Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilikuwa Mwanasiasa Lakini Sasa Mimi Ni Mkristo

Nilikuwa Mwanasiasa Lakini Sasa Mimi Ni Mkristo

Nilikuwa Mwanasiasa Lakini Sasa Mimi Ni Mkristo

LIMESIMULIWA NA LADISLAV ŠMEJKAL

Baada ya kuhukumiwa, nilirudishwa kwenye seli yangu. Punde, nikaanza kumpitishia ujumbe rafiki yangu aliyekuwa kwenye ghorofa ya pili juu yangu kwa njia ya mawasiliano ya kugonga ukuta ya Morse. Alikuwa akingoja kusikia nimepata kifungo cha muda gani.

“Miaka 14,” nikamgongea ukutani.

Hakuweza kuamini jambo hilo. Kwa hiyo akauliza: “Miezi 14?”

“La, miaka 14,” nikamjibu.

JAMBO hilo lilitukia mwaka wa 1953, huko Liberec, Chekoslovakia (ambayo sasa ni Jamhuri ya Cheki). Nilikuwa mwanasiasa mwenye umri wa miaka 19. Nilitaka mabadiliko ya kisiasa. Sisi wanasiasa tulieneza maoni yetu kwa kugawanya makaratasi yaliyochambua Chama cha Kikomunisti kilichokuwa kinatawala wakati huo. Utendaji wetu ulionwa kuwa uhaini mkubwa, ndiyo sababu nikahukumiwa kifungo kirefu gerezani.

Tayari nilikuwa nimekaa kizuizini kwa mwaka mmoja hivi kabla ya hukumu yangu kutangazwa. Kabla ya kuhukumiwa, wafungwa wawili-wawili walikuwa wakiwekwa katika seli moja, na mara kwa mara walipelekwa kuhojiwa wakiwa wamefunikwa macho. Hatukuruhusiwa kuongea katika seli zetu, kwa hiyo tulinong’onezeana au kuwasiliana kwa njia ya mawasiliano ya kugonga ukuta ya Morse.

Upesi niligundua kwamba wengi kati ya wale waliokuwa gerezani walikuwa Mashahidi wa Yehova. Huko gerezani, kulikuwa na desturi ya kuhamisha wafungwa kutoka seli moja hadi nyingine baada ya kila mwezi mmoja au miwili. Kwa kuwa nilipendezwa na Biblia, nilifurahi hatimaye waliponiweka katika seli pamoja na Shahidi mmoja. Baada ya muda, nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi.

Labda unaweza kusema kwamba mazungumzo yetu yalikuwa mafunzo ya Biblia hata ingawa hatukuwa na Biblia wala vichapo vya Biblia. Kwa kweli, sikuwa nimewahi kuona Biblia maishani mwangu. Lakini tulizungumza—Shahidi huyo alinieleza habari za Biblia ambazo alikumbuka—nami niliandika aliyosema huku tukinong’onezeana tukiwa tumeketi karibu sana.

Tulikuwa tu na karatasi ya chooni na kichana. Nilitumia kichana kuandika kwenye karatasi ya chooni. Niliyakariri maandiko mengi. Mashahidi walionifunza walinifundisha nyimbo za Ufalme pia. Shahidi mmoja aliniambia hivi: “Sasa uko gerezani ukiwa mfungwa wa kisiasa, lakini wakati ujao unaweza kufungwa kwa sababu wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”

Hatimaye, baada ya mahoji mengi, nilihukumiwa na kupelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu karibu na mji wa Jáchymov. Kufikia wakati huo nilikuwa na hakika kwamba siku moja ningekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Miaka Mingi Gerezani

Nilipofika kwenye kambi hiyo ambapo madini aina ya yuraniamu yalichimbwa, mara moja nikaanza kuwatafuta Mashahidi. Lakini upesi nikagundua kwamba walikuwa wamehamishwa na kupelekwa mahali pengine. Hata hivyo, Shahidi mmoja alibaki kwa sababu alikuwa mpishi. Alinikopesha Biblia ambayo ilikuwa imechakaa sana na iliyokuwa imefichwa mahali pengi. Kwa hiyo niliweza kusoma maandiko ambayo tayari nilikuwa nimeyakariri. Wakati nilipokuwa nikisoma nilijiambia, ‘Naam, ni kama tu vile akina ndugu walivyonifundisha.’

