Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 IGENI IMANI YAO

‘Alitangazwa Kuwa Mwadilifu kwa Matendo’

‘Alitangazwa Kuwa Mwadilifu kwa Matendo’

RAHABU alichungulia dirishani huku jua likichomoza kwenye eneo tambarare lililozunguka mji wa Yeriko. Jeshi la wavamizi lilikuwa limekusanyika, yaani, kikosi cha Waisraeli. Jeshi hilo lilipoanza tena kuzunguka jiji, kulikuwa na vumbi hewani na mlio wa pembe ulisikika kotekote.

Rahabu alikuwa mwenyeji wa Yeriko; alijua barabara, masoko, na maduka ya jiji hilo. Aliwafahamu watu wa jiji hilo. Aliona jinsi walivyozidi kuwa na wasiwasi kadiri muda ulivyopita huku Waisraeli wakiendelea na shughuli isiyoeleweka, yaani, kuzunguka jiji mara moja kwa siku. Hata hivyo, mlio wa pembe uliposikika katika jiji la Yeriko, Rahabu hakukata tamaa wala kuwa na wasiwasi kama watu wengine.

Rahabu alitazama jeshi lilipoanza kuzunguka jiji siku ya saba asubuhi. Kati ya askari-jeshi Waisraeli, aliona makuhani wakipuliza pembe na kubeba sanduku takatifu la agano lililowakilisha kuwepo kwa Mungu wao, Yehova. Tunaweza kumwazia Rahabu akiwa ameshika kamba ya uzi mwekundu iliyokuwa ikining’inia kwenye dirisha lake lililokuwa kwenye ukuta mkubwa wa Yeriko. Kamba hiyo ilimkumbusha Rahabu kwamba yeye na familia yake hawangeangamizwa pamoja na jiji hilo. Je, Rahabu alikuwa msaliti? Yehova hakumwona hivyo, alimwona kuwa mwanamke mwenye imani thabiti. Acheni tuchunguze mwanzo wa hadithi ya Rahabu na tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwake.

RAHABU YULE KAHABA

Rahabu alikuwa kahaba. Jambo hilo liliwashangaza sana wafafanuzi fulani wa Biblia hivi kwamba wakadai alifanya kazi katika nyumba ya wageni. Hata hivyo, Biblia inasema mambo waziwazi na haifichi ukweli. (Yoshua 2:1; Waebrania 11:31; Yakobo 2:25) Inawezekana kazi ya Rahabu iliheshimiwa na Wakanaani. Hata hivyo, utamaduni hauwezi kuzuia dhamiri kwa sababu Yehova aliwapa watu wote uwezo huo wa kutambua mema na mabaya. (Waroma 2:14, 15) Huenda Rahabu alitambua kwamba maadili yake yalikuwa mapotovu. Labda, kama wengi leo, alihisi amenaswa, bila njia nyingine ya kutunza familia yake.

Bila shaka, Rahabu alitamani kubadili maisha yake. Nchi yao ilijaa jeuri na uovu, kutia ndani ngono kati ya watu wa ukoo na ngono kati ya wanadamu na wanyama. (Mambo ya Walawi 18:3, 6, 21-24) Uovu huo ulienea sana katika nchi hiyo kwa sababu ya dini. Mahekalu yalijaa ukahaba, na pia ibada ya miungu ya kishetani kama vile Baali na Moleki ilihusisha kuwachoma watoto wakiwa hai katika moto wa dhabihu.

Yehova aliona uovu uliokuwa ukiendelea huko Kanaani. Kwa sababu ya mazoea mengi maovu huko Kanaani, Yehova alisema: “Nchi si safi, nami nitaleta adhabu kwa ajili ya kosa lake juu yake, nayo nchi itawatapika wakaaji wake.” (Mambo ya Walawi 18:25) “Adhabu kwa ajili ya kosa lake” ilihusisha nini? Mungu aliwaahidi hivi Waisraeli: “Yehova Mungu wako atayasukumia mbali mataifa haya toka mbele yako kidogo kidogo.” (Kumbukumbu  la Torati 7:22) Karne nyingi mapema, Yehova alikuwa ameahidi kumpa Abrahamu na familia yake nchi hiyo, na tunajua ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’Tito 1:2; Mwanzo 12:7.

