Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vipi Kwenda Disko?

Vipi Kwenda Disko?

Vijana Huuliza . . .

Vipi Kwenda Disko?

“Nilienda huko kwa kusudi moja tu—kujifurahisha.”—Shawn.

“Kusema kweli, niliponda raha sana. Mambo yalikuwa bambam! Nilicheza dansi mpaka che.”—Ernest.

KATIKA miaka ya karibuni, disko zimependwa sana. Vijana wengi wanaotaka kuponda raha huenda disko kwa ukawaida.

Bila shaka, sote tunapenda kujifurahisha. Biblia husema kwamba kuna “wakati wa kucheka” na hata “wakati wa kucheza ngoma.” (Mhubiri 3:4, Verbum Bible) Hata hivyo, je, kwenda disko ni tafrija inayofaa? Au je, tunapaswa kufikiri kwa uzito kabla ya kwenda disko?

“Karamu za Kupindukia”

Ijapokuwa Biblia haishutumu karamu za kiasi, inaonya kuhusu “karamu za kupindukia.” (Wagalatia 5:19-21) Katika nyakati za Biblia, karamu za kupindukia zilitokeza matendo mapotovu. Nabii Isaya aliandika hivi: “Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema ili watafute tu kileo, wanaokawia mpaka giza la jioni sana hivi kwamba divai inawawasha! Na kutakuwa na kinubi na kinanda, tari na filimbi, na divai katika karamu zao; lakini hawauangalii utendaji wa Yehova.”—Isaya 5:11, 12.

Katika karamu hizo kulikuwa na “kileo” na muziki usiofaa. Zilianza mapema na kwisha usiku sana. Ona pia kwamba watu walioshiriki karamu hizo walitenda kana kwamba hakuna Mungu! Basi, si ajabu kwamba Mungu alishutumu karamu hizo. Hata hivyo, Mungu anayaonaje mambo yanayofanywa katika disko nyingi leo?

Fikiria mambo haya. Kwanza, katika disko fulani watu huinuliwa na umati na kurushwa-rushwa hewani huku wengine wakicheza dansi kwa kichaa. Gazeti moja linasema kwamba kucheza dansi kwa kichaa “kulianza katikati ya miaka ya 1980 katika disko za Marekani baada ya kipindi cha harakati za punk. Dansi hiyo ilitokana na . . . mtindo wa watu kugongana wanapocheza dansi.” Dansi hiyo hutia ndani kurukaruka, kutikisa kichwa kupita kiasi, kuigiza jinsi wanyama hugongana vichwa, na kugongana wakati wa kucheza dansi. Mara nyingi, watu huvunjika na kujeruhiwa miguu na mikono, na wengine wamepata majeraha ya uti wa mgongo na ya kichwa. Hata wengine hufa. Katika dansi ya kurushwa-rushwa juu, mtu huinuliwa na kubebwa juu kwa juu na umati. Wengi wao huanguka na kuumia. Mara nyingi wasichana hupapaswa na kushikwa-shikwa isivyofaa.

Hapana shaka kwamba Mungu hakubali mwenendo huo. Neno lake linawaamuru Wakristo ‘wakatae kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na waishi kwa utimamu wa akili.’—Tito 2:12.

Muziki na Dawa za Kulevya

Fikiria pia muziki unaochezwa kwenye disko nyingi. Disko nyingine hucheza muziki wa roki wenye mdundo mzito au muziki wa heavy metal, ambao una mdundo mzito na maneno machafu. Lakini katika disko nyingi muziki wa rapu ndio unaopendwa. Muziki huo pia huzungumzia ngono, jeuri, na uasi. Je, unaweza kuathiriwa unapocheza dansi ya muziki huo mahali pasipofaa? David Hollingworth, mshauri wa mambo ya disko alisema: “Muziki unaathiri watu sana kiakili na kihisia. Wanapokuwa katika umati, muziki unaweza kuwachochea kuwa wajeuri.” Si ajabu kwamba visa vya jeuri vimetokea katika disko za majiji kadhaa ya Marekani. Watu wengi wanaona kwamba jambo hilo husababishwa na muziki unaotukuza mwenendo mchafu na ukatili. *

Katika miaka ya karibuni dawa za kulevya zimetumiwa pia katika disko. Mtafiti mmoja alisema kwamba “disko zimependwa sana . . . kwa sababu dawa mbalimbali za kulevya zinapatikana na kutumiwa huko.” Hata kuna dawa za kulevya zinazoitwa dawa za kucheza dansi. Watu fulani wanaopenda kwenda disko hutumia dawa kadhaa pamoja. Kati ya dawa za kulevya zinazotumiwa pamoja ni ketamine ambayo inaweza kusababisha matatizo ya kihisia, kuchanganyikiwa, kushindwa kupumua, na kuharibika kwa mfumo wa neva. Dawa ya methamphetamine inaweza kumfanya mtu asahau mambo, awe mjeuri, na anaweza kupata magonjwa ya moyo na ya neva. Dawa ya ecstasy inayotokana na kemikali ya amphetamine inapendwa sana. Inaweza kusababisha kuchanganyikiwa, mahangaiko, ongezeko la mpigo wa moyo, kupanda kwa shinikizo la damu, na homa kali sana. Baadhi ya watu waliotumia dawa hizo wamekufa.

