Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 WAFUNDISHE WATOTO WAKO

Mungu Anaweza Kuhuzunika—Tunawezaje Kumfurahisha

Mungu Anaweza Kuhuzunika—Tunawezaje Kumfurahisha

Je, umewahi kuumizwa hivi kwamba ukalia? * Labda umewahi. Nyakati nyingine tunaweza kulia kwa sababu ya huzuni. Huenda mtu akasema uwongo kutuhusu. Bila shaka tunaumia, sivyo?— Mungu pia anaumia watu wanaposema uwongo kumhusu. Acheni tuzungumzie jambo hilo na tuone tunavyoweza kumfurahisha badala ya kumuumiza.

Biblia inasema kwamba baadhi ya watu waliosema wanampenda Mungu ‘walimhuzunisha.’ Ndiyo, “walimtia uchungu” Mungu! Bila shaka, hakuna anayeweza kuumiza mwili wa Yehova Mungu. Yeye ni mweza yote. Hivyo basi, acheni tuone kwa nini Yehova anahuzunika tunapokosa kumtii.

Watu wawili wa kwanza walioumbwa na Yehova walimhuzunisha sana. Waliwekwa kwenye Paradiso iliyoitwa “bustani ya Edeni.” Watu hao wawili walikuwa akina nani?— Adamu na Hawa. Acheni tuone jambo walilofanya ambalo lilimhuzunisha Yehova.

Baada ya Yehova kuwaweka katika bustani, aliwaambia waitunze. Pia aliwaambia wangepata watoto na kuishi pamoja bila kufa. Lakini kabla hawajapata watoto, jambo baya lilitokea. Je, unajua ni jambo gani hilo?— Malaika aliwashawishi Adamu na Hawa wamwasi Yehova. Acheni tuone ilivyokuwa.

Malaika alimfanya nyoka aongee. Hawa alipenda alichosikia—nyoka alisema Hawa angekuwa “kama Mungu.” Kwa hiyo alifanya kile alichoambiwa na nyoka. Unajua alifanya nini?

 Hawa alikula matunda ya mti ambao Yehova aliwakataza kula. Kabla Hawa hajaumbwa, Mungu alimwambia Adamu: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.”

Hawa alijua amri hiyo. Hata hivyo, aliendelea kuuangalia na akaona kwamba “mti huo ulikuwa wenye kupendeza kuutazama . . . Kwa hiyo akaanza kuchukua kati ya matunda yake akala. Baadaye akampa [Adamu] naye akaanza kula.” Kwa nini Adamu alifanya hivyo?— Adamu alimpenda Hawa kuliko Yehova. Kwa hiyo, akachagua kumfurahisha Hawa badala ya Mungu. Lakini kumtii Yehova ni muhimu zaidi kuliko kumtii mtu yeyote!

Je, unamkumbuka nyoka aliyeongea na Hawa? Kama vile mtu anavyoweza kufanya mwanasesere aonekane kwamba anazungumza ndivyo mtu fulani alivyofanya nyoka azungumze. Ni nani aliyekuwa akizungumza?— Ni “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.”

Je, unajua jinsi unavyoweza kumfurahisha Yehova?— Ni kwa kumtii sikuzote. Shetani anadai kwamba anaweza kuwashawishi watu wote wamtii yeye. Ndiyo maana Yehova anatuambia: “Uwe na hekima, mwanangu [au binti yangu], na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” Shetani anamdhihaki Yehova. Anasema kwamba anaweza kuwashawishi watu wote waache kumwabudu Yehova. Kwa hiyo, unaweza kumfurahisha Yehova kwa kumtii na kumtumikia. Je, utajitahidi kufanya hivyo?

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo atoe maoni yake.