Hata hivyo, Yehova aliamuru jamii fulani katika nchi hiyo ziangamizwe kabisa. (Kumbukumbu la Torati 7:1, 2) Akiwa “Mwamuzi [mwadilifu] wa dunia yote,” alikuwa amechunguza mioyo yao na kuona jinsi walivyokuwa wamepotoka. (Mwanzo 18:25; 1 Mambo ya Nyakati 28:9) Rahabu alihisije kuishi katika jiji hilo? Tunaweza kuwazia jinsi alivyohisi aliposikia habari kuhusu Waisraeli. Alikuwa amesikia kwamba Mungu wa Waisraeli alikuwa amewakomboa watu wake kutoka utumwani huko Misri, ingawa wakati huo nchi ya Misri ilikuwa na jeshi lenye nguvu zaidi ulimwenguni. Sasa Waisraeli walikuwa karibu kushambulia Yeriko. Ingawa hivyo, watu waliendelea na uovu katika jiji hilo. Hilo linaonyesha ni kwa nini Biblia inawaita Wakanaani watu “waliotenda kwa kutotii.”Waebrania 11:31.

Rahabu alikuwa tofauti. Kwa miaka kadhaa, huenda alitafakari habari alizosikia kuhusu Waisraeli na Mungu wao, Yehova. Alikuwa tofauti kabisa na miungu ya Wakanaani! Alikuwa Mungu aliyewapigania watu wake badala ya kuwakandamiza, na ambaye aliwapa waabudu wake mwongozo kuhusu maadili badala ya kuwakosea heshima. Mungu huyo aliwathamini wanawake badala ya kuwaona kama vyombo vya kutosheleza tamaa za ngono vinavyoweza kununuliwa, kuuzwa, na kunajisiwa katika ibada ya ukatili. Rahabu aliposikia kwamba Waisraeli wamepiga kambi ng’ambo ya mto Yordani wakiwa tayari kuvamia, alihuzunika sana alipofikiria uharibifu ambao ungewapata wakaaji wa Yeriko. Je, Yehova alimtambua Rahabu na kuona kilichokuwa moyoni mwake?

Leo, kuna watu wengi walio kama Rahabu. Wanahisi kwamba wamenaswa katika maisha yaliyopotoka kiadili na hivyo hawana shangwe wakifikiri hakuna mtu anayewatambua au kuwathamini. Kisa cha Rahabu kinatukumbusha kwamba Yehova anamwona kila mtu. Hata tukilemewa na hisia, “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Yuko karibu nasi, tayari kabisa kuwapa tumaini wote wanaomwamini. Je, Rahabu alimwamini Mungu?

ALIWAPOKEA WALE WAPELELEZI

Siku moja, kabla ya Waisraeli kuzunguka jiji la Yeriko, wageni wawili walimtembelea Rahabu. Wanaume hao walifikiri hawangetambuliwa na mtu yoyote, lakini watu walikuwa na wasiwasi jijini na hivyo waliwatambua kwa urahisi wapelelezi hao Waisraeli. Huenda Rahabu aliwatambua mara moja. Hakushangaa alipotembelewa na wanaume wageni, lakini alishangaa kujua kwamba wanaume hao walitaka mahali pa kulala bali si huduma zake za ukahaba.

Wanaume hao wawili walikuwa wapelelezi kutoka kwenye kambi ya Waisraeli. Kiongozi wao, Yoshua, alikuwa amewatuma wachunguze uwezo wa kivita wa Wakaaji wa Yeriko. Hilo ndilo jiji la kwanza la Wakanaani ambalo Waisraeli  wangeshambulia na labda lilikuwa na nguvu kuliko majiji mengine yote. Yoshua alitaka kujua uwezo wa watu wa jiji hilo. Huenda wapelelezi waliamua kimakusudi kwenda kwenye nyumba ya Rahabu. Katika nyumba ya kahaba, ingekuwa rahisi kwa wageni kutotambuliwa. Huenda pia wapelelezi walitaka kupata habari muhimu kutokana na mazungumzo ya watu.

