Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unapaswa Kuogopa Har-magedoni?

Je, Unapaswa Kuogopa Har-magedoni?

Maoni ya Biblia

Je, Unapaswa Kuogopa Har-magedoni?

“HAR-MAGEDONI” ni nini? Kwa ufupi, neno hilo linawakilisha hali ambayo watawala wa ulimwengu wanakusanywa ili kumpinga Mungu na Ufalme wake ulio mkononi mwa Yesu Kristo. Katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, mtume Yohana aliona maono ya watawala waliokusanyika pamoja kumpinga Mungu katika mahali pa mfano panapoitwa Har–Magedoni.

Neno “Har–Magedoni” linapatikana mara moja tu katika Biblia, lakini leo katika lugha fulani neno hilo hutumiwa sana kwa njia ya mfano. Neno hilo limetumiwa kuwakilisha msiba mkubwa au mdogo, iwe ni maangamizi makubwa ya nyuklia au programu hatari zinazoharibu kompyuta. Vitabu kadhaa ambavyo vimeuzwa sana vimezungumzia kile kinachoitwa mwisho wa dunia, au kipindi kabla tu ya Har–Magedoni. Nakala milioni 60 za kitabu kimoja cha hadithi kinachotegemea kichwa hicho zimeuzwa katika miaka kumi iliyopita.

Watu fulani huogopa Har–Magedoni. Wanahisi kuwa magaidi, mataifa yanayochochea vita, au misiba isiyoweza kuzuiwa na mwanadamu itaangamiza ulimwengu mzima, na kuifanya dunia isiweze kutegemeza uhai. Wengine wanaamini kwamba katika wakati wake, Mungu mwenyewe atakasirika na kuiangamiza sayari yetu na kila kitu kilichomo. Maoni hayo yanatisha kwelikweli! Lakini ni maoni gani yaliyo sahihi kuhusu “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” kwenye Har–Magedoni?—Ufunuo 16:14, 16.

Je, Dunia Itaharibiwa?

Si wanadamu wote watakaoharibiwa kwenye Har–Magedoni. Tunajuaje? Biblia inatuhakikishia kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.” (2 Petro 2:9) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atadhibiti nguvu zake nyingi kikamili. Ni wale tu wanaopinga enzi kuu ya Mungu ndio tu watakaopatwa na hasira yake kwenye Har–Magedoni. Watu wasio na hatia hawataumia.—Zaburi 2:2, 9; Mwanzo 18:23, 25.

Biblia inatuambia kwamba Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Basi, ni wazi kwamba Yehova Mungu hakusudii kuiangamiza sayari yetu. Badala yake, ataondoa wanadamu waovu wanaopinga utawala wake. Hilo linapatana na yale aliyofanya wakati wa Gharika ya siku za Noa.—Mwanzo 6:11-14; 7:1; Mathayo 24:37-39.

‘Siku Yenye Kuogopesha’

Kwa kweli, unabii mbalimbali wa Biblia kuhusu uharibifu unaokuja unaogopesha. Kwa mfano, nabii Yoeli alizungumza kuhusu “siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.” (Yoeli 2:31) Silaha za Mungu zinatia ndani theluji, mvua ya mawe, matetemeko ya nchi, magonjwa ya kuambukiza, mvua kubwa yenye mafuriko, mvua ya moto na kiberiti, mvurugo unaosababisha kifo, radi, na tauni inayofanya nyama ioze. * (Ayubu 38:22, 23; Ezekieli 38:14-23; Habakuki 3:10, 11; Zekaria 14:12, 13) Nayo Biblia inafafanua waziwazi wakati ambapo maiti zitafunika dunia, ili kuwa mbolea au chakula cha ndege na wanyama wengine. (Yeremia 25:33, 34; Ezekieli 39:17-20) Maadui wa Mungu wataogopa sana wakati wa vita hivyo.—Ufunuo 6:16, 17.

Je, hilo linamaanisha waabudu watiifu wa Mungu wa kweli wanapaswa kuogopa mambo yenye kushangaza yatakayotukia wakati wa Har–Magedoni? La hasha, kwani watumishi wa Mungu walio duniani hawatashiriki katika vita hivyo. Isitoshe, Yehova atawalinda. Hata hivyo, waabudu wa kweli watashangazwa na wonyesho wenye kuogopesha wa nguvu za Mungu.—Zaburi 37:34; Methali 3:25, 26.

Kwa kupendeza, mtume Yohana aliongozwa na roho kutuhakikishia hivi: “Mwenye furaha ni yeyote anayeshika maneno ya unabii wa kitabu hiki cha kukunjwa,” kutia ndani onyo kuhusu Har–Magedoni. (Ufunuo 1:3; 22:7) Mtu anawezaje kuwa mwenye furaha kwa kutafakari kuhusu Har–Magedoni? Hilo linawezekanaje?

Mungu Atoa Wito wa Kuchukua Hatua

Wakati kimbunga au tufani kali inapokaribia, wenye mamlaka wa eneo fulani hutoa maonyo ya kuokoa uhai. Ili kuhakikisha kwamba kila mtu anasikia onyo hilo, polisi wanaweza kutumwa wakiwa na vifaa vya kutoa onyo au kutoka nyumba moja hadi nyingine. Kusudi si kuwaogopesha watu bali ni kuwasaidia wachukue hatua ya kujiokoa. Watu wenye utambuzi hushukuru kwa onyo hilo, na wale wanaochukua hatua hufurahi kwamba walifanya hivyo.

Hilo linapatana na onyo la Yehova kuhusu “upepo wa dhoruba” unaokaribia wa Har–Magedoni. (Methali 10:25) Yehova ametoa habari nyingi kuhusu vita vyake katika Neno lake. Hataki kuwaogopesha bali anataka kutoa onyo la kutosha na kuwaongoza watu watubu na waazimie kumtumikia. (Sefania 2:2, 3; 2 Petro 3:9) Wale wanaochukua hatua hiyo wataokoka. Kwa hiyo, hatuhitaji kuogopa vita vya Mungu vinavyokaribia. Badala yake, tunatazamia wakati ujao tukiwa na uhakika kwamba “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.”—Yoeli 2:32.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ni muhimu kukumbuka kuwa sehemu fulani za Biblia ziliandikwa kwa kutumia lugha ya mfano, au “ishara.” (Ufunuo 1:1) Kwa hiyo hatupaswi kushikilia sana maoni kwamba mambo yanayotajwa katika unabii huo mbalimbali ni halisi.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wakati dhoruba kali inapokaribia, wenye mamlaka wa eneo fulani hutoa maonyo ya kuokoa uhai

[Picha katika ukurasa wa 13]

Onyo la Mungu kuhusu Har–Magedoni ni wito wa kuokoa uhai