Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Omba Msaada

Omba Msaada

“Tuna marafiki wazuri katika kutaniko letu. Wanatupenda na kututegemeza. Wao ni kama familia yetu.”​—LIZAAN, MAMA YA MATINEJA WAWILI.

Tatizo.

“Matatizo yangu makubwa,” anasema Alina, aliye na wavulana wawili wachanga, “ni kwamba mimi huchoka sana na ninakosa wakati.” Hali anayokabili Alina ni jambo la kawaida kwa akina mama wasio na wenzi. Hiyo ndiyo sababu wazazi wengi wasio na wenzi huwa na orodha ya watu ambao wanaweza kuwaomba msaada bila kuona aibu.

Mapendekezo.

Omba msaada kutoka kwa marafiki na watu wa ukoo wanaotegemeka. Unaweza kuandika orodha ya watu unaoweza kuwaomba wakusaidie kusafiri, kutunza watoto, kufanya ukarabati nyumbani, au wakutegemeze kihisia. Rekebisha orodha hiyo mara kwa mara. Pia chunguza ikiwa kuna msaada wowote unaoweza kupata kutoka kwa serikali au mashirika yasiyo ya kiserikali.

Renata, ambaye ni Shahidi wa Yehova, amesaidiwa sana na Wakristo wenzake. Anasema, “Sikuzote wao huwa tayari kunisaidia. Pindi mmoja mimi na binti zangu wawili wenye umri wa miaka tisa tulipokuwa na mafua, singeweza kupika. Washiriki wa kutaniko waliposikia jambo hilo, kila siku mtu fulani alituletea chakula.” Matendo hayo ya fadhili yanatukumbusha maneno yanayopatikana katika Biblia kwenye 1 Yohana 3:18: “Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”

Je, mzazi huyo mwingine wa watoto wako anaweza kukusaidia kuwalea hata ingawa hana haki kisheria ya kuwalea? Ikiwa huyo mzazi mwingine, hasa baba, anaruhusiwa kisheria kuwa pamoja na watoto kwa muda fulani na anategemeka na angependa kukusaidia, mbona usimruhusu akusaidie? Isitoshe, watoto wako wanahitaji kuwa pamoja na baba yao. *

Wazoeze watoto wako wakusaidie. Unapowapa watoto wako kazi za kufanya kulingana na umri wao, unawasaidia na unajisaidia mwenyewe. Kazi huwafunza watoto kuwa watu wenye kutegemeka na kuwa wafanyakazi wazuri, jambo ambalo litawasaidia sana maishani.

^ fu. 6 Wazazi Wakristo wanapaswa kufuata kanuni za Biblia kadiri wawezavyo chini ya hali zao huku wakitilia maanani masilahi ya watoto wao. Maamuzi ya mahakama yanapaswa kuheshimiwa.