Biblia inasema Rahabu ‘aliwakaribisha wale wajumbe.’ (Yakobo 2:25) Aliwapokea ndani ya nyumba yake, na ingawa huenda aliwashuku na hakuwajua, aliwaruhusu wanaume hao wakae kwake. Labda alitaka kujifunza mengi kuhusu Mungu wao, Yehova.

Hata hivyo, ghafula wajumbe wa mfalme wa Yeriko wakawasili! Walikuwa wamepokea habari kwamba wapelelezi Waisraeli walikuwa wameingia ndani ya nyumba ya Rahabu. Rahabu angefanya nini? Kama angewaficha wageni hao wawili, je, hangehatarisha uhai wake pamoja na familia yake? Bila shaka, familia hiyo ingeuawa kwa kuwaficha wapelelezi hao. Kwa upande mwingine, sasa Rahabu alipata uthibitisho kwamba wanaume hao walikuwa Waisraeli. Kama alikuwa amejua kwamba Yehova ni Mungu bora kuliko miungu ya Wakanaani, je, angechagua kumwabudu Yehova?

Ingawa Rahabu hakuwa na muda mwingi wa kufikiria, alikuwa mwenye busara na alitenda haraka. Aliwaficha wapelelezi katikati ya majani ya kitani yaliyokuwa yametandikwa ili yakauke juu ya paa la nyumba yake. Kisha akazungumza na wajumbe wa mfalme, akisema: “Ni kweli, wanaume hao walikuja kwangu, lakini sikujua walikotoka. Ikawa wakati wa kufungwa kwa lango, kulipokuwa na giza, wanaume wale wakatoka. Wala sijui walikokwenda. Wafuatilieni haraka, kwa maana mtawafikia.” (Yoshua 2:4, 5) Wazia Rahabu akitazama nyuso za wajumbe wa mfalme. Je, aliogopa kwamba wangetambua wasiwasi wake?

Rahabu alihatarisha uhai wake kwa kuwaficha watumishi wawili wa Yehova kwenye majani ya kitani

Mbinu yake ilifanikiwa! Wajumbe wa mfalme walitimua mbio kuelekea vivuko vya Yordani. (Yoshua 2:7) Haikosi wasiwasi wa Rahabu ulipungua. Kwa kutumia busara, alikuwa amewapotosha wanaume wauaji ambao hawakuwa na haki ya kujua ukweli, na alikuwa ameokoa watumishi wasio na hatia wa Yehova.

Rahabu akarudi haraka kwenye paa na kuwaambia wale wapelelezi wawili alichokuwa amefanya. Pia, aliwapa ujumbe huu muhimu: Wakaaji wa Yeriko walikuwa wamekata tamaa na waliwaogopa Waisraeli. Bila shaka, wapelelezi walifurahi kusikia jambo hilo. Wakanaani hao waovu waliogopa nguvu za Yehova, Mungu wa Israeli. Kisha Rahabu akafunua jambo lingine muhimu zaidi  kwetu. Alisema hivi: “Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.” (Yoshua 2:11) Habari alizokuwa amesikia kumhusu Yehova zilitosha kumsadikishia jambo hili: Angeweza kumtegemea Mungu wa Israeli. Alimwamini Yehova.

Rahabu hakuwa na shaka kwamba Yehova angewasaidia watu wake kushinda. Hivyo, akaomba ahurumiwe na kusihi asiangamizwe pamoja na familia yake. Wapelelezi wakakubali na kumwambia Rahabu asifunue habari kuwahusu na kwamba aning’inize kamba ya uzi mwekundu dirishani kwenye ukuta wa jiji ili askari-jeshi wasimwangamize pamoja na familia yake.Yoshua 2:12-14, 18.

Tunaweza kujifunza jambo muhimu kuhusu imani kutokana na Rahabu. Biblia husema kwamba “imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Waroma 10:17) Rahabu alikuwa amesikia habari za kuaminika kuhusu nguvu na haki ya Yehova Mungu, hivyo, akamwamini na kumtegemea. Leo, tuna ujuzi mwingi zaidi kumhusu Yehova. Je, tutajitahidi kumjua na kumwamini kwa kutegemea mambo tunayojifunza kumhusu katika Neno lake, Biblia?