Baada ya mwezi mmoja, nilihamishwa hadi kwenye kambi iliyoitwa Bytiz, karibu na mji wa Příbram. Nikiwa huko nilikutana na Mashahidi wengine. Huko Bytiz tulipokea kwa ukawaida vichapo vya Biblia ambavyo vilikuwa vinaingizwa kambini kisiri. Ijapokuwa wasimamizi wa kambi walijaribu kujua vilitufikia jinsi gani, hawakuwahi kujua kamwe. Wafungwa 14 walikuwa wakiwahubiria wengine kwa ukawaida. Nusu ya idadi hiyo walikuwa Mashahidi waliobatizwa, na sisi wengine tulikuwa tumekubali imani ya Mashahidi tukiwa gerezani.

Wengi wetu tulitaka kuonyesha kupitia ubatizo wa maji kwamba tumejiweka wakfu kwa Mungu. Lakini kwa sababu ya kukosa maji—au wacha niseme kwa usahihi zaidi, kwa sababu ya kukosa chombo kikubwa vya kutosha cha maji—haikuwa rahisi kupanga kuwe na uzamisho. Kwa hiyo, wakati huo iliwabidi wengi wangoje mpaka wafunguliwe ili wabatizwe. Hata hivyo, katika kambi ya Bytiz, kulikuwa na minara mikubwa yenye maji ya kupozea migodi ya makaa ya mawe. Katikati ya miaka ya 1950, baadhi yetu tulibatizwa katika tangi moja katika minara hiyo.

Miaka michache baadaye, mnamo Machi 1960, niliitwa na afisa mmoja wa polisi ambaye alisimamia wafungwa wa kisiasa. Alisema kwamba kama ningemjulisha juu ya shughuli za wafungwa wengine, angepanga nipunguziwe miaka ya kifungo changu. Nilipokataa kufanya hivyo, alianza kunitusi. “Umepoteza nafasi ya kuwa huru,” akafoka. “Nitahakikisha kwamba hutarudi nyumbani tena! Utafia hapa.” Hata hivyo, miezi miwili baadaye, nilisamehewa baada ya kuwa gerezani kwa miaka minane na nikarudi nyumbani.

Kipindi Kifupi cha Uhuru

Kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku huko Chekoslovakia tangu Aprili 1949, kwa hiyo punde nikajifunza kwamba kumtumikia Mungu katika ule ulioonekana kama uhuru kulikuwa sawa na kumtumikia nilipokuwa kifungoni. Baada ya kufunguliwa, nilikabili tatizo jingine. Kila mwanamume nchini alilazimishwa kutumikia jeshini kwa miaka miwili.

Wanaume fulani ambao walifanya kazi na makampuni ya Serikali hawakulazimika kutumikia jeshini. Kwa mfano, wale waliofanya kazi kwenye migodi ya makaa ya mawe hawakuhitaji kutumikia jeshini. Kwa kuwa nilikuwa nimefanya kazi hiyo, nilipata kazi katika mgodi mmoja. Nilipokewa kwa uchangamfu sana huko. “Usijali mambo ya jeshi,” nikaambiwa. “Hatuwezi kushindwa kukutoa huko.”

Miezi miwili baadaye, nilipoitwa kujiunga na jeshi, wasimamizi wa migodi walinihakikishia hivi: “Usijali, ni lazima wawe wamekosea. Tutaandikia wakubwa wa jeshi, na mambo yatakuwa sawa.” Lakini mambo hayakuwa sawa. Baada ya muda, afisa mmoja alinijia na kuomba radhi akisema: “Hii ni mara ya kwanza jambo hili kutendeka, lakini itakubidi uripoti jeshini.” Kupatana na msimamo wangu wa kidini kuhusu vita, nilikataa kujiunga na jeshi, nikakamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha kijeshi kilichokuwa karibu.—Isaya 2:4.

Nafikishwa Mahakamani

Baada ya kutiwa gerezani mjini Kladno mnamo Januari 1961, walijaribu kunifanya niwe askari-jeshi. Afisa msimamizi wa jeshi alipanga kuwe na mkutano. Nilipelekwa kwenye chumba cha mazungumzo ambacho kilikuwa na meza kubwa ya mviringo iliyozungukwa na viti vya ngozi vya starehe. Punde maafisa wakaanza kufika na kuketi mezani. Yule mwenye kusimamia alinijulisha kwa kila mmoja wao. Kisha akaketi na kusema: “Sasa, twambie kuhusu dini yako.”

Baada ya kusali kwa haraka, nilianza kuongea mbele ya wasikilizaji waliokuwa makini sana. Mazungumzo yakageuka kuwa juu ya mageuzi, na wakadai kuwa mageuzi yamethibitishwa na wanasayansi. Katika kambi ya kazi ngumu ambapo nilikuwa hapo awali, nilikuwa nimesoma kijitabu Evolution Versus the New World. * Kwa hiyo nikawaonyesha kwamba nadharia ya mageuzi haina uthibitisho, nao wakashangaa sana.

