadamu anavyofanya. Roboti inaweza kuwekwa programu ya kudaka mpira, lakini itafanya hivyo kwa kufuata maagizo ambayo tayari yamewekwa. Haiwezi kufanya hivyo bila kutiwa programu hususa. Uwezo wetu wa kujifunza umezidi ule wa mashine kwa kiwango kikubwa sana—na mashine zimetengenezwa na watu fulani! Jambo hilo ni moja tu kati ya mambo mengi yaliyonisaidia nifikie mkataa kwamba lazima tuwe tuliumbwa na mtu fulani.

Kwa nini uliamua kuwa Shahidi wa Yehova?

Sababu moja ni kwamba mimi na Barbara tulipendezwa na jinsi wanavyojifunza kwa kina. Nilipendezwa hasa na jinsi vitabu vyao vinavyofanyiwa utafiti mwingi. Utafiti wenye kina huwapendeza watu kama mimi ambao wangependa kuchimba ili kupata habari hususa. Kwa mfano, nilipendezwa sana na unabii mwingi ulio katika Biblia. Kuchunguza unabii kulinisadikisha kwamba kwa kweli Biblia ni kitabu cha Mungu. Katika mwaka wa 1992, mimi na Barbara tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

Je, kujifunza sayansi kumedhoofisha imani yako?

Tofauti na hilo, sayansi imeimarisha imani yangu. Kwa mfano, fikiria jinsi tunavyotambua nyuso za watu. Mtoto anaweza kuanza kutambua nyuso saa chache tu baada ya kuzaliwa. Mimi na wewe tunaweza kutambua mtu tunayemfahamu mara moja, hata ikiwa yuko katikati ya umati. Hata tunaweza kutambua hali yake ya kihisia. Hata hivyo, huenda tusijue kwamba mfumo wetu wa kuona huchanganua habari nyingi sana na kwa kasi sana ili tufaulu kutambua mambo hayo.

Nimesadikishwa kabisa kwamba mfumo wetu wa kuona ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Yehova Mungu. Zawadi zake, ambazo zinatia ndani Biblia, zinanichochea kumshukuru na kuwaambia wengine kumhusu. Isitoshe, haki inadai kwamba yeye anapaswa kupokea sifa kwa kazi zake zote.