Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 59

Sababu Yampasa Daudi Akimbie

Sababu Yampasa Daudi Akimbie

BAADA ya Daudi kumwua Goliathi, Abneri mkuu wa jeshi anampeleka kwa Sauli. Sauli anapendezwa sana na Daudi. Anamfanya mkuu katika jeshi lake na kumchukua akakae katika nyumba ya mfalme.

Baadaye, jeshi linaporudi kupigana na Wafilisti, wanawake wanaimba hivi: ‘Sauli ameua maelfu, lakini Daudi makumi ya maelfu.’ Hilo lamfanya Sauli aone wivu, kwa sababu Daudi anaheshimiwa kuliko Sauli. Lakini Yonathani mwana wa Sauli haoni wivu. Anampenda Daudi sana, naye Daudi anampenda Yonathani pia. Hao wawili wanapeana ahadi kwamba watakuwa rafiki sikuzote.

Daudi anajua sana kupiga kinubi, naye Sauli anapenda muziki anaopiga Daudi. Lakini siku moja wivu wa Sauli wamfanya atende jambo baya. Wakati Daudi anapopiga kinubi, Sauli anachukua mkuki wake na kuutupa, akisema: ‘Nitampigilia Daudi ukutani!’ Lakini Daudi apiga chenga (aepa), na mkuki wamkosa. Baadaye Sauli akosa tena kumpiga Daudi kwa mkuki wake. Basi Daudi anajua yampasa awe mwangalifu sana.

Unajua ahadi ya Sauli! Alisema angetoa binti yake awe mke wa yule mtu ambaye angeua Goliathi. Mwishowe Sauli anamwambia Daudi achukue Mikali binti yake, lakini kwanza yampasa aue Wafilisti adui 100. Ebu wazia hilo! Sauli anatumaini kwamba Wafilisti watamwua Daudi. Lakini hawamwui, hivyo Sauli anampa Daudi binti yake awe mke wake.

Siku moja Sauli anamwambia Yonathani na watumishi wake wote kwamba anataka kumwua Daudi. Lakini Yonathani anamwambia babaye hivi: ‘Usimwumize Daudi. Hajakukosea. Kila alichofanya kimekuwa msaada mkubwa kwako. Aliweka uhai wake katika hatari alipomwua Goliathi, na ulipoona, ukafurahi.’

Sauli amsikiliza mwanawe, na kuahidi asimwumize Daudi. Daudi anarudishwa, naye anamtumikia Sauli tena nyumbani mwake kama zamani. Lakini, siku moja wakati Daudi anapopiga muziki, Sauli anamtupia Daudi mkuki wake tena. Daudi apiga chenga, mkuki unapiga ukuta. Hii ndiyo mara ya tatu! Sasa Daudi ajua yampasa akimbie!

Usiku huo Daudi aenda nyumbani kwake. Lakini Sauli anatuma watu fulani wakamwue. Mikali anajua mipango ya baba yake. Anamwambia mume wake hivi: ‘Usipoondoka usiku huu, kesho utakuwa umekufa.’ Inampasa Daudi ajifiche hapa na pale muda wa karibu miaka saba, Sauli asimwone.