Matumizi ya dawa za kulevya hayapatani na amri ya Biblia inayosema “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Je, inafaa kuwa mahali ambapo dawa za kulevya zinatumiwa sana?

Mashirika Mabaya

Kumbuka onyo hili ambalo hunukuliwa mara nyingi: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Kama wale watu walioshiriki karamu za kupindukia katika nyakati za Biblia, inaonekana vijana wengi wanaopenda kwenda disko hawahangaikii kumpendeza Mungu. Wengi wanaweza kufafanuliwa kuwa watu “wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:4) Je, ungependa kushirikiana kwa ukaribu na umati wenye sifa hiyo?

Huenda wengine wakasema kwamba hakuna hatari kubwa kwenda disko pamoja na vijana wengine Wakristo. Hata hivyo, haielekei kwamba vijana Wakristo ambao ni ‘kielelezo kwa waaminifu katika mwenendo’ watakubali kwenda huko. (1 Timotheo 4:12) Hata kikundi cha vijana Wakristo kikienda disko na kubaki pamoja bila kuachana, bado kutakuwa na muziki mchafu na hali zisizofaa. Huenda wakajipata taabani wakati watu wengine wanapowaomba kucheza dansi nao. Vijana wengine hata wamejiingiza katika vita! Hivyo Biblia inasema kweli inaposema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

Dansi za Kuamsha Nyege

Sasa, fikiria dansi yenyewe. Kuna dansi fulani isiyo ya kawaida ambayo inapendwa sana, hasa na vijana nchini Marekani. Dansi hiyo huchezwa kuambatana na muziki wa rapu wenye maneno machafu ya ngono. Isitoshe, dansi yenyewe huchezwa kwa kuiga tendo la ngono. Hata njia ya kucheza dansi hiyo imefafanuliwa kuwa ‘kufanya ngono ukiwa na nguo.’

Je, inafaa kijana Mkristo ashiriki dansi kama hiyo? Hawezi kufanya hivyo ikiwa anataka kumpendeza Mungu anayetuamuru ‘tuukimbie uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18) Huenda wengine wakasema, ‘Kwa kuwa kila mtu anacheza dansi hiyo, basi haina ubaya wowote.’ Hata hivyo, umati wa watu unaweza kukosea. (Kutoka 23:2) Uwe na ujasiri wa kutotenda kama wengine na udumishe dhamiri njema mbele za Mungu!—1 Petro 4:3, 4.

Kuamua

Hiyo haimaanishi kwamba dansi zote ni mbaya. Biblia inasema kwamba Mfalme Daudi alifurahi sana baada ya kurudi Yerusalemu na sanduku takatifu la agano hivi kwamba ‘alicheza dansi kwa nguvu zake zote.’ (2 Samweli 6:14) Katika mfano wa Yesu kuhusu mwana mpotevu, kulikuwa na shangwe na “sauti za muziki na dansi” mwana huyo aliporudi.—Luka 15:25.

Huenda aina fulani za dansi zikakubaliwa na Wakristo mahali unapoishi. Hata hivyo, ni muhimu kuwa na usawaziko na utambuzi. Ni salama zaidi kufurahia muziki na dansi kwenye karamu za Wakristo ambazo zimesimamiwa vizuri kuliko kwenye disko za vijana. Kwenye karamu za Wakristo zinazosimamiwa vizuri, vijana hufurahia ushirika unaofaa na Wakristo wa umri mbalimbali badala ya kujitenga.

Naam, huenda kuna mikahawa mahali unapoishi ambayo huwa na muziki na dansi zinazokubalika. Lakini kabla ya kukubali kwenda huko unapoalikwa, ni jambo la busara kujiuliza maswali kama vile: Mahali hapo pana sifa gani? Je, ni mahali pa vijana tu? Ikiwa ndivyo, je, kweli ni mahali panapofaa? Ni muziki wa aina gani utakaochezwa? Ni dansi za aina gani zinazochezwa huko? Wazazi wangu wataonaje nikienda huko? Kujiuliza maswali kama hayo kunaweza kukulinda.

Shawn, aliyenukuliwa mwanzoni, anamalizia kwa kauli safi. Kabla ya kuwa Mkristo, alizoea kwenda disko. Anasema hivi: “Kuna mwenendo mwingi mpotovu kwenye disko. Kwa kawaida muziki huwa mchafu, mtindo wa kucheza dansi haupatani na maadili, na watu wengi huenda huko wakiwa na kusudi—wanataka kutoka huko na mtu wa kufanya ngono naye.” Shawn aliacha kwenda disko baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baada ya kupitia hali zenye kuhuzunisha, anatoa kauli hii: “Disko haziwafai Wakristo.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ona makala “Sababu Inayofanya Muziki Utuathiri,” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 8, 1999.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Vijana wengine wameingia taabani kwenye disko