Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kila Mtu Anapaswa Kusoma Kitabu Hiki”

“Kila Mtu Anapaswa Kusoma Kitabu Hiki”

“Kila Mtu Anapaswa Kusoma Kitabu Hiki”

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI POLAND

Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kilitolewa katika lugha nyingi wakati wa makusanyiko yaliyofanywa ulimwenguni kote mwaka wa 2003. Kama ilivyokuwa katika sehemu nyingine, watu huku Poland walifurahia sana kupata kitabu hicho chenye picha zinazovutia. Ingawa kitabu hicho kimechapishwa hasa kwa ajili ya watoto wadogo, barua zilizotoka kwa vijana na watu wazima zimeonyesha kwamba watu wa umri mbalimbali wanakifurahia. Haya ni baadhi ya maelezo yao.

“Jina langu ni Agata, nami nina umri wa miaka minane. Mara tu nilipopata kitabu hiki, nilihisi kwamba Yehova ananijali kwelikweli. Ninapenda hasa sura ya 7 yenye kichwa, ‘Utii Unakulinda Wewe.’ Nyakati nyingine nimekosa kuwatii wazazi wangu, lakini sasa ninafahamu kwamba lazima nibadilike kwa sababu Yehova anawapenda watoto watiifu.”

Marlena, msichana mwenye umri wa miaka 13, aliandika hivi kwa uthamini: “Ninajua kwamba kitabu hiki kimechapishwa hasa kwa ajili ya watoto wadogo, lakini nadhani kinawavutia watu wote. Ninapokisoma, imani yangu katika Yehova na Yesu huimarishwa. Hata mambo magumu yanaelezwa kwa njia rahisi. Sitaki kuacha kukisoma. Nazo picha zinavutia sana! Maswali yanayoambatana na picha hizo yatachochea upendezi wa vijana. Kitabu hiki kinapendeza, kwa hiyo ninakisoma kwa makini. Asanteni sana.”

Justyna, msichana mwenye umri wa miaka 15, anaeleza jinsi amependezwa na kitabu hicho: “Sura ambazo nimesoma zimenipendeza sana, nami nashukuru sana kwa sababu ya zawadi hii yenye kupendeza na yenye kuelimisha. Ninafikiri kwamba kila mtu anapaswa kusoma kitabu hiki, hata watu wenye umri mkubwa. Mifano inayotolewa katika kitabu hiki ni rahisi, nami nafikiri kwamba inaweza kueleweka hata na mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja. Nazo picha zinafundisha. Siwezi hata kueleza jinsi ninavyohisi ninaposoma kitabu hiki.”

Pia, Eunika alishukuru kwa kupokea kitabu hicho. Ingawa ana umri wa miaka 19, alisoma kitabu hicho kipya na anasema aliona kuwa “kinawafaa hata vijana.” Anaandika hivi pia: “Kina mashauri mengi mazuri kwa ajili ya maisha yetu ya kila siku, tuwe nyumbani, shuleni, na hata kutanikoni. Ninawashukuru sana kwa zawadi hii.”

Maria, ambaye ni mama ya mtoto aliye na umri wa mwaka mmoja anayeitwa Oliwia, alisema hivi baada ya kuona jinsi binti yake alivyofurahia picha zenye kuvutia: “Ninawashukuru kwa moyo wangu wote kwa ajili ya kitabu hiki cha pekee cha kuwafundisha watoto. Binti yetu Oliwia amevutiwa sana na kitabu hiki. Yeye huketi juu ya mapaja yetu na kutuuliza yale yaliyomo katika sura moja baada ya nyingine. Alipendezwa sana na picha iliyo kwenye ukurasa wa 83, inayoonyesha wasichana wawili wa rangi tofauti wakikumbatiana. Picha nyingine ni halisi sana hivi kwamba yeye huzigusa, huzikumbatia, na hata kutabasamu anapozitazama.”

Maria pia anakazia jinsi kitabu hicho kinavyoelimisha: “Kinashughulikia mambo muhimu kama vile ngono (ukurasa wa 58-60) na kutendewa vibaya kwa watoto (ukurasa wa 170-171). Kitabu hiki ni msaada mzuri kwa wazazi wanaotaka kuwalea watoto wao kwa njia nzuri katika ulimwengu huu mwovu ambao una hatari nyingi sana.”

Wachapishaji wa kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu wanatumaini kwamba kitabu hicho kitakusaidia wewe na watoto wako mfaidike na mambo ambayo Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, aliwafundisha watu karibu miaka 2,000 iliyopita.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Agata

[Picha katika ukurasa wa 31]

Marlena

[Picha katika ukurasa wa 31]

Eunika

[Picha katika ukurasa wa 31]

Maria na Oliwia

[Picha katika ukurasa wa 31]

Justyna