Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Jibu la Biblia

 Mungu aliwaumba wanadamu na kuruhusu mwanamume na mwanamke wawe na mahusiano ya kingono katika ndoa yao. (Mwanzo 1:​27, 28; Mambo ya Walawi 18:22; Methali 5:​18, 19) Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja na kati ya mwanamume na mwanamke ambao hawajafunga ndoa. (1 Wakorintho 6:​18) Biblia inashutumu pia kumpiga punyeto mtu mwingine na ngono ya kinywa au ulawiti.

 Ingawa Biblia inashutumu matendo ya ushoga, haiwahimizi watu kuwachukia mashoga. Badala yake, Wakristo wanaagizwa “wamheshimu kila mtu.”​—1 Petro 2:​17, Good News Translation.

Je, mtu anaweza kuzaliwa akiwa shoga?

Ingawa Biblia inataja kwamba sote tunazaliwa na mwelekeo wa kuvunja sheria za Mungu, haisemi moja kwa moja jinsi mtu anavyoanza kuwa na tamaa ya kufanya ngono na mtu wa jinsia yake. (Waroma 7:​21-​25) Badala ya kukazia fikira kinachosababisha tamaa hiyo, Biblia inakataza matendo ya kingono kati ya watu wa jinsia moja.

Mtu mwenye tamaa ya kufanya ngono na mtu wa jinsia yake anawezaje kumpendeza Mungu?

Biblia inasema hivi: “Usiongozwe na mwili wako. Ua kila tamaa isiyofaa ya ngono.” (Wakolosai 3:5, Contemporary English Version) Ili kuua tamaa mbaya zinazosababisha matendo yasiyofaa, unahitaji kudhibiti njia yako ya kufikiri. Ikiwa kwa kawaida unajaza akilini mwako mambo yanayofaa, itakuwa rahisi zaidi kuondoa haraka tamaa mbaya. (Wafilipi 4:8; Yakobo 1:​14, 15) Huenda isiwe rahisi mwanzoni lakini baada ya muda utafanikiwa. Mungu anaahidi kukusaidia ‘kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yako.’​—Waefeso 4:​22-​24.

 Mamilioni ya watu wanaotaka kufuata viwango vya Biblia wanapambana na tamaa ya kufanya ngono na mtu wa jinsia tofauti. Watu hao wanatia ndani waseja ambao hawana matumaini ya kufunga ndoa au wale walio na mwenzi wa ndoa mlemavu asiyeweza kutosheleza tamaa yao ya ngono, wanadhibiti tamaa yao ya kutaka kufanya ngono ijapokuwa vishawishi. Wanaishi kwa furaha, na wale wenye tamaa ya kufanya ngono na watu wa jinsia moja wanaweza pia kufanya hivyo ikiwa kwa kweli wanataka kumpendeza Mungu.​—Kumbukumbu la Torati 30:19.