Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hekima ya Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Kutatanisha

Hekima ya Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Kutatanisha

Hekima ya Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Kutatanisha

“Mungu humpa mtu anayempendeza hekima na ujuzi na shangwe.”—MHUBIRI 2:26, THE NEW ENGLISH BIBLE.

SI RAHISI kufanya maamuzi yenye hekima na yanayofaa kimaadili katika ulimwengu ambamo matibabu na tekinolojia inazidi kuwa tata. Hebu angalia baadhi ya maendeleo ya karibuni ambayo yamezusha mzozo. Sasa wanawake wanaweza kuharibu mimba ambayo hawataki kwa kumeza tu tembe za kuondoa mimba. Wanasayansi wanaweza sasa kubadili maumbile ya chembe za urithi katika mimea na wanyama. Maabara zinang’ang’ania kupata chembe muhimu za msingi kutoka kwa viinitete vya wanadamu, na watu wengi wanatumaini kwamba jitihada hizo zitaleta mabadiliko makubwa ya kitiba.

Jitihada hizo za kujaribu kubadili maumbile ya asili zinawatia wasiwasi na woga watu wengi, mbali na kuwatatanisha kimaadili. Matokeo hayo yanatukumbusha maneno haya ya Biblia: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Naam, kama watoto wanavyohitaji kuongozwa na wazazi, ndivyo wanadamu wote wanavyohitaji mwongozo wa Baba yetu wa mbinguni ili watembee kwa hekima.—Mithali 1:33.

Hekima ya Kumsikiliza Mungu

Sisi humsikiliza Mungu kwa kusoma na kufuata Neno lake lililoandikwa. Ni kweli kwamba Biblia haizungumzii masuala yote magumu ya kisayansi na ya kitiba yanayotukabili leo. Hata hivyo, kanuni zake ambazo zinadumu milele, zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima.—1 Petro 1:25.

Kwa mfano, fikiria mzozo unaosababishwa na chembe za msingi za kiinitete. Kama tulivyoona, kiinitete kilicho hai huangamizwa ili chembe zake za msingi zichukuliwe. Francis Collins, mkurugenzi wa Taasisi ya Kitaifa ya Utafiti wa Chembe za Urithi za Wanadamu huko Marekani, alisema hivi kuhusu tatizo la kimaadili linalozuka: “Jambo hilo linaonyesha wazi mgongano uliopo kati ya kanuni mbili muhimu sana. Kanuni moja ni utakatifu wa uhai wa wanadamu na kanuni ya pili ni wajibu mzito tulio nao wa kukomesha mateso na kutibu magonjwa hatari . . . Nadhani watu wengi wana sababu nzuri ya kufikiri kwamba utafiti wa kutumia chembe zinazotolewa kwenye kiinitete cha mwanadamu unakiuka kanuni ya utakatifu wa uhai wa wanadamu.”

Biblia inatusaidia kuelewa suala hili zito kwa kutueleza maoni ya Mungu kuhusu watoto wasiozaliwa bado. Katika Israeli la kale, Mungu alimwona mtu aliyemjeruhi mwanamke mjamzito au mtoto wake asiyezaliwa bado, kuwa muuaji. Alitozwa “uhai kwa uhai.” * (Kutoka 21:22, 23) Kwa hiyo, tunaweza kusema kwa uhakika kwamba Muumba anaona uhai wa kila mwanadamu kuwa mtakatifu, hata uhai wa mtoto asiyezaliwa bado. Kwa kweli, Mungu hupendezwa nasi tunapokuwa tungali tumboni, kama mtunga-zaburi anavyofunua: “Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; chuoni mwako ziliandikwa zote pia.”—Zaburi 139:16.

Licha ya maendeleo makubwa ya kitekinolojia ambayo yamefanywa na wanadamu, Biblia inatusaidia kuwa na mtazamo wenye kiasi na ulio halisi kuelekea wanadamu na mambo ambayo wametimiza. Inasema hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hana nguvu za kuokoa. Pumzi yake hutoka, huurudia udongo; saa ileile mawazo yake hukoma.” (Zaburi 146:3, 4, New English Bible) Huenda watu wengine wakatilia shaka maneno hayo. Lakini je, ni yenye kutiliwa shaka? Je, si maneno hakika na ya kweli? Bila shaka, kwa sababu hata mwanadamu mwenye nguvu zaidi ya wote hawezi kujizuia asizeeke, asiwe mgonjwa, na hatimaye kujizuia asife—sembuse kuwazuia wengine wasipatwe na mambo hayo.

Lakini Muumba hana mipaka kama yetu. Isitoshe, ana “nguvu za kuokoa” na ana nia ya kufanya hivyo. Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Yesu alipokuwa duniani alitupatia sababu ya ‘kudhihirisha imani,’ kwa kuwaponya wagonjwa wote na walemavu waliomjia. Naam, hata alifufua wafu!—Luka 7:21, 22.

Yesu alionyesha kimbele mpango wa Mungu wa kuwaponya wanadamu wote, Ufalme wake utakapoanza kuitawala dunia kikamili. Watu husali juu ya Ufalme huo katika ile inayoitwa kwa kawaida Sala ya Bwana. Mapenzi ya Mungu yatafanywa hapa duniani kupitia Ufalme wa Mungu peke yake, yaani, serikali ya mbinguni ya Mungu iliyo mikononi mwa Yesu Kristo.—Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

Je, ahadi hizo za Biblia zinakupa tumaini? Na je, unataka kufanya yote uwezayo umpendeze Mungu kwa kujitahidi kujua maoni yake kuhusu masuala mengi magumu yanayotukabili? Ikiwa ndivyo, basi tunakutia moyo usikilize na kutii Neno la Mungu. Kwa kweli lina hekima ya kutuwezesha kuishi—naam, kuishi milele na milele.—Yohana 17:3; 2 Timotheo 3:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Watu fulani wamedai kwamba sheria hii ilihusu kumjeruhi mama peke yake. Hata hivyo, maandishi ya awali ya Kiebrania hayasemi hivyo. Wasomi wa Biblia wenye kuheshimiwa C. F. Keil na F. Delitzsch wanasema kwamba kulingana na maandishi ya Kiebrania, “yaonekana maneno hayo hayahusu kamwe kumjeruhi mwanamke peke yake.”—Ona Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 1977, Kiingereza, ukurasa wa 478.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Biblia inatoa mwongozo sasa na tumaini hakika la kuwa na uhai mkamilifu wakati ujao