Methali 5:1-23
5 Mwanangu, sikiliza hekima yangu.+ Tega sikio usikie utambuzi wangu,+
2 ili ulinde uwezo wako wa kufikiri;+ na midomo yako mwenyewe ilinde ujuzi.+
3 Kwa maana midomo ya mwanamke mgeni hudondoka-dondoka kama sega la asali,+ nalo kaakaa lake ni laini kuliko mafuta.+
4 Lakini matokeo yake ni machungu kama pakanga;+ ni makali kama upanga wenye makali kuwili.+
5 Miguu yake inashuka kwenye kifo.+ Hatua zake hushika Kaburi.*+
6 Yeye hatafakari njia za uzima.+ Mapito yake yamepotoka wala hajui yanakoelekea.+
7 Basi sasa, enyi wana, nisikilizeni+ wala msiache maneno ya kinywa changu.+
8 Itenge njia yako mbali naye, wala usiukaribie mlango wa nyumba yake,+
9 ili usije ukawapa wengine heshima yako,+ wala kukipa kilicho kikatili miaka yako;+
10 ili wageni wasijishibishe kwa nguvu zako,+ wala vitu vyako ulivyovipata kwa maumivu visiwe ndani ya nyumba ya mgeni,+
11 wala usije kulalamikia wakati wako ujao,+ nyama yako na mwili wako vitakapofikia mwisho.+
12 Nawe utalazimika kusema: “Nimechukia nidhamu+ kama nini nao moyo wangu umedharau karipio+ kama nini!
13 Nami sikusikiliza sauti ya wafundishaji wangu,+ wala sikuwategea sikio langu walimu wangu.+
14 Nimeingia kwa urahisi katika kila namna ya ubaya+ katikati ya kutaniko na kusanyiko.”+
15 Unywe maji ya birika lako mwenyewe, na maji yanayotiririka kutoka katikati ya kisima chako mwenyewe.+
16 Je, chemchemi zako mwenyewe zitawanyike nje,+ na vijito vyako vya maji katika viwanja vya watu wote?
17 Na yawe yako peke yako, wala si ya wageni pamoja nawe.+
18 Chemchemi yako ya maji na ibarikiwe,+ na ushangilie pamoja na mke wa ujana wako,+
19 paa mwenye kupendeka na mbuzi wa milimani mwenye kuvutia.+ Na maziwa yake yakuleweshe nyakati zote.+ Upendo wake na ukufurahishe sikuzote.+
20 Basi mwanangu, kwa nini umfurahie mwanamke mgeni au kukumbatia kifua cha mwanamke wa kigeni?+
21 Kwa maana njia za mwanadamu ziko mbele za macho ya Yehova,+ naye anayatafakari mapito yake yote.+
22 Makosa yake mwenyewe yatamkamata mwovu,+ naye atashikwa katika kamba za dhambi yake mwenyewe.+
23 Atakufa yeye mwenyewe kwa sababu hakuna nidhamu,+ na kwa sababu ya upumbavu wake mwingi yeye hupotea.+
Maelezo ya Chini
^ Sheoli. Tazama Nyongeza 4.

