Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inawezekana Kuishi Bila Woga?

Je, Inawezekana Kuishi Bila Woga?

Je, Inawezekana Kuishi Bila Woga?

JE, MTU anayeishi katika ulimwengu huu hatari anaweza kuishi bila woga kabisa? Huenda isiwezekane. Hata watu wanaomwamini Mungu hukabili hatari zinazowafanya wawe na wasiwasi. Kwa mfano, katika karne ya kwanza W.K. mtume Paulo aliyesafiri kwa mapana na marefu alitaja kwamba alivunjikiwa na meli, akapata hatari kutokana na mito, hatari kutoka kwa wanyang’anyi wa njia kuu, na hatari ndani ya jiji. (2 Wakorintho 11:25-28) Vivyo hivyo leo, wengi wetu hulazimika kukabiliana na hali hatari.

Hata hivyo, tunaweza kuchukua hatua za kujilinda na kwa kupunguza hatari, huenda tukapunguza wasiwasi. Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Tunaweza kuchukua hatua zipi zinazofaa?

Kuchukua Hatua za Kujilinda

Inapendeza kwamba ingawa Biblia iliandikwa zamani sana, ina kanuni nyingi ambazo bado zinaweza kutumiwa ili kuepuka hatari leo. Kwa mfano, inasema: “Mtu yeyote mwenye hekima, macho yake yamo katika kichwa chake; lakini mjinga anaendelea kutembea katika giza tupu.” (Mhubiri 2:14) Ni jambo la hekima kujua ni nani aliye karibu nawe na kuepuka mahali penye giza iwezekanapo. Huenda ukatumia barabara zilizo na nuru ya kutosha unaporudi nyumbani, hata ikiwa itamaanisha kutembea umbali mrefu kidogo. Pia Biblia inasema: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja . . . Mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake.” (Mhubiri 4:9, 12) Ikiwa unaishi eneo hatari, je, unaweza kupanga urudi nyumbani pamoja na mtu mwingine?

Ukishambuliwa na jambazi, ni jambo la hekima kukumbuka kwamba uhai ni wenye thamani zaidi kuliko mali. (Mathayo 16:26) Pia ni jambo la hekima kukumbuka kwamba umati wenye hasira unapokusanyika, ni hatari na unaweza kufanya jambo lolote.—Kutoka 23:2.

Ukisumbuliwa na mtu fulani anayejaribu kukutongoza, kukuambia mizaha michafu, au kukugusa kwa njia isiyofaa, ni vizuri kumkataza kwa uthabiti. Huenda ikakubidi kuondoka kama Yosefu alivyofanya wakati mwanamke fulani asiye na maadili alipomshika. ‘Alikimbia na kwenda nje.’ (Mwanzo 39:12) Ikiwa huwezi kuondoka, unaweza kusema: “Acha kufanya hivyo!” au “Usiniguse!” au “Sifurahishwi na maneno hayo.” Ukiweza, epuka maeneo ambako watu husumbuliwa kwa ukawaida.

Kukabiliana na Woga Nyumbani

Unaweza kufanya nini ikiwa unamwogopa mume mjeuri? Ni vizuri kufikiria jinsi unavyoweza kutoroka iwapo mwenendo wa mume wako utahatarisha afya au uhai wako au wa watoto wako. * Biblia inasimulia jinsi Yakobo alivyopanga kwa uangalifu namna ambavyo angetoroka ikiwa ndugu yake Esau angekuwa mjeuri. Kama ilivyotukia, hakuhitaji kufanya hivyo, lakini lilikuwa jambo la hekima kufanya mpango huo. (Mwanzo 32:6-8) Njia ya kutorokea inaweza kutia ndani kutafuta mtu unayeweza kukimbilia kwake hali ya dharura inapotokea. Unaweza kuzungumza na mtu huyo mapema kuhusu mahitaji yako. Huenda ikafaa kuweka hati na vitu vingine muhimu mahali unapoweza kuvipata kwa urahisi.

Pia huenda ukamripoti mume wako anayekutendea vibaya kwa wenye mamlaka na kutafuta ulinzi wao. * Biblia inafundisha kwamba lazima kila mtu akabiliane na matokeo ya matendo yake. (Wagalatia 6:7) Biblia husema hivi kuhusu mamlaka za serikali: “Hiyo ni mhudumu wa Mungu kwako kwa faida yako. Lakini ikiwa unafanya mabaya, ogopa.” (Waroma 13:4) Kupigwa nyumbani ni uhalifu mbaya kama tu kupigwa barabarani. Pia katika nchi nyingi ni kosa kunyemelea watu.

