Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unahitaji Kuwa na Kiasi Unapokusanya Vitu

Unahitaji Kuwa na Kiasi Unapokusanya Vitu

Unahitaji Kuwa na Kiasi Unapokusanya Vitu

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI AUSTRALIA

JE, WEWE hukusanya vitu ambavyo unafikiri utavihitaji siku moja? Huenda ukavitupa unapotambua kwamba huvihitaji. Hata hivyo, watu wengi hufurahia kukusanya vitu ambavyo huenda hawatavitumia kwa njia yoyote. Watu hao wamesitawisha mazoea ya kukusanya vitu.

Watu fulani ambao wana mazoea hayo hupenda kukusanya vitu vya kawaida kama vile mawe, stempu, au sarafu za kale. Wengine hupenda kukusanya vitu vya kuchezea, vijiko, medali, kadi za posta, vitu vya kale, kanda za muziki, vitu wanavyopata wanapokwenda kutalii, na kadhalika. Kwa mfano, wakili mmoja huko Marekani amekusanya misumari 200,000 ya reli! Yeye ni mmoja kati ya mamia ya watu ambao hutembea katika maeneo ya mashambani wakitafuta misumari ya reli iliyotumiwa zamani ambayo ina chapa ya tarehe.

Gazeti Harper’s Magazine linasema: “Watu hukusanya vitu vya kushangaza, kama vile meno, nywele bandia, mafuvu, mikebe ya biskuti, . . . nywele, feni, tiara, koleo, mbwa, sarafu, mikongojo, chiriku, na viatu, . . . vifungo, mifupa, pini za kofia, sahihi bandia, matoleo ya kwanza ya vichapo, na vitambaa vya kuzuia gesi.”

Pia kuna watu ambao hukusanya vitu vya ajabu. Fikiria kisa cha mwanamke mmoja mwenye cheo huko Urusi ambaye alikusanya karai za kuendea haja ambazo zilikuwa zimetumiwa na watu matajiri na maarufu. Mtu mmoja mwenye cheo huko Japani alikusanya mbwa 5,000 na kuwafuga katika nyumba zilizopambwa sana. Kulingana na gazeti Harper’s Magazine, mkusanyaji mmoja tajiri alikusanya maelfu ya viroboto “na aliwahifadhi katika vyombo vyenye kemikali vilivyokuwa na majina ya mahali ambapo walipatikana na majina ya wanyama au watu waliokuwa na viroboto hao.”

Zoea la kukusanya vitu lilianza zamani za kale. Kwa mfano, zoea la kukusanya vitabu na hati ni la zamani sana. Kitabu Light From the Ancient Past husema kwamba Mfalme Ashurbanipal wa Ashuru (wa karne ya saba K.W.K.) aliwatuma waandishi wake kotekote ili wakusanye nakala za maandishi na hati za awali kwa ajili ya maktaba yake huko Ninawi. Jumba la kifalme la Ashurbanipal lilichimbuliwa mwaka wa 1853 likiwa na maktaba hiyo yenye kustaajabisha.

Pia, watawala Wagiriki na Waroma walijulikana sana kwa zoea la kukusanya vitu. Kitabu Collecting—An Unruly Passion kinasema: “Katika enzi za Cicero na Kaisari, Roma lilijulikana kwa anasa zake na ukusanyaji wa vitu. . . . Wauzaji wa sanaa walipatikana katika majengo mengi ya jiji. Hata baadhi ya wakaaji matajiri walikuwa na nyumba za kuonyesha vitu walivyokusanya.”

Kwa Nini Watu Hupenda Kukusanya Vitu?

Kwa nini watu hufurahia kukusanya vitu leo? Kitabu The Encyclopedia Americana kinasema hivi: “Watu hufanya mambo kwa sababu mbalimbali, lakini sababu yao kuu ni kujifurahisha. Mambo yanayofurahisha hustarehesha na huwapumzisha watu baada ya shughuli zao za kawaida.” Wengi hufurahia kuchunguza vitu wanavyopenda ambavyo wamekusanya.

Makala moja katika gazeti Canberra Times la Australia linasema kwamba vitu vilivyokusanywa “vinaweza kumkumbusha mtu mahali na watu ambao alikuwa amewasahau. Mtu anapokusanya vitu vya kale, yeye hukumbushwa ustadi na miradi ya vizazi vya zamani na huthamini maendeleo yaliyopo sasa.” Naam, mtu anaweza kujifunza mambo mengi kwa kukusanya vitu. Kwa mfano, Rex Nan Kivell, alikuwa mkusanyaji maarufu nchini Australia. Alikusanya vitu 15,000 kuhusu historia ya kale ya Australia na New Zealand.

