Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?

Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?

Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?

MAKALA zilizotangulia zimeeleza kwa nini Wakristo wa kweli hawashiriki katika siasa. Hata hivyo, Wakristo wanaweza kuonyeshaje kwamba wanataka kuwasaidia watu katika jamii wawe na maisha bora? Njia moja ni kwa kutii amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”​—Mathayo 28:19, 20.

Kutii amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi’ kunahusiana na kufuata mashauri yake ya kuwa kama chumvi na nuru kwa ulimwengu. (Mathayo 5:13, 14) Mambo hayo yanahusianaje? Na kazi hiyo inaweza kuwasaidiaje watu?

Ujumbe wa Kristo Unaelimisha na Kulinda

Chumvi hutumiwa kuhifadhi vitu visiharibike. Vivyo hivyo, ujumbe ambao Yesu aliwaamuru wafuasi wake wawapelekee watu wa mataifa yote unaweza kuwahifadhi. Watu wanaokubali na kuishi kulingana na mafundisho ya Yesu wanajilinda kutokana na maadili mapotovu ambayo yameenea sana leo. Hilo linawezekanaje? Wanajifunza jinsi ya kuepuka mazoea ambayo yanaweza kuwadhuru kiafya, kwa mfano kuvuta sigara, na wanasitawisha sifa kama vile upendo, amani, ustahimilivu, fadhili, na wema. (Wagalatia 5:22, 23) Sifa kama hizo zinafanya wawe watu wazuri katika jamii. Wakristo wanaoshiriki pamoja na jirani zao ujumbe huo wenye kuhifadhi, wanasaidia sana jamii zao.

Vipi kuhusu mfano