Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pambano la Muda Mrefu Dhidi ya Utumwa

Pambano la Muda Mrefu Dhidi ya Utumwa

Pambano la Muda Mrefu Dhidi ya Utumwa

“Huu ndio ufafanuzi wa utumwa: kudhulumiwa na kuvumilia, kustahimili udhalimu kwa sababu ya kuogopa kutendewa ukatili.”—Euripides, Mgiriki aliyekuwa mwandishi wa michezo ya kuigiza katika karne ya tano K.W.K.

UTUMWA umekuwepo kwa muda mrefu na mara nyingi umekuwa wenye ukatili. Tangu zama za ustaarabu wa Misri na Mesopotamia, mataifa yenye uwezo yalitumikisha mataifa jirani yasiyokuwa na uwezo. Basi, huo ukawa mwanzo wa mojawapo ya matendo mabaya zaidi ya dhuluma.

Kati ya mwaka wa 2000 na 1000 K.W.K., Misri ilitumikisha taifa zima lenye mamilioni ya watu. (Kutoka 1:13, 14; 12:37) Wakati Ugiriki ilipotawala eneo la Mediterania, familia nyingi za Wagiriki zilikuwa na angalau mtumwa mmoja—kama vile familia za kawaida katika nchi fulani leo zinavyoweza kuwa na gari moja. Mwanafalsafa Mgiriki Aristotle alifanya zoea hilo lionekane kuwa halali aliposema kwamba wanadamu wamewekwa katika vikundi viwili, yaani, kuna mabwana na watumwa, na mabwana huzaliwa wakiwa na haki ya kuamuru, na watumwa huzaliwa tu ili watii.

Waroma waliendeleza utumwa hata kuliko Wagiriki. Katika siku za mtume Paulo, huenda nusu ya idadi ya wakazi wa jiji la Roma—yamkini mamia ya maelfu ya watu—walikuwa watumwa. Na yaonekana kwamba Milki ya Roma ilihitaji watumwa nusu milioni kila mwaka ili kujenga minara ya ukumbusho, kuchimba migodi, kulima, na kufanya kazi katika nyumba kubwa za matajiri. * Kwa kawaida, watu waliotekwa vitani walifanywa kuwa watumwa. Basi, yawezekana kwamba Milki ya Roma iliendeleza vita hasa kwa sababu ilihitaji watumwa wengi zaidi.

Japo utumwa ulipungua kwa kadiri fulani baada ya kuanguka kwa Milki ya Roma, zoea hilo liliendelea. Kitabu Domesday Book (1086 W.K.) kinasema kwamba asilimia 10 ya wafanyakazi huko Uingereza katika Zama za Kati (500-1500 W.K.) walikuwa watumwa. Na bado watumwa walipatikana kupitia vita.

Hata hivyo, tangu wakati wa Kristo, bara la Afrika ndilo limeathiriwa zaidi na matokeo ya biashara ya watumwa kuliko bara jingine lolote. Hata kabla ya wakati wa Yesu, Wamisri wa kale waliwauza na kuwanunua watumwa Waethiopia. Katika kipindi cha miaka 1,250 hivi, inakadiriwa kwamba Waafrika milioni 18 walipelekwa Ulaya na Mashariki ya Kati kwa sababu ya uhitaji mkubwa wa watumwa huko. Wakati Amerika ilipofanywa kuwa koloni kuanzia miaka ya 1500, watumwa walianza kupelekwa huko pia, na biashara ya kuwasafirisha watumwa kupitia kwenye bahari ya Atlantiki ikawa mojawapo ya biashara kubwa zaidi ulimwenguni. Wanahistoria wanakadiria kwamba kati ya mwaka wa 1650 na 1850, zaidi ya watumwa milioni 12 walihamishwa kutoka Afrika. * Wengi waliuzwa katika masoko ya watumwa.

Mapambano Dhidi ya Utumwa

Katika karne zilizopita, mataifa na watu mbalimbali wamepigania uhuru kutoka utumwani. Katika karne ya kwanza kabla ya Kristo, Spartacus aliongoza jeshi la watumwa Waroma 70,000 ili kupigania uhuru, lakini hakufua dafu. Karne mbili hivi zilizopita, watumwa Wahaiti walifanya mapinduzi yaliyofanikiwa na serikali huru ilianzishwa mnamo mwaka wa 1804.

Utumwa ulidumu kwa muda mrefu zaidi huko Marekani. Watumwa fulani walipambana juu chini ili wao na wapendwa wao wapate uhuru. Na watu fulani waliokuwa huru walipinga sana utumwa kwa kuteta ukomeshwe au kwa kuwasaidia watumwa watoro. Hata hivyo, ni katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1800 ndipo utumwa ulipopigwa marufuku hatimaye katika sehemu zote za nchi hiyo. Lakini, vipi leo?

Je, Mapambano Hayo Yameambulia Patupu?

Azimio la Watu Wote la Haki za Binadamu linasema hivi: ‘Hakuna mtu atakayewekwa utumwani wala kutumikishwa; aina zote za utumwa na za biashara ya watumwa hazitaruhusiwa.’ Kwa wazi, mradi huo, ambao ulitangazwa kwa bidii mnamo mwaka wa 1948, ni mradi mzuri. Watu wengi wenye nia njema wametenga wakati wao, nguvu zao, na mali zao ili kufanikisha mradi huo. Hata hivyo, si rahisi kupata mafanikio.

Kama makala iliyotangulia inavyosema, mamilioni ya watu wangali wanafanya kazi kwa jasho bila malipo katika hali mbaya sana, na wengi wao wamenunuliwa au kuuzwa kwa lazima. Japo watu wenye nia nzuri wamejitahidi kukomesha utumwa—na mikataba ya kimataifa imetiwa sahihi ili kuupiga marufuku—bado ni vigumu kwa watu wote kupata uhuru wa kweli. Biashara ya ulimwenguni pote imewezesha biashara haramu ya watumwa kuchuma fedha nyingi. Yaonekana hata utumwa unaendelea kuimarika. Je, kuna tumaini lolote? Hebu tuone.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kitabu kimoja cha kale kinasema kwamba huenda ikawa Waroma fulani matajiri sana walikuwa na watumwa 20,000.

^ fu. 7 Wahubiri fulani wa uwongo walidai kwamba Mungu alikubali biashara hiyo ya watumwa yenye ukatili. Hivyo, watu wengi wangali wanadhani kwamba Biblia huunga mkono ukatili huo, na kumbe haifanyi hivyo. Tafadhali ona makala yenye kichwa “Maoni ya Biblia: Je, Mungu Alikubali Biashara ya Watumwa?” katika toleo la Amkeni! la Septemba 8, 2001.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Hapo zamani, mara nyingi watumwa waliosafirishwa kwa meli (juu) kutoka Afrika waliuzwa katika masoko ya watumwa huko Amerika

[Hisani]

Godo-Foto

Archivo General de las Indias