Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangilia Katika Tumaini

Shangilia Katika Tumaini

Shangilia Katika Tumaini

JOE alikuwa mahututi akiugua kansa. Mke wake, Kirsten, na marafiki wachache walikuwa kando ya kitanda chake wakizungumza. Kirsten alimtazama mume wake na akaona akidondokwa na machozi. Mwanzoni, alifikiri kwamba Joe alikuwa na maumivu. Huenda Joe alikuwa akihisi maumivu, lakini machozi hayo hayakuwa ya maumivu.

Kirsten anasema: “Wakati huo mgumu, Joe alikuwa amezungukwa na marafiki wa karibu waliokuja kumtembelea. Pia alikuwa na tumaini zuri ambalo alikuwa na uhakika kwamba litatimizwa, na alijua kwamba hakuna mtu anayeweza kumpokonya tumaini hilo. Alikiri kwamba machozi yake yalikuwa ya furaha. Joe alikufa usiku huo.”

Ni tumaini gani hilo lililomtegemeza Joe alipokuwa akiugua? Ni ahadi ya Yehova Mungu ya uzima wa milele katika paradiso duniani tukiwa na afya kamilifu. (Zaburi 37:10, 11, 29) Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linasema hivi: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu. . . Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani [kutia ndani matatizo mengi ya leo] yamepitilia mbali.”

Tumaini Hata kwa Wafu

Kutimizwa kwa ahadi hiyo kunamaanisha kwamba Joe atafufuliwa. Kwa kweli, alifarijiwa na ahadi ya Yesu kwamba “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho,” yaani, wafu ambao wako katika kumbukumbu la Mungu, watafufuliwa. (Yohana 5:28, 29) Je, unahuzunika kwa sababu umefiwa na mshiriki wa familia au rafiki? Ikiwa ndivyo, tumaini la ufufuo linaweza kukuchangamsha. Ni kweli kwamba tumaini hilo haliondoi uchungu mwingi tunaohisi tunapompoteza mpendwa wetu. Yesu ‘alitokwa na machozi’ rafiki yake Lazaro alipokufa. Lakini tumaini letu hupunguza uchungu tunaohisi.—Yohana 11:14, 34, 35; 1 Wathesalonike 4:13.

“Joe alipokufa kutokana na kansa, nilihisi kwamba sitakuwa na furaha tena,” anasema Kirsten. “Hata sasa, miaka michache baadaye, ninatambua kwamba maisha yangu katika mfumo huu hayatakuwa sawa tena. Joe aliacha pengo ambalo haliwezi kuzibwa. Hata hivyo, ninaweza kusema kwa unyoofu kwamba sasa nina amani ya akili na uradhi tena.”

Maneno ya Kirsten yanatukumbusha kwamba katika mfumo wa sasa hatuwezi kububujika kwa furaha kila wakati. Maisha ni kupanda na kushuka. Kuna nyakati ambazo tunapaswa kuhuzunika, ambapo haingefaa kabisa kufurahi. (Mhubiri 3:1, 4; 7:2-4) Pia, huenda baadhi yetu tunakabiliana na mshuko-moyo, ambao unaweza kusababishwa na mambo mbalimbali. Hata hivyo, ahadi za Biblia hufariji sana, na hekima ya Biblia isiyo na kifani inaweza kutusaidia tuepuke hatari ambazo hufanya tusiwe wenye furaha. Mungu anasema: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:33.

Naam, Yehova anapendezwa nasi kikweli. Anataka tuwe na furaha, si ya kijuu-juu tu, bali ya moyoni na, si kwa miaka michache tu, bali milele! Kwa hiyo, Mwana wake alisema maneno haya yasiyoweza kupitwa na wakati: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Ni jambo la hekima kutenda kupatana na maneno yake.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Mambo Tisa Yanayochangia Furaha

1. Kusitawisha uthamini kwa ajili ya mambo ya kiroho.Mathayo 5:3.

2. Kuridhika, na kuepuka “kupenda pesa.”1 Timotheo 6:6-10.

3. Kuweka raha mahali panapofaa.2 Timotheo 3:1, 4.

4. Kuwa mkarimu, na kujitahidi kuwafurahisha wengine.Matendo 20:35.

5. Kuwa mwenye shukrani, na kufikiria baraka zako.Wakolosai 3:15.

6. Kuwa mwenye kusamehe.Mathayo 6:14.

7. Kuchagua marafiki kwa hekima.Methali 13:20.

8. Kutunza mwili wako, na kuepuka mazoea mabaya.2 Wakorintho 7:1.

9. ‘Kushangilia katika tumaini’ linalotajwa katika Biblia.Waroma 12:12.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Tumaini la Biblia la kuishi katika ulimwengu mpya ni chanzo cha faraja kuu