Kisha meja mmoja ambaye alikuwa amelelewa katika dini ya Katoliki akaniuliza, “Unamwonaje Bikira Mariamu? Na maoni yako ni nini kuhusu Misa Takatifu?” Nilijibu maswali yake na kisha nikasema: “Mheshimiwa, naona kwamba wewe ni mtu wa dini, kwa kuwa maswali yako ni tofauti na yale ya wale wengine.”

“La! La! La! Mimi si mtu wa dini!” akapinga kwa sauti kubwa. Katika Serikali ya Kikomunisti, watu waliodai kuwa Wakristo hawakuheshimiwa au kupewa madaraka yoyote. Kwa hiyo, baada ya kusema hivyo, afisa huyo hakushiriki tena katika mazungumzo. Nilifurahi sana kupata fursa ya kueleza wanaume hao imani ya Mashahidi wa Yehova.

Fursa Nyingine za Kuhubiri

Baada ya siku chache, nilipelekwa kwenye jengo la kijeshi huko Prague na kuwekwa chini ya ulinzi mkali wa wanajeshi. Askari jeshi wa kwanza kunilinda ambaye alikuwa na silaha, alishangazwa na ulinzi huo mkali. “Hii ni mara ya kwanza kumlinda mtu mmoja hususa,” akasema. Kwa hiyo nikamweleza kwa nini nimetiwa gerezani. Hiyo ilimfanya atake sana kujua hivi kwamba akaketi chini kusikiliza, bunduki yake ikiwa katikati ya magoti yake. Baada ya muda wa saa mbili, askari jeshi mwingine akaja kuchukua mahali pake, naye pia akataka kujua na tukaendelea na mazungumzo ya Biblia.

Katika siku zilizofuata, nilipata nafasi ya kuongea na wale walionilinda na wafungwa wengine wakati walinzi waliponiruhusu. Hata walinzi walifungua seli na kuwaruhusu wafungwa wakusanyike kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia! Baada ya muda, nilianza kuwa na wasiwasi kwamba uhuru ambao walinzi walikuwa wamenipa ili niongee na wafungwa wengine ungejulikana na hilo lingesababisha matatizo. Lakini siri yetu haikufichuka.

Hatimaye, nilipopelekwa kotini kuhukumiwa, nilitiwa moyo na wale ambao nilikuwa nikiongea nao kuhusu imani yangu. Nilihukumiwa kifungo cha miaka miwili. Miaka hiyo ikaongezwa kwenye miaka sita ya kifungo cha awali ambayo sikumaliza kwa sababu ya msamaha niliopewa. Hiyo ilimaanisha kwamba nilikuwa na kifungo cha miaka minane.

Natambua Msaada wa Mungu

Mara nyingi, nilitambua msaada wa Mungu nilipokuwa nikihamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine na gereza moja hadi jingine huko Chekoslovakia. Nilipofika gerezani huko Valdice, kamanda aliniuliza kwa nini nilikuwa nimefungwa. “Nilikataa kujiunga na jeshi,” nikamjibu. “Imani yangu hairuhusu kujiingiza katika vita.”

“Ingefaa kama kila mtu angekuwa na mtazamo kama huo,” akasema kwa huruma. Lakini baada ya kufikiria kwa muda mfupi, akasema: “Hata hivyo, kwa kuwa watu wengi leo hawana maoni kama hayo, lazima tukuadhibu—tena tukuadhibu vilivyo!”

Nilipelekwa kwenye idara ya kukata kioo, ambayo ilikuwa idara ya adhabu kali. Ijapokuwa nilihukumiwa kwa sababu ya kukataa utumishi wa kijeshi nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, bado nilionwa kuwa mfungwa wa kisiasa, kwa hiyo, nikapewa kazi ngumu. Kukata kioo kwa ajili ya mashada ya taa na vitu vingine vya mapambo kulikuwa kazi ngumu sana kwa sababu vitu hivyo vilipaswa kutengenezwa bila kasoro. Lilikuwa jambo la kawaida kwa wafungwa kupeleka vitu walivyomaliza, kisha kesho yake nusu ya vitu hivyo vingerudishwa ili kufanyiwa marekebisho. Kwa hiyo lilikuwa jambo gumu kutengeneza idadi ya vitu vilivyoagizwa.

Siku niliyoingia kwenye idara ya kukata kioo, nilihitaji kumngojea msimamizi wa idara hiyo kwanza. Alipofika, alianza kuwapigia kelele wafungwa ambao kulingana na maoni yake, hawakuwa wakifanya kazi kwa bidii. Alipita kati yao na kuja kwangu kisha akasema: “Na wewe je? Kwa nini hufanyi kazi?”

