Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baraka Kubwa Zaidi Kuliko Utajiri

Baraka Kubwa Zaidi Kuliko Utajiri

Baraka Kubwa Zaidi Kuliko Utajiri

JON alikuwa na kazi nzuri sana huko Marekani. Hata alipokuwa kijana, alisafiri sehemu mbalimbali za ulimwengu na akachuma pesa nyingi. Yeye na mke wake walikuwa na nyumba maridadi na waliishi maisha ya starehe. Kwa maoni ya wengi, walikuwa wamebarikiwa sana.

Fikiria kisa kingine. Kati ya watu zaidi ya 5,000 waliotuma maombi yao ya kufunzwa kazi katika benki moja mashuhuri huko Ulaya, Kostas * alikuwa mmoja kati ya watu 80 waliochaguliwa. Katika muda wa miaka michache tu alikuwa amepandishwa cheo mara nyingi na mwishowe akawekwa asimamie idara fulani muhimu katika benki nyingine. Kufikia wakati alipoacha kazi hiyo ili aanzishe kampuni yake mwenyewe, alikuwa akipata pesa nyingi kwa mwaka mmoja kuliko pesa ambazo watu wengi hupata maishani mwao. Alihisi kwamba alikuwa amebarikiwa sana.

Hata hivyo, wanaume hao wawili wanasadiki kwamba kuna baraka kubwa zaidi kuliko utajiri. Kwa mfano, leo Jon ni mwalimu wa Biblia anayejitolea kuwasaidia watu wamkaribie Mungu. “Nimejionea kwamba mali hazimletei mtu furaha,” anasema Jon. “Jitihada ya kuzipata na kuzidumisha haimruhusu mtu awe na wakati wa kufanya mambo mengine. Kwa upande mwingine, kuishi kupatana na viwango vya Biblia kunaleta baraka nyingi kama vile, ndoa yenye furaha zaidi, amani ya akili, na dhamiri njema.”

Kostas anasema hivi pia: “Mungu hataki tufuatilie sana mali. Ninahisi kwamba chochote anachotupa zaidi ya mahitaji yetu ya kila siku kinatupa jukumu la kukitumia kupatana na mapenzi yake.” Hivi majuzi, Kostas na familia yake walianza kujifunza lugha nyingine ili wawafundishe watu wengi zaidi kanuni za Biblia. Anasema: “Tumejifunza kwamba kuwapa watu vitu kunatuletea furaha zaidi kuliko kupokea.”—Matendo 20:35.

Kwa kweli, Jon na Kostas wamejifunza kwamba baraka za kiroho ni zenye thamani kuliko utajiri. Daniel Gilbert, profesa katika Chuo Kikuu cha Harvard, anasema kwamba wataalamu wa afya ya akili “wametumia miaka mingi kujifunza uhusiano kati ya mali na furaha, na wamefikia mkataa kwamba mali huongeza furaha ya wanadamu inapowatoa katika umaskini.” Lakini anaongezea hivi: “Baada ya hapo haiongezi furaha.”

Somo Ambalo Wengi Wanajifunza kwa Uchungu

Mtu mmoja alisema hivi: “Mtu anapoacha kuwa maskini ndipo yeye hutambua kwamba kuchuma pesa zaidi hakuna uhusiano wowote na kupata furaha.” Mapema katika karne iliyopita, mwandishi mmoja wa habari alijifunza ukweli wa maneno hayo alipokuwa akimhoji Andrew Carnegie mwanzilishi wa biashara ya chuma, na ambaye wakati huo alikuwa mmoja kati ya watu matajiri zaidi ulimwenguni. “Watu hawapaswi kutamani maisha yangu,” Carnegie akamwambia. “Mali zangu zinaweza kunisaidia jinsi gani? Nina umri wa miaka 60 na mwili wangu hauwezi kumeng’enya chakula. Ningetoa pesa zangu zote ili tu nipate nguvu za ujana na afya.”

Kisha mwandishi huyo akasema hivi: “Bw. Carnegie akageuka kwa ghafula, na kwa sauti nzito yenye uchungu na hisia nyingi zisizoelezeka akasema, ‘Ningeuza chochote nilicho nacho ikiwa ningeweza kuanza maisha yangu upya.’” Akikubaliana na maoni hayo, J. Paul Getty ambaye ni tajiri mkubwa sana mwenye visima vya mafuta, alisema hivi: “Si lazima kuwe na uhusiano wowote kati ya pesa na furaha. Huenda zikamfanya mtu asiwe na furaha.”

Huenda ukakubaliana na mwandikaji wa Biblia aliyeomba hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile chakula nilichoamriwa, nisije nikashiba nikakukana, nikasema: ‘Yehova ni nani?’ wala nisiwe maskini, nikaiba na kulishambulia jina la Mungu wangu.”—Methali 30:8, 9.

Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alieleza hivi: “Nikawa mkuu zaidi na kuongezeka kuliko mtu yeyote aliyenitangulia katika Yerusalemu.” Lakini aliongeza hivi: “Kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo.” Pia Sulemani alisema hivi: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Mhubiri 2:9-11; 5:12, 13; Methali 10:22.

Jinsi ya Kupata Baraka za Milele

Ni wazi kwamba tunaweza tu kupata furaha ya kweli na yenye kudumu tunapotosheleza uhitaji wetu wa kiroho kwa njia inayofaa. Tukimtanguliza Mungu maishani, tutaona kwamba kila sehemu ya maisha yetu inakuwa bora na yenye kuthawabisha zaidi.

Kwa furaha, tunaweza kusema kwamba hatutahangaishwa sikuzote na pesa. Biblia inatuhakikishia kwamba kuna wakati ambapo pupa na biashara za unyonyaji zitakuwa zimeondolewa kabisa. (1 Yohana 2:15-17) Mfumo mpya wa Mungu utakaofuata utaongozwa kwa kanuni zake za uadilifu. Dunia itageuzwa kuwa paradiso kama Mungu alivyokusudia awali alipomuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza. Itakuwa baraka iliyoje kuiona dunia nzima ikiwa imejawa na furaha, amani, na upendo!—Isaya 2:2-4; 2 Petro 3:13; 1 Yohana 4:8-11.

Wakati huo, maisha yatakuwa yenye kupendeza na hayatachosha. Baraka za kimwili zitaambatana na za kiroho, huku Mungu akitimiza kusudi lake la awali kwa wanadamu la kuishi milele katika paradiso duniani. Tumehakikishiwa kwamba kutakuwa na chakula kingi, makao, na kazi yenye kufurahisha kwa ajili ya wote. Umaskini utaondolewa kabisa.—Zaburi 72:16; Isaya 65:21-23; Mika 4:4.

Kila mtu anayemwamini kikweli Yehova, yule Mungu wa Biblia, hatakatishwa tamaa. (Waroma 10:11-13) Kwa hiyo, ni jambo la hekima sasa kufuatia baraka kubwa zaidi kuliko utajiri!—1 Timotheo 6:6-10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jina limebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Tukimtanguliza Mungu maishani, maisha yetu yatakuwa yenye kuthawabisha zaidi

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kutumia pesa kwa hekima kunaweza kufanya maisha yafurahishe zaidi