Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Hutupata Tunapokufa?

Ni Nini Hutupata Tunapokufa?

Maoni ya Biblia

Ni Nini Hutupata Tunapokufa?

WANA wa kidunia wa Mungu hawakukusudiwa wafe. (Waroma 8:20, 21) Kwa kweli, Yehova alipomtajia Adamu kifo mara ya kwanza, hakuwa akieleza kile ambacho wanadamu walipaswa kutarajia bali alikuwa akizungumzia adhabu ambayo wangepata wakikosa kumtii. (Mwanzo 2:17) Adamu alijua kifo ni nini, kwani alikuwa amewaona wanyama wakifa.

Adamu alipofanya dhambi aliilipia kwa kufa akiwa na miaka 930. (Mwanzo 5:5; Waroma 6:23) Kwa kuwa alikuwa amefukuzwa kutoka kwa familia ya Mungu kwa kutotii, hakuwa mwana wa Mungu tena. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Biblia inasema hivi kuhusu matokeo yenye kuhuzunisha kwa wanadamu wote: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote.”—Waroma 5:12.

Je, Tukifa Tunaweza Kufikiri?

Pia, Biblia inasema: “Kuna mwisho ambao huwafikia wana wa binadamu na mwisho ambao huwafikia wanyama, nao hufikiwa na mwisho uleule. Anavyokufa mmoja, ndivyo anavyokufa yule mwingine; nao wote wana roho moja, hivi kwamba mwanadamu si bora kuliko mnyama, kwa kuwa yote ni ubatili. Wote wanaenda mahali pamoja. Wote wametoka katika mavumbi, nao wote wanarudi mavumbini.” (Mhubiri 3:19, 20) Kurudi mavumbini kunamaanisha nini?

Usemi huo ‘kurudi mavumbini’ unatukumbusha maneno ya Mungu kwa mwanadamu wa kwanza: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Hilo linamaanisha kwamba wanadamu ni viumbe wa kimwili kama wanyama. Sisi si viumbe wa roho ndani ya miili ya nyama. Mwili wetu unapoangamia fikira zetu haziwezi kuokoka. Biblia inasema hivi kuhusu mtu anapokufa: “Anavuta pumzi yake ya mwisho, anarudi mavumbini; na katika saa hiyohiyo fikira zake zote zinakwisha.”—Zaburi 146:4, The New English Bible.

Ikiwa ni hivyo, wafu wako katika hali gani? Neno la Mungu linatupa jibu lililo wazi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Kifo si kama rafiki anayetukaribisha katika maisha bora zaidi, badala yake Biblia inakiita “adui wa mwisho” kwani kinasimamisha shughuli zetu zote. (1 Wakorintho 15:26; Mhubiri 9:10) Je, hiyo inamaanisha kwamba kifo ni hali isiyo na tumaini?

Habari Njema Kuhusu Kifo

Mamilioni ya watu wataamka kutoka katika kifo kama vile mtu anavyoamka kutoka usingizini. Wakati mmoja Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi kuhusu rafiki yao aliyekuwa amekufa: “Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” Yesu alipokuwa akielekea kaburini, alikuta umati wa watu wakiomboleza. Alipofika kaburini aliagiza kwamba kaburi lifunguliwe, kisha akaita kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!” Huyo mtu aliyekuwa mfu siku nne akatoka. (Yohana 11:11-14, 39, 43, 44) Kwa kuwa mwili wa Lazaro ulikuwa umeanza kuoza, Yesu alionyesha kwamba Mungu anaweza kukumbuka kila kitu kuhusu wafu, yaani, utu wao, kumbukumbu zao, na hata sura yao. Anaweza kuwafanya waishi tena. Wakati mwingine Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [yaani, ya Yesu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

Biblia inatuletea habari njema hata zaidi, inasema: “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Wakorintho 15:26) Watu wenye huzuni hawatahitaji tena kwenda makaburini ili kumzika mpendwa wao. Biblia inasema: “Kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Je, hukubali kwamba maoni ya Biblia kuhusu kinachotupata tunapokufa yanafariji?

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, wafu wanajua lolote?—Mhubiri 9:5.

▪ Je, kifo cha wanadamu ni hali isiyo na tumaini?—Yohana 5:28, 29.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Anavuta pumzi yake ya mwisho, anarudi mavumbini; na katika saa hiyohiyo fikira zake zote zinakwisha.” —Zaburi 146:4, “The New English Bible”