Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 24

Yusufu Anajaribu Ndugu Zake

Yusufu Anajaribu Ndugu Zake

YUSUFU anataka kujua kama ndugu zake 10 bado hawana huruma. Basi anasema hivi: ‘Ninyi ni wapelelezi. Mmekuja kuona udhaifu wa nchi yetu.’

‘Sivyo,’ wanasema. ‘Sisi ni watu wanyofu. Sote ni ndugu. Tuko 12. Lakini ndugu mmoja hayupo, na yule mdogo zaidi yuko nyumbani pamoja na baba yetu.’

Yusufu anajifanya kuwa haamini. Anamweka ndugu anayeitwa Simeoni gerezani, na kuwaachilia wengine wakachukue chakula na kwenda kwao. Lakini anawaambia hivi: ‘Mtakaporudi, lazima mmlete ndugu yenu mdogo zaidi.’

Wanaporudi kwao Kanaani, ndugu hao wanamwambia Yakobo baba yao yote yaliyowapata. Yakobo anahuzunika sana. ‘Yusufu hayupo,’ analia, ‘na sasa Simeoni hayupo. Sitawaruhusu mmchukue mwanangu mdogo zaidi Benyamini.’ Lakini chakula chao kinapoanza kuwa kidogo, Yakobo anawaruhusu wamchukue Benyamini kwenda Misri ili wakanunue chakula zaidi.

Sasa Yusufu anawaona ndugu zake wakija. Anafurahi sana kumwona Benyamini mdogo wake. Lakini hakuna kati yao anayejua kwamba mkuu huyo ni Yusufu. Sasa Yusufu anawajaribu ndugu zake kumi.

Anawaagiza watumishi wake wajaze mifuko yao yote chakula. Lakini bila kuwajulisha, anawaagiza pia watie kikombe chake cha pekee cha fedha katika mfuko wa Benyamini. Wote wakiisha kuondoka na kutmebea mwendo mfupi njiani, Yusufu anawatuma watumishi wake wawafuate. Wanapowakuta, watumishi hao wanasema hivi: ‘Kwa nini mmeiba kikombe cha fedha cha bwana yetu.’

‘Hatukuiba kikombe chake,’ ndugu wote wanajibu. ‘Ukiona kikombe hicho kwa yeyote kati yetu, mtu huyo na auawe.’

Basi watumishi wanachunguza mifuko yote, wanakiona kikombe katika mfuko wa Benyamini, kama unavyoona hapa. Watumishi hao wanasema: ‘Ninyi wengine nendeni, lakini Benyamini atakwenda nasi.’ Sasa ndugu hao 10 watafanya nini?

Wote wanarudi pamoja na Benyamini kwenye nyumba ya Yusufu. Yusufu anawaambia ndugu zake hivi: ‘Nyote nendeni kwenu, lakini Benyamini atakaa huku awe mtumwa wangu.’

Yuda anapaza sauti, hivi: ‘Tukirudi kwetu bila kijana huyu, baba yangu atakufa kwa sababu ampenda sana. Tafadhali, unifanye mimi niwe mtumwa wako huku, lakini mruhusu kijana huyu aende nyumbani.’

Yusufu anajua kwamba ndugu zake wamebadilika. Sasa wana huruma. Na tuchunguze tuone anayofanya Yusufu sasa.