Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Wanyama-Vipenzi Asanteni sana kwa mfululizo wenye kichwa “Unawaonaje Wanyama-Vipenzi?” (Februari 22, 2004) Nilifurahia jinsi makala hizo zilivyoandikwa, kwani zilionyesha upendo na fadhili kuwaelekea wanyama. Nitampa daktari anayetibu wanyama wangu gazeti hilo. Makala kama hizo zinaweza kuwachochea watu wanaopenda wanyama wamkaribie Yehova.

O. M., Italia

Nimeanza kuishi peke yangu hivi karibuni, na kwa sasa ninawatunza paka wawili wadogo. Mimi hufurahia sana kuwa nao, lakini pia ninaona umuhimu wa kutowatendea kama wanadamu. Makala hizo zilinisaidia kuelewa umuhimu wa kuwa na kiasi tunaposhughulika na wanyama-vipenzi.

K. O., Japani

Asanteni sana. Majuma matatu yaliyopita niliamua mbwa wangu mwenye umri wa miaka 13 auawe ili kumaliza maumivu yake. Hilo lilikuwa mojawapo ya maamuzi magumu zaidi niliyowahi kukabili. Asubuhi hiyo nilisoma tena mfululizo huo kuhusu wanyama-vipenzi. Mfululizo huo uliandikwa kwa fadhili na huruma nao ulinisaidia sana.

S. G., Marekani

Ninafanya kazi kwa mtu anayejulikana sana kwa sababu ya mchango wake katika biashara ya chakula cha wanyama-vipenzi. Niliacha gazeti lililozungumzia wanyama-vipenzi juu ya kinara cha kupigia chapa. Nilipoenda kula chakula cha mchana, aliona gazeti hilo, akalisoma, na kulifurahia sana hivi kwamba akasema angependa kupokea Amkeni! kwa ukawaida.

L. W., Marekani

Makala hizo zilikuwa safi sana nazo zilinisaidia niwe na kiasi ninaposhughulika na wanyama-vipenzi. Ningependa tu kusema kwamba mtu anapotaka kufuga mbwa au paka, anapaswa kufikiria kuondoa uwezo wake wa kuzalisha. Sababu moja inayofanya mbwa na paka wengi wauawe kila mwaka ni kwamba hakuna makao ya kutosha ya kuwatunzia.

C. B., Marekani

“Amkeni!” linajibu: Asante sana kwa kuwafahamisha wasomaji wetu jambo hilo.

Makala yenu ilisema kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “wanyama wote, wawe ni wa kufugwa au wa mwituni, wataishi kwa amani wao kwa wao.” Je, inafaa kuamini kwamba wanyama-wawindaji hawatakuwapo wakati huo?

D. B., Kanada

“Amkeni!” linajibu: Mambo mengi yamebadilika duniani tangu mwanadamu alipofanya dhambi. Wakati ujao tutaona jinsi unabii wa Biblia kuhusu uhusiano wenye amani kati ya wanyama utakavyotimizwa katika Paradiso. Hata hivyo, tuna hakika kabisa kwamba Muumba wetu ataondoa vitu vyote vinavyoweza kusababisha madhara duniani.—Zaburi 37:10, 11.

Kutembea Asanteni kwa makala yenye kichwa “Faida za Kutembea.” (Februari 22, 2004) Inafaidi kujua kwamba kwa kutembea, mtu anaweza kupunguza hatari ya kupata ugonjwa wa moyo na kiharusi. Makala hiyo ilinisaidia kuona kwamba nilikuwa nimeishi maisha ya kizembe kwa muda mrefu sana. Nitafuata shauri na kutembea kwa ukawaida.

L. B., Sweden

Ngono ya Simu Ningependa kushukuru kwa makala yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Ngono ya Simu Ina Ubaya Gani?” (Februari 22, 2004) Nimefadhaishwa sana na tatizo hilo zito. Hali yangu ya kiroho ilidhoofika, hatimaye nikafanya dhambi nzito, na kupoteza mapendeleo. Yehova na aendelee kuwapa hekima mnapotayarisha makala nyingine zitakazotusaidia kudumu tukiwa na nguvu kiroho.

J. H., Hispania