Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Mimi Si Mtumwa wa Jeuri Tena”

“Mimi Si Mtumwa wa Jeuri Tena”
  • Alizaliwa: 1956

  • Nchi: Kanada

  • Historia: Alikata tamaa, upotovu wa kimaadili, na jeuri

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa katika jiji la Calgary huko Alberta, Kanada. Nilipokuwa mtoto mdogo, wazazi wangu walitalikiana, kisha mimi na mama yangu tukahamia nyumbani kwa wazazi wa mama. Walitupenda sana, nami nilikuwa mtoto mwenye furaha sana. Bado ninakumbuka miaka hiyo ya utotoni iliyokuwa na amani.

 Nilipokuwa na umri wa miaka saba, maisha yangu yalibadilika mama alipoamua kuolewa tena na baba kisha tukahamia St. Louis, Missouri, nchini Marekani. Nilitambua upesi kwamba baba yangu alikuwa mkatili sana. Kwa mfano, siku ya kwanza niliporudi nyumbani kutoka shuleni, baba aligundua kwamba watoto fulani walinipiga nami sikujitetea. Alikasirika sana kisha akanipiga kwa nguvu zaidi kuliko nilivyokuwa nimepigwa na watoto hao! Hilo lilikuwa somo kwangu, kwa hiyo nilianza kupigana na watoto wenzangu nilipokuwa na umri wa miaka saba tu.

 Mama yangu alichukizwa na hasira ambayo baba yangu alikuwa nayo, na mara nyingi waligombana sana nyumbani. Nilianza kutumia dawa za kulevya na kunywa pombe nilipokuwa na umri wa miaka 11. Hatua kwa hatua nilizidi kuwa mgomvi na mara nyingi nilipigana na watu mtaani. Kufikia wakati nilipomaliza shule ya sekondari, nilikuwa nimebadilika kabisa na kuwa mjeuri sana.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilijiandikisha kwenye Kikosi cha Jeshi la Wanamaji la Marekani. Ukatili wangu pamoja na mafunzo niliyopata huko yalinifanya kuwa muuaji stadi. Baada ya miaka mitano niliondoka jeshini ili kusomea saikolojia nikiwa na lengo la kufanya kazi katika Shirika la Upelelezi la Marekani. Nilianza masomo yangu ya chuo kikuu nilipokuwa Marekani, kisha niliendeleza masomo hayo baada ya kurudi Kanada.

 Nilipokuwa chuo kikuu, tumaini lolote nililokuwa nalo katika wanadamu na jamii kwa ujumla lilipotea hivi kwamba nikakata tamaa. Niliona kwamba watu walikuwa wabinafsi sana, kila kitu ulimwenguni kilionekana kuwa hakina maana, na ilionekana ni kana kwamba matatizo ya wanadamu hayangeweza kusuluhishwa. Niliona wazi kabisa kwamba wanadamu hawangeweza kuibadili dunia iwe nzuri.

 Kwa sababu nilikosa kusudi maishani, jambo kuu maishani mwangu lilikuwa kufuatilia pesa, kunywa pombe, kutumia dawa za kulevya, na kufanya ngono. Nilichokuwa nikifikiria ni maisha ya anasa tu na ni mwanamke gani ningelala naye. Kwa kuwa nilijiamini kwa sababu ya mafunzo yangu ya kijeshi, mara kwa mara nilipigana na watu. Nilijiamulia mwenyewe jambo ambalo ni haki na ambalo si haki na ningepambana na mtu yeyote ambaye nilifikiri anawaonea wengine. Lakini ukweli ni kwamba nilizidi kuwa mtumwa wa jeuri.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Siku moja, mimi na rafiki yangu, tukiwa tumelewa dawa za kulevya huku tunafunga shehena ya bangi ili ikauzwe kwa magendo, aliniuliza ikiwa ninaamini kama kuna Mungu. Nilimjibu, “Ikiwa Mungu ndiye anayehusika na mateso duniani, basi sitaki kujua chochote kumhusu!” Siku iliyofuata, nilipoenda kazini katika kampuni mpya niliyoajiriwa, mfanyakazi mwenzangu aliyekuwa Shahidi wa Yehova aliniuliza, “Unafikiri Mungu ndiye anayesababisha mateso duniani?” Swali lake lilinishtua sana kwa kuwa siku moja tu iliyotangulia ndiyo nilikuwa nimezungumzia jambo hilo, hivyo alichochea upendezi wangu. Tulikuwa na mazungumzo mengi sana kwa miezi sita iliyofuata, na alinionyesha majibu ya Biblia kwa baadhi ya maswali yangu magumu sana niliyokuwa nayo kuhusu maisha.

