Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?

KULINGANA na historia, mtu anayeitwa Yesu alizaliwa zaidi ya miaka 2,000 iliyopita katika mji mdogo unaoitwa Bethlehemu katika nchi ya Yudea. Wakati huo, Herode Mkuu alikuwa mfalme wa Yerusalemu, naye Kaisari Augusto alikuwa maliki wa Roma. (Mathayo 2:1; Luka 2:1-7) Kwa ujumla, wanahistoria Waroma wa karne mbili za kwanza waliepuka kumtaja Yesu kwa kuwa watawala wa Roma walikuwa wakijaribu kuukandamiza Ukristo wakati huo.

Kwa upande mwingine, kichapo kimoja (The Historians’ History of the World) kinasema: “Hata watu ambao hawakuwa wafuasi wa dini waliona wazi kwamba utendaji [wa Yesu] uliathiri historia kwa njia ya pekee sana kuliko utendaji wa mtu mwingine yeyote katika historia. Hata mataifa mengi yenye ustaarabu yanakubali kwamba enzi mpya ilianza wakati [Yesu] alipozaliwa.”

Gazeti moja (Time) liliripoti kwamba vitabu vingi zaidi vimeandikwa kumhusu Yesu kuliko mtu mwingine yeyote katika historia. Vingi kati ya vitabu hivyo hujibu swali, Yesu ni nani? Yaelekea kwamba kumekuwa na ubishi mkubwa zaidi kuhusu suala hilo kuliko kuhusu habari nyingine yoyote katika historia ya wanadamu.

Yesu Alikuwa Nani?

Maria alipoambiwa kwamba angepata mtoto na kumwita Yesu, aliuliza: “Hilo litawezekanaje, kwa kuwa silali na mwanamume?” Malaika Gabrieli aliyetumwa na Mungu akamjibu hivi: “Nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.”Luka 1:30-35.

Baadaye, Yesu alifanya miujiza iliyowastaajabisha mitume wake. Dhoruba kali ilipotishia kupindua mashua yao kwenye Bahari ya Galilaya, Yesu aliyatuliza maji kwa kuyakemea: “Nyamaza, utulie!” Kwa mshangao, mitume wake wakauliza: “Kwa kweli huyu ni nani?”Marko 4:35-41; Mathayo 8:23-27.

Watu wengi walioishi siku zake, walitaka kujua Yesu ni nani, kwa hiyo, Yesu aliwauliza mitume wake watu wanasema yeye ni nani. “Baadhi yao husema Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, na wengine bado Yeremia au mmoja wa manabii.” Wote hao walikuwa tayari wamekufa. Kisha Yesu akawauliza: “‘Ninyi mnasema mimi ni nani?’ Simoni Petro akajibu, akasema: ‘Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.’” Hata mashetani—malaika waovu—walisema hivi kumhusu Yesu: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu.”Mathayo 16:13-16; Luka 4:41.

Yesu Alisema Yeye Ni Nani?

Ingawa mara nyingi Yesu hakujitambulisha kuwa Mwana wa Mungu, alikubali kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. (Marko 14:61, 62; Yohana 3:18; 5:25, 26; 11:4) Hata hivyo, karibu kila wakati alisema kwamba alikuwa “Mwana wa binadamu.” Kwa kujitambulisha hivyo, alikazia kuzaliwa kwake akiwa mwanadamu. Kwa kufanya hivyo, alijitambulisha pia kuwa “mwana wa binadamu” ambaye Danieli alikuwa amemwona katika maono akiwa mbele za Mungu Mweza-Yote, yule “Mzee wa Siku.”—Mathayo 20:28; Danieli 7:13.

Badala ya kujitangaza mwenyewe kuwa Mwana wa Mungu, Yesu aliacha watu wafikie mkataa huo wao wenyewe. Na hata watu wengine mbali na mitume wake walifikia mkataa huohuo, kutia ndani Yohana Mbatizaji na Martha, rafiki ya Yesu. (Yohana 1:29-34; 11:27) Watu hao waliamini kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Walijua kwamba aliishi mbinguni akiwa mtu wa kiroho mwenye nguvu na kwamba Mungu aliuhamisha uhai wake kimuujiza hadi kwenye tumbo la bikira Maria.—Isaya 7:14; Mathayo 1:20-23.

Alilingana na Mtu wa Kwanza, Adamu

Yesu alilingana sana na mwanadamu wa kwanza, Adamu. Kwa mfano, wote wawili walikuwa wanadamu wakamilifu wasio na baba wa kibinadamu. (Mwanzo 2:7, 15) Kwa hiyo, Biblia inamwita Yesu “Adamu wa mwisho”—mwanadamu mkamilifu ambaye angeweza kuwa “fidia inayolingana.” Maisha ya Yesu yalilingana na ya “mtu wa kwanza Adamu,” ambaye Mungu alimuumba akiwa mkamilifu.—1 Wakorintho 15:45; 1 Timotheo 2:5, 6.

Katika Biblia, Adamu wa kwanza anaitwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Hata hivyo, alipomwasi Mungu kimakusudi, Adamu huyo wa kwanza alipoteza uhusiano wake wenye thamani wa kuwa mwana wa Mungu. Kwa upande mwingine, sikuzote Yesu alikuwa mwaminifu kwa Baba yake wa mbinguni naye aliendelea kuwa Mwana wa Mungu anayekubalika. (Mathayo 3:17; 17:5) Biblia inasema kwamba wote wanaomwamini Yesu na kumkubali kuwa Mwokozi wao, wanaweza kupata uzima wa milele.—Yohana 3:16, 36; Matendo 5:31; Waroma 5:12, 17-19.

Hata hivyo, watu fulani hudai kwamba Yesu si Mwana wa Mungu tu bali ni Mungu mwenyewe. Wanasema kwamba yeye na Baba yake ni Mungu Mweza-Yote. Je, ni kweli? Je, Yesu ni Mungu? Je, ndivyo alivyosema Yesu au waandikaji wengine wa Biblia? Kwa kweli, ni nani aliye Mungu wa pekee wa kweli? Yesu alisema Mungu huyo ni nani? Na tuchunguze jambo hilo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

Hakuna Ajulikanaye Zaidi

Masimulizi na maisha ya Yesu yaliandikwa na watu wanne walioishi wakati huo, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Wawili kati yao walikuwa rafiki zake wa karibu. Vitabu walivyoandika vinaitwa Injili, baadhi yake vimetafsiriwa katika lugha zaidi ya elfu mbili. Vitabu hivyo vidogo ni sehemu ya Biblia. Vitabu hivyo vya Injili vikiwa kimoja-kimoja au pamoja na vitabu vingine vya Biblia vimesambazwa sana kuliko maandishi mengine yoyote katika historia. Basi, si ajabu kwamba Yesu anajulikana zaidi kuliko mtu mwingine yeyote aliyepata kuishi!

[Picha katika ukurasa wa 3]

Mitume waliuliza: “Kwa kweli huyu ni nani?”