Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Tarehe ya Hati za Zamani Hujulikanaje? (Februari 2008) Makala hiyo iliniudhi. Ninaelewa kwamba herufi W.K. zinawakilisha “Wakati wa Kawaida” na K.W.K. zinawakilisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.” Tangu nizaliwe miaka 70 iliyopita, nimeona herufi K.K. na A.D. zikitumiwa kuwakilisha kabla na baada ya kuzaliwa kwa Yesu. Kwa maoni yangu, ni kana kwamba kutumia K.W.K. au W.K. kunapinga kwamba Yesu alizaliwa.

R. W., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Ingawa herufi A.D. (Anno Domini, linalomaanisha “katika mwaka wa Bwana wetu”) na K.K. (kabla ya Kristo) zinatumiwa katika nchi zilizo na watu wengi wanaodai kuwa Wakristo, tumechagua kutumia herufi W.K. (Wakati wa Kawaida) na K.W.K. (Kabla ya Wakati wa Kawaida). Kwa nini? Kwanza, kuna uthibitisho wa kutosha kuonyesha kwamba Yesu alizaliwa mwaka wa 2 K.W.K. Pili, vichapo vya Mashahidi wa Yehova vinasambazwa katika lugha zinazosomwa na watu wengi wasio Wakristo. Tatu, jina la cheo “Kristo” lamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Yesu alikuwa Masihi au Kristo alipotiwa mafuta na roho ya Mungu wakati alipobatizwa mnamo 29 W.K. (Mathayo 3:13-17) Kwa hiyo, Yesu hakuwa Kristo alipozaliwa; alikuwa Kristo katika mwaka aliobatizwa. Inafaa kutambua kwamba herufi W.K. na K.W.K. zimeanza kutumika sana na zinaonekana katika karibu kamusi zote za kisasa na vitabu vingine vya wasomi. Uwe na hakika kwamba Mashahidi wa Yehova wanamwona Yesu na dhabihu yake kuwa muhimu sana katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu na wokovu wetu binafsi.

Vijana Huuliza . . . Ninaweza kukabilianaje na ugonjwa au ulemavu? (Februari 2008) Nilithamini sana kupokea makala hiyo kwa wakati unaofaa! Mwezi mmoja hivi uliopita, nilikuwa mgonjwa na nikalazwa hospitalini kwa majuma matatu. Nilikuwa tu nimetoka hospitali nilipopata gazeti hilo. Ningeweza kujiweka katika hali za vijana waliotajwa katika makala hiyo. Asanteni kwa mifano na mashauri yaliyotolewa.

K. P., Kanada

Niliguswa sana moyo kujua kwamba Yehova Mungu anawafariji hata walemavu kama mimi. Nilipokuwa mdogo, iligunduliwa kwamba nilikuwa na ugonjwa wa kupooza ubongo. Ingawa siwezi kutembea, mimi ni painia msaidizi. Ninatazamia wakati ujao katika paradiso duniani ambapo walemavu wote ‘watapanda juu kama vile paa anavyofanya.’—Isaya 35:5, 6.

J. J., Jamhuri ya Korea

Niliisoma makala hiyo tena na tena. Singeweza kujizuia kutokwa na machozi kwa kuwa nilihisi upendo wa Yehova. Ni kana kwamba ametufunika na blanketi yenye joto ili tusipate madhara yoyote. Asanteni sana.

M. T., Japani

Je, Kweli Kifo Ndio Mwisho? (Desemba 2007) Mama yangu alikuwa amekufa miezi michache mapema, na maelezo katika makala hizo, hasa ahadi kuhusu ufufuo ziligusa sana moyo wangu. Asanteni sana. Nilifarijiwa na kutiwa moyo sana.

M. R., Madagaska