Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Njia Bora ya Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

Njia Bora ya Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

Njia Bora ya Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

KWA NINI WATU wanahitaji dini? Watu fulani wanaweza kusema kwamba wanadamu hufuata mambo ya kiroho ili kupata usalama katika ulimwengu huu wenye hatari. Lakini kuna sababu nyingine. Makala moja katika jarida la American Sociological Review ilisema hivi: “Mbali na usalama, kuna mambo mengine yanayowafanya watu wafuate dini. Sikuzote, wanadamu wametafuta majibu kwa maswali kama haya: Uhai ulianzaje? Ni nini kitakachotokea wakati ujao? Ni nini kusudi la uhai?”

Inaelekea unakubali kwamba maswali hayo ni muhimu sana. Kwa hiyo, yanahitaji majibu yenye kutegemeka. Maswali hayo ni muhimu sana na mazito sana hivi kwamba hayawezi kujibiwa kwa kuchagua tu mafundisho yanayotupendeza kutoka kwenye dini mbalimbali. Iwapo tunataka kupata majibu yenye kutegemeka na yenye kuridhisha kuhusu kusudi la uhai, tunahitaji kutumia njia nyingine bora.

Je, kuna njia bora? Ferrar Fenton, mtafsiri wa Biblia, alisema jambo la kupendeza kuihusu. Alisema kwamba Biblia ni ‘njia pekee ya kumsaidia mwanadamu kuelewa ulimwengu, na ya kumsaidia kujielewa mwenyewe.’ Naam, Biblia hujibu maswali kuhusu wakati uliopita, wakati uliopo, na wakati ujao. Inatueleza jinsi uhai ulivyoanza, kusudi la kuwa hai, jinsi tunavyoweza kupata furaha, na yale yatakayotokea wakati ujao. Hakuna kitabu kinginecho chote katika historia ambacho kimekuwa na uwezo kama Biblia, wala hakuna kitabu kinginecho chote ambacho kimeokoka mashambulizi makali sana. Hata hivyo, kwa nini watu wengi sana hupuuza kitabu hicho cha pekee wanapotafuta majibu kwa maswali yao kuhusu uhai?

Watu wengi hawajafikiria kuhusu tofauti kubwa zilizopo kati ya Biblia na dini ambazo wanajua. Wameona jinsi ambavyo watu wanaodai kuwa Wakristo wamechinjana wakitumia jina la Mungu. Kama vile gazeti la The Guardian lilivyosema, wengi wamelalamika kwamba “siku hizi makasisi wanapenda kukusanya pesa badala ya kuwatembelea waumini ili kuwasaidia kiroho.” Huenda watu hao wanafikiri kwamba Biblia hukubali mwenendo huo. Hata hivyo, Biblia inawaagiza Wakristo ‘kupendana,’ nayo inawaambia wahubiri wa neno hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Yohana 13:34; Mathayo 10:8) Basi, je, ni sawa kuishutumu Biblia kwa sababu ya matendo ya watu wanaodai kwamba wanaiheshimu na kumbe wanaipuuza?

Wengi huamini kwamba Biblia haipatani na sayansi, kwamba inajipinga, na kwamba si kitabu cha kisasa. Lakini ukiichunguza kwa makini utaona kwamba maoni hayo si kweli. Ni kweli kwamba Biblia si kitabu cha sayansi. Lakini inapotaja mambo yanayohusiana na sayansi—kama vile mfuatano wa kutokea kwa viumbe duniani, umbo la dunia, au jinsi ya kushughulikia vizuri magonjwa ya kuambukiza—Biblia haisemi jambo lolote lisilo la kweli. Badala yake, ina habari ambazo wanasayansi waligundua karne nyingi baadaye. Na ijapokuwa Biblia ina vitabu 66 vilivyoandikwa kwa kipindi cha miaka 1,600, vyote vinapatana. Isitoshe, Biblia ni kitabu cha kisasa kabisa kwani inaeleza vizuri sana kuhusu tabia za wanadamu.

Kitabu hicho cha kipekee kinasema jambo la maana sana kuhusu kumwabudu Mungu. Kinasema kwamba ibada hiyo yapasa kutolewa kulingana na mapenzi ya Mungu, bali si kama wanadamu wapendavyo. (Yohana 5:30; Yakobo 4:13-15; 2 Petro 1:21) Lakini ni watu wachache tu ambao wamefuata kanuni hiyo. Tangu zamani, wanadamu wameanzisha dini zao ili kutosheleza mapendezi yao. Jambo hilo linaonekana wakati watu wanapochonga miungu yao ya mbao na kuiabudu. Linaonekana wakati dini zinapofundisha mafundisho ya kujitungia. Na hivyo ndivyo watu wanaochagua kuamini mafundisho wanayopenda wanavyofanya.

Hebu fikiria hatua hii nyingine. Mbona usifanye kama vile hakimu mmoja mkuu wa Mahakama Kuu ya Marekani alivyofanya? Sawa na alivyokuwa akisikiliza kesi mahakamani, hakimu huyo alichunguza bila kubagua uthibitisho unaoonyesha kwamba Biblia ni kitabu cha kweli na ule unaopinga jambo hilo. Na uamuzi wake ulikuwa nini? Alisema hivi: “Nimekata kauli kwamba Biblia ni kitabu kinachozidi uwezo wa wanadamu, kwamba ni kitabu cha Mungu.”

Unaweza kufanyaje uchunguzi kama huo? Unaweza kujaribu kujifunza Biblia hatua kwa hatua kwa kuchunguza majibu yake kwa maswali ambayo yaliulizwa mwanzoni mwa makala hii. Mashahidi wa Yehova wapatao milioni sita, katika nchi 235, wamefanya uchunguzi huo. Wao hutumia wakati wao kwa hiari ili kuwaeleza wengine yale ambayo wamejifunza. Funzo la Biblia ambalo wao hutoa bila malipo limewasaidia mamilioni kupata dini ambayo ni thabiti na isiyotegemea mapendezi ya mtu binafsi. Ukristo wa kweli unaotajwa katika Biblia si dini ya kawaida tu. Ukristo huo unahusu kweli kumhusu Mungu na makusudi yake. Basi, mbona usifuate kweli hiyo?—Yohana 17:17.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Njia bora ya kutosheleza mahitaji yako ya kiroho ni kujifunza kumhusu Mungu kupitia Biblia na kushirikiana na waabudu wa kweli