Nilimwambia kwamba nilikuwa mpya hapo. Alinipeleka ofisini mwake na kama kawaida aliniuliza kwa nini nilikuwa kifungoni. Baada ya kumweleza hali yangu, alisema: “Kwa hiyo je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?”

Nikamjibu, “Naam.”

Mtazamo wake ukabadilika. “Usijali,” akasema. “Tumekuwa na Mashahidi wa Yehova wengi hapa. Twawaheshimu wote, kwa kuwa ni wafanyakazi wenye bidii na watu wazuri. Nitahakikisha kwamba unapewa kiasi cha kazi utakachoweza kutimiza.”

Badiliko hilo la tabia ya msimamizi huyo lilinishangaza kabisa. Nilimshukuru Yehova na wale waamini wenzangu nisiowajua ambao walifanya Mashahidi wawe na sifa nzuri hivyo katika gereza hilo. Kusema kweli, Yehova alinisaidia kwa upendo muda wote niliokuwa gerezani.

Hata wakati hali yangu ilipokuwa ngumu sana, sikuzote nilihisi kwamba hatimaye ningekutana na ndugu zangu Wakristo. Kisha ningeona tabasamu zao zenye kupendeza na kutiwa moyo. Bila wao ingalikuwa vigumu sana kwangu kuvumilia kifungoni.

Wafungwa wengi walifikiri tu juu ya kulipiza kisasi kwa sababu ya mateso waliyofanyiwa. Lakini sikuhisi hivyo. Nilitambua kwamba nilikuwa nikiteseka kwa sababu ya kutii kanuni adilifu za Mungu. Kwa hiyo nilijua kwamba kwa kila siku niliyokuwa gerezani, Yehova ataweza kunipa siku nyingi nzuri za maisha katika Paradiso yake katika dunia mpya.—Zaburi 37:29; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Nashukuru kwa Baraka Nilizo Nazo Leo

Katika Mei 1968, baada ya miaka 15 kizuizini, nilifunguliwa hatimaye. Mwanzoni, nilikuwa naona ugumu wa kuongea na watu, jambo ambalo ni kawaida kwa wale ambao wamekuwa kifungoni kwa muda mrefu, miongoni mwa walinzi na wafungwa wanaovalia mavazi ya gereza. Lakini upesi ndugu zangu Wakristo walinisaidia kushiriki katika kazi ya kuhubiri ambayo bado ilikuwa ikifanywa chini ya marufuku.

Majuma machache baada ya kufunguliwa, nilikutana na Eva. Ujapokuwa upinzani mkali kutoka kwa familia yake, yeye na kaka yake walikuwa wamechukua msimamo thabiti kwa ajili ya kweli za Biblia miaka mitatu hivi mapema. Punde tukaanza kuhubiri pamoja. Pia tulifanya kazi ya kuchapisha vichapo vyetu vya Biblia. Hiyo ilifanywa kwa siri tukitumia mashine za kuchapia. Kisha Novemba 1969 tukaoana.

Mwaka wa 1970 tukamzaa mtoto wetu wa kwanza, Jana. Baada ya muda, nikaanza kutembelea na kutia moyo kiroho makutaniko kwenye miisho-juma nikiwa mhudumu mwenye kusafiri wa Mashahidi wa Yehova. Nilipokuwa nikifanya kazi hiyo mwaka wa 1975, nilikamatwa na kupelekwa gerezani tena. Lakini safari hii nilikaa huko kwa miezi michache tu. Kisha mwaka wa 1977, mwana wetu Štěpán akazaliwa.

Hatimaye, Septemba 1 1993, Jamhuri ya Cheki ilitambua kihalali Mashahidi wa Yehova. Mwaka uliofuata binti yetu Jana, aliolewa na Dalibor Dražan, mzee Mkristo. Kisha mwaka wa 1999, mwana wetu Štěpán ambaye ni mtumishi wa huduma, akaoa Blanka, ambaye ni mhudumu wa wakati wote. Sisi sote sasa ni washiriki wa makutaniko mbalimbali huku Prague. Sote tunatazamia ulimwengu mpya—lakini mimi natamani sana wakati ambapo hapatakuwa na magereza popote pale.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1950.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nilitumia kichana kuandikia maandiko ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kambi ya Bytiz, ambapo nilifungiwa na baadaye kubatizwa

[Picha katika ukurasa wa 23]

Siku yetu ya harusi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Eva na mimi, tukiwa na Štěpán na Blanka upande wa kushoto na Jana na Dalibor upande wa kulia