Kuchukua hatua ambazo tumezungumzia kunaweza kupunguza woga kwa kiasi fulani. Lakini Biblia haitoi tu mashauri yanayofaa. Ni kitabu chenye unabii unaotegemeka ambacho hufunua yale ambayo Mungu anafanya sasa na atakayofanya wakati ujao. Biblia inatoa tumaini gani kwa watu ambao hulazimika kuishi kwa woga?

Woga Mwingi Uliopo Unaonyesha Nini?

Mtume Paulo aliandika maneno haya muhimu: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema.” (2 Timotheo 3:1-3) Bila shaka maneno hayo yanataja nyakati zenye kuogopesha sana!

Yesu alipozungumzia “umalizio wa mfumo wa mambo,” alisema hivi: “Taifa litasimama kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi, na katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni na upungufu wa chakula; kutakuwa na mambo yenye kuogopesha na ishara kubwa kutoka mbinguni.” (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11) Kwa hiyo, hatupaswi kushangazwa na “mambo yenye kuogopesha” ambayo tumeona na ambayo yamechangia woga mwingi leo. Lakini yanamaanisha nini?

Yesu alisema: “Mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Luka 21:31) Katika siku zetu, tunaweza kutazamia serikali ya Mungu itawale kutoka mbinguni juu ya wanadamu wote. (Danieli 2:44) Maisha yatakuwaje wakati huo?

Kuishi Bila Woga!

Biblia inaeleza kuhusu wakati ujao ambapo vita vitakwisha, hakutakuwa na watenda maovu, nayo dunia itajaa watu wanaompenda Mungu. Petro, mtume wa Yesu, aliandika kuhusu “siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu” itakayokuja wakati ujao. Hakutakuwa na mtu yeyote mwovu wa kuogopwa kwani “uadilifu utakaa” duniani. (2 Petro 3:7, 9, 13) Hebu wazia kitulizo tutakachopata kuishi miongoni mwa watu wanaotumainiana na kupendana kikweli! Tumaini hilo hutusaidia tuwe na maoni yanayofaa kuhusu nyakati hizi hatari. Hazitaendelea kuwapo milele.—Zaburi 37:9-11.

Nabii wa Yehova aliambiwa hivi kwa faida ya wale wanaohangaika: “Waambieni wale wanaohangaika moyoni: ‘Iweni na nguvu. Msiogope. Tazameni! Mungu wenu atakuja na kisasi, Mungu akiwa na malipo. Yeye mwenyewe atakuja na kuwaokoa ninyi.’” (Isaya 35:4) Kwa hiyo, watumishi wa Mungu wa kweli wanaweza kutazamia wakati ujao wakiwa na uhakika. (Wafilipi 4:6, 7) Watu ambao wamelazimika kuishi kwa woga, wanafarijika sana kujua kwamba Yehova hajabadili kusudi lake la awali kwamba dunia ijawe na watu wanaomjua na wanaoonyesha sifa zake zenye upendo.—Mwanzo 1:26-28; Isaya 11:9.

Tunajua kwamba hakuna jambo linaloweza kumzuia Yehova asitimize makusudi yake yenye upendo kwa ajili ya wanadamu. (Isaya 55:10, 11; Waroma 8:35-39) Tunapoelewa hilo, maneno ya Zaburi inayojulikana sana huwa na maana ya pekee. Tunasoma hivi: “Yehova ni Mchungaji wangu. . . . Anaiburudisha nafsi yangu. Ananiongoza katika mapito ya uadilifu kwa ajili ya jina lake. Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami.” (Zaburi 23:1-4) Ingawa huenda nyakati zenye kuogopesha zikawa mbaya sana, kwa hakika hivi karibuni kutakuwa na ulimwengu usio na woga.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kuhusu hali zinazopatana na kanuni za Biblia ambazo zinaweza kumfanya mtu atengane na mwenzi wake wa ndoa, ona gazeti la Amkeni!, Februari 8, 2002, ukurasa wa 10.

^ fu. 10 Kuhusu watu waliopatwa na jeuri nyumbani, ona gazeti la Amkeni!, Novemba 8, 2001, ukurasa wa 3 hadi 12, na Amkeni!, Februari 8, 1993, ukurasa wa 3 hadi 14.

[Picha katika ukurasa wa 8-10]

Hivi karibuni, Mungu ataleta ulimwengu usiokuwa na woga