JIJI KUBWA LAANGUKA

Wale wapelelezi wawili walifuata ushauri wa Rahabu. Walishuka kwenye ukuta wa jiji wakitumia kamba iliyoning’inizwa dirishani kisha wakaelekea milimani. Kulikuwa na mapango mengi kwenye miteremko iliyokuwa kaskazini mwa Yeriko ambako wapelelezi wangejificha mpaka iwe salama kwao kurudi kwenye kambi ya Waisraeli wakiwa na habari njema walizokuwa wamepata kutoka kwa Rahabu.

Rahabu alimwamini Mungu wa Israeli

Baadaye, wakaaji wa Yeriko walitetemeka kwa woga waliposikia Yehova alikuwa ametenganisha kimuujiza Mto Yordani na kuwawezesha Waisraeli kuvuka kwenye nchi kavu. (Yoshua 3:14-17) Hata hivyo, habari hizo zilimthibitishia Rahabu kwamba alikuwa amefanya uamuzi wa busara wa kumwamini Yehova.

Kisha Waisraeli wakalizunguka jiji la Yeriko kwa siku sita, mara moja kila siku. Siku ya saba ilipofika, mambo yakabadilika. Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii, walianza kuzunguka jua lilipochomoza, na baada ya kuzunguka mara moja, waliendelea kulizunguka jiji la Yeriko tena na tena. (Yoshua 6:15) Kwa nini walifanya hivyo?

Mwishowe, baada ya kulizunguka jiji mara saba, wakasimama. Wakaacha kupuliza pembe. Kimya kikatanda. Watu wakajawa na wasiwasi jijini. Kisha kufuatia agizo la Yoshua, jeshi la Waisraeli likapaaza sauti mara moja, kukawa na mlio wenye kishindo. Je, walinzi waliokuwa juu ya kuta za Yeriko walifikiri kilio hicho kilikuwa mbinu mpya ya kushambulia? Kama walifikiria hivyo, walikuwa wamekosea. Zile kuta kubwa zilianza kutetemeka. Ziliendelea kutetemeka, zikapasuka, kisha zikaanguka na kuporomoka kabisa! Hata hivyo, vumbi lilipotulia, kipande kimoja cha ukuta hakikuwa kimeanguka. Nyumba ya Rahabu ilikuwa imesimama, ulikuwa mnara wa mwanamke mwenye imani. Wazia alivyohisi alipoona jinsi Yehova alivyomkomboa! * Familia yake iliokolewa pia!Yoshua 6:10, 16, 20, 21.

Watu wa Yehova vilevile walimheshimu Rahabu kwa sababu ya imani yake. Walipoona kwamba nyumba moja ilibaki ikiwa imesimama, walijua kwamba Yehova alikuwa amemwokoa mwanamke huyo. Aliokolewa pamoja na familia yake jiji la Yeriko lenye uovu lilipoharibiwa. Baada ya vita hivyo, Rahabu aliruhusiwa kuishi karibu na kambi ya Waisraeli. Baadaye, Rahabu alijiunga na Wayahudi. Aliolewa na mwanamume anayeitwa Salmoni. Mwana wao, Boazi, alikuwa mwanamume mwenye imani thabiti. Alimwoa Ruthu Mmoabu. * (Ruthu 4:13, 22) Hatimaye Mfalme Daudi na pia Masihi, Yesu Kristo, wakawa wazao wa familia hiyo.Yoshua 6:22-25; Mathayo 1:5, 6, 16.

Hadithi ya Rahabu inaonyesha kwamba Yehova anamtambua kila mmoja wetu. Anatuona sote na anafurahi sana anapoona watu wenye imani kama ile ya Rahabu. Imani yake ilimchochea kutenda. Biblia inasema, Rahabu ‘alitangazwa kuwa mwadilifu kwa matendo.’ (Yakobo 2:25) Ni jambo la hekima kwetu kuiga imani yake!

^ fu. 27 Inafurahisha kuona kwamba Yehova aliheshimu makubaliano kati ya Rahabu na wale wapelelezi wawili.

^ fu. 28 Ili ujifunze mengi kumhusu Ruthu na Boazi, soma makala “Igeni Imani Yao” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 1 na Oktoba 1, 2012.