Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU

Uwongo Unaomfanya Mungu Aonekane Kuwa Mkatili

Uwongo Unaomfanya Mungu Aonekane Kuwa Mkatili

MAONI YA WATU WENGI

“Punde tu baada ya kifo nafsi za watu wanaokufa wakiwa watenda dhambi zinaenda motoni, ambako zinateseka milele.” (Catechism of the Catholic Church) Baadhi ya viongozi wa kidini wanasema kwamba mtu akifa anatengwa kabisa na Mungu.

UKWELI WA BIBLIA

“Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Ezekieli 18:4) Wafu “hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Ikiwa nafsi inayokufa haijui lolote inawezaje kuteseka kwenye “moto wa mateso”?

Katika Biblia neno ambalo hutafsiriwa “kuzimu” kihalisi linarejelea kaburi la watu wote. Kwa mfano, Ayubu alipopatwa na ugonjwa mbaya sana, alisali hivi: “Laiti ungenificha kuzimuni.” (Ayubu 14:13, Biblia Habari Njema) Ayubu alitaka kupumzika kaburini na si mahali penye mateso.

KWA NINI NI MUHIMU?

Ikiwa Mungu ni mkatili hatuwezi kumpenda, tutamchukia. “Tangu nikiwa mtoto nilifundishwa kuhusu moto wa mateso,” anasema Rocío, anayeishi Mexico. “Niliogopa sana na kudhani Mungu ni mkatili. Nilifikiri kwamba alikuwa mwenye hasira na asiye na upendo.”

Rocío alibadili maoni yake kumwelekea Mungu aliposoma katika Biblia kuhusu hukumu za Mungu na hali ya wafu. Anasema, “Nilijihisi huru—ni kama nilikuwa nimeondolewa mzigo mkubwa wa kihisia. Nilianza kuamini kwamba Mungu anataka tufanikiwe, anatupenda, na ninaweza kumpenda. Yeye ni kama baba anayewapenda na kuwajali watoto wake.”Isaya 41:13.

Watu wengi wamejitahidi kumcha Mungu kwa sababu wanaogopa kuteswa motoni, hata hivyo, Mungu hataki umtumikie kwa sababu unamwogopa. Badala yake, Yesu alisema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako.” (Marko 12:29, 30) Zaidi ya hayo, tukiwa na uhakika kwamba Mungu anatenda kwa haki sasa, tunaweza kutazamia kwamba atahukumu kwa haki wakati ujao. Kama Elihu, rafiki ya Ayubu, tunaweza kusema: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu, na Mweza-Yote kutenda isivyo haki!”Ayubu 34:10.