Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 52

Gideoni na Wanaume Wake 300

Gideoni na Wanaume Wake 300

UNAONA yanayofanyika hapa? Wote hao ni wanajeshi wa Israeli. Wanaume hao wanaoinama wanakunywa maji. Mwamuzi Gideoni ndiye anayesimama karibu yao. Anatazama wanavyokunywa maji.

Ebu watazame sana wanaume hao wanavyokunywa kwa namna tofauti. Wengine wanatia uso wao karibu na maji. Lakini mmoja anachota maji kwa mkono wake, ili aone yanayotendeka karibu yake. Hilo ni la maana, kwa kuwa Yehova alimwambia Gideoni achague wanaume wale tu walio macho wanapokunywa. Wengine, Mungu akasema, warudishwe nyumbani. Ebu tuone sababu.

Tena Waisraeli wanapata taabu nyingi. Wamekataa kumtii Yehova. Wamidiani wamewazidi nguvu na wanawaumiza. Basi Waisraeli hao wanamlilia Yehova awasaidie. Yehova asikia vilio vyao.

Yehova anamwambia Gideoni atayarishe jeshi. Basi Gideoni akusanya wanajeshi 32,000. Lakini wanajeshi wanaopigana na Israeli ni 135,000. Hata hivyo Yehova anamwambia Gideoni hivi: ‘Una wanajeshi wengi mno.’ Kwa nini Yehova alisema hivyo?

Kwa sababu Waisraeli wakishinda, labda watadhani wameshinda kwa uwezo wao. Labda watadhani hawakutaka Yehova awasaidie washinde. Basi Yehova anamwambia Gideoni hivi: ‘Waambie wanaume wote ambao ni waoga warudi nyumbani.’ Gideoni anapofanya hivyo, wanajeshi 22,000 wanarudi nyumbani. Wanabaki wanajeshi 10,000 wa kupigana na askari wote 135,000.

Lakini, sikiliza! Yehova anasema: ‘Bado una wanajeshi wengi mno.’ Basi anamwambia Gideoni awanyweshe maji penye mto huu na kuwarudisha wote wale wanaoinamisha uso wao karibu na maji wanywe. ‘Nitakupa ushindi kwa wanaume hawa 300 ambao wamekuwa macho walipokunywa maji,’ asema Yehova.

Wakati wa vita wafika. Gideoni anagawa wanaume wake 300 kuwa vikundi vitatu. Anampa kila mwanamume tarumbeta, na mtungi ulio na mwenge ndani. Kama usiku wa manane hivi, wote wanaizunguka kambi ya askari maadui. Kisha, wakati ule ule, wote wazipiga tarumbeta zao na kuivunja mitungi yao, wakipiga kelele hivi: ‘Upanga wa Yehova na wa Gideoni!’ Askari maadui wanapoamka, wanatatizwa na kuogopa. Wote wanaanza kukimbia, na Waisraeli wanashinda.