 Mchumba wangu, niliyekuwa nikiishi naye kwa wakati huo, hakutaka nimwambie mambo niliyokuwa nikijifunza. Jumapili moja nilimwambia kwamba nimewaalika Mashahidi waje nyumbani kujifunza Biblia pamoja nasi. Siku iliyofuata, niliporudi nyumbani kutoka kazini, nilikuta amechukua kila kitu nyumbani akaondoka na kuniacha. Nilitoka nje na kulia. Pia nilisali kwa Mungu na kumwomba anisaidie. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kusali kwa kutumia jina la kibinafsi la Mungu, Yehova.—Zaburi 83:18.

 Baada ya siku mbili nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi ambao walikuwa wenzi wa ndoa. Walipoondoka niliendelea kusoma kitabu tulichotumia kujifunzia, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, na nikamaliza kukisoma usiku huohuo. a Mambo niliyojifunza kumhusu Yehova Mungu na mwanaye, Yesu Kristo, yalinigusa moyo sana. Niliona kwamba Yehova ni mwenye huruma na kwamba anaumia moyoni tunapoteseka. (Isaya 63:9) Niliguswa moyo zaidi na upendo wa Mungu kunielekea mimi binafsi na dhabihu ambayo Mwana wake alitoa kwa niaba yangu. (1 Yohana 4:10) Nilifikia mkataa kuwa Yehova alinionyesha subira “kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Nilihisi kwamba Yehova alikuwa akinivuta kwake.—Yohana 6:44.

 Nilianza kuhudhuria mikutano ya kutaniko juma hilohilo. Nilikuwa na nywele ndefu, nilivaa hereni na nilikuwa na mwonekano ulioogopesha, lakini Mashahidi walinitendea kama mtu wao wa ukoo aliyekuwa amepotea. Walitenda kama Wakristo wa kweli. Nilijihisi ni kana kwamba nimerudi nyumbani kwa babu na nyanya yangu, lakini katika mazingira bora zaidi.

 Punde, mambo niliyokuwa nikijifunza katika Biblia yalianza kubadili maisha yangu. Nilikata nywele, nikaacha kujihusisha katika upotovu wa maadili kingono, na nikaacha kutumia dawa za kulevya na ulevi. (1 Wakorintho 6:9, 10; 11:14) Nilitaka kumfurahisha Yehova. Kwa hiyo, nilipojifunza kwamba hakubaliani na jambo fulani nililokuwa nikifanya, sikutafuta kisingizio. Badala yake, nilihisi kana kwamba ninachomwa moyoni. Nilijiambia, ‘Siwezi kuendelea kufanya jambo hili.’ Na bila kusita, nilijaribu kubadili mawazo na matendo yangu. Hatimaye, nilianza kuona faida ya kufanya mambo kwa njia ya Yehova. Julai 29, 1989, miezi sita baada ya kuanza kujifunza Biblia, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Biblia imenisaidia kubadili utu wangu. Awali, mara nyingi ikiwa ningechokozwa na mtu mgomvi, ningepigana naye. Lakini sasa ninajitahidi sana ‘kufanya amani na watu wote.’ (Waroma 12:18) Kwa kweli, sijafanikiwa kufanya haya yote kwa nguvu zangu, bali ninamshukuru Yehova kwa sababu ya nguvu za Neno lake na roho yake takatifu.—Wagalatia 5:22, 23; Waebrania 4:12.

 Badala ya kuwa mtumwa wa dawa za kulevya, jeuri, na tamaa potovu, sasa ninajaribu kumpendeza Yehova Mungu na kumpa kilicho bora zaidi. Hilo linatia ndani kuwasaidia wengine wamjue. Miaka michache baada ya kubatizwa, nilihamia sehemu nyingine ya ulimwengu iliyokuwa na uhitaji mkubwa wa waeneza-injili. Kwa miaka mingi nimepata shangwe ya kuwafundisha watu wengi Biblia na kuona jinsi ilivyobadili maisha yao na kuyafanya kuwa bora. Pia, ninafurahi kuwa mama yangu amekuwa Shahidi wa Yehova, hasa kwa sababu ya kuona mabadiliko mazuri katika mtazamo na mwenendo wangu.

 Mwaka 1999, nilihitimu shule ya Biblia ambayo sasa inaitwa, Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, huko El Salvador. Shule hiyo ilinipa mafunzo na maagizo yanayonisaidia kuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri na kuchunga kutaniko. Baadaye, mwaka huohuo, nilimwoa mke wangu mpendwa, Eugenia. Sasa tunatumikia pamoja tukiwa wahubiri wa wakati wote nchini Guatemala.

 Sasa, badala ya kukata tamaa, nina furaha sana maishani. Kutumia mafundisho ya Biblia kumeniweka huru kutokana na upotovu wa maadili na jeuri na kumefanya maisha yangu yawe na upendo wa kweli na amani tele.

a Sasa, Mashahidi wa Yehova hutumia kitabu cha kujifunzia Biblia, Biblia Inatufundisha Nini?