Watu wengi hupenda kukusanya vitu kwa sababu wanaamini vinaweza kuwaletea pesa nyingi wakati ujao. Gazeti Utne Reader linasema: “Kwa nini mtu atumie dola 80 kununua ‘tiketi za awali za 1969 za [maonyesho ya muziki wa roki ya] Woodstock’ pamoja na barua ya kuthibitisha kwamba tiketi hizo ni za kweli hata ingawa hakuhudhuria maonyesho hayo? . . . Leo, kukusanya vitu vinavyohusiana na umaarufu ni biashara kubwa.”

Hata hivyo, kuna tahadhari. Makala ileile ya The Canberra Times inaonya hivi: “Ijapokuwa kukusanya vitu hufurahisha, kuna hatari. Wauzaji wengine si waaminifu na kuna vitu vingi bandia vinavyouzwa kwa kukiuka kanuni za haki na za adili.” Inavunja moyo kama nini kugundua kwamba kitu ni bandia baada ya kukinunua kwa pesa nyingi! Maneno ya Methali 14:15 yanawafaa sana wakusanyaji wa vitu: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”

Unahitaji Kuwa na Kiasi

Zoea la kukusanya vitu linaweza kuchukua wakati, nguvu, na pesa nyingi. Mwanamke mmoja anayekusanya vitu alisema hawezi kudhibiti tamaa yake ya kukusanya vitu. Alastair Martin, ambaye amekusanya vitu kwa muda mrefu, alisema kwamba wakusanyaji fulani “hufanya mambo ya ajabu sana.”

Katika kitabu chake Collecting—An Unruly Passion, Werner Muensterberger alisema: “Unapowatazama wakusanyaji, utatambua mara moja kwamba wana tamaa isiyodhibitiwa ya kupata vitu. . . . Kile kinachofanya zoea la kukusanya vitu lionekane kuwa la ajabu si zoea lenyewe bali ni jinsi wakusanyaji wengi wanavyojiendesha kwa kuwa na tamaa kubwa sana ya kupata vitu, jinsi wanavyosisimuka wanapovipata na kufadhaika wanapovipoteza, na nyakati nyingine kuwa na maoni na tabia za kiajabu-ajabu.”

Je, Mkristo anapaswa kuruhusu zoea lolote analopenda limfanye atende mambo ya kipumbavu au yenye kuaibisha? La. Biblia inatuhimiza “kuwa na kiasi.” (1 Petro 1:13, Union Version) Ijapokuwa huenda ukafurahia zoea unalolipenda, hilo si mojawapo ya “mambo yaliyo ya maana zaidi” ambayo mtu anayempendeza Mungu anapaswa kuhangaikia. (Wafilipi 1:10) Jifunze kutokana na Mfalme Sulemani. Alitumia utajiri wake mwingi kukusanya nyumba, mashamba ya mizabibu, miti, na mifugo mingi sana. Sulemani alisema: “Sikuyanyima macho yangu chochote ambacho yaliomba.” Lakini je, aliridhika alipotumia maisha yake kukusanya vitu vyote hivyo? Sulemani alijibu hivi: “Na mimi, naam, mimi nikageuka kuelekea kazi zangu zote ambazo mikono yangu ilikuwa imefanya na kuelekea kazi ngumu niliyokuwa nimejitahidi kuitimiza, na, tazama! kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:3-11.

Unaweza kufanya nini ili kuzuia zoea lako la kukusanya vitu lisichukue mahali pa mambo yaliyo muhimu zaidi? Jiulize hivi: ‘Ningependa kutumia muda mwingi kadiri gani kukusanya vitu?’ Tambua kwamba mbali na wakati unaotumia kukusanya vitu, unahitaji pia wakati ili kuvitunza, kuvisafisha kwa ukawaida, kuvipanga, kuvitazama, na kuvilinda. Vipi gharama zinazohusika? Je, zoea hilo litamaliza pesa ambazo unahitaji ili kutunza familia yako? (1 Timotheo 5:8) Je, unaweza kujizuia kununua kitu fulani ikiwa huwezi kukigharimia? Naam, hata ukijitahidi juu chini, huwezi kukusanya kila kitu. Kile ambacho Sulemani alisema kuhusu vitabu kinahusu pia vitu vingine ambavyo mtu anaweza kukusanya: “Hakuna mwisho wa kutungwa kwa vitabu vingi, na kushughulika navyo sana huuchosha mwili.” (Mhubiri 12:12) Kwa hiyo, kama vile kanuni za Kikristo zinavyoonyesha, ni muhimu kuwa na kiasi.

Kama ilivyotajwa mapema, wengine wamesema kwamba zoea la kukusanya vitu haliwezi kudhibitiwa. Lakini si lazima iwe hivyo. Zoea hilo linaweza kumfurahisha, kumburudisha, na hata kumwelimisha mtu iwapo ana maoni yanayofaa na anakusanya vitu kwa kiasi.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ni jambo la hekima kufikiria wakati na gharama inayohusika katika zoea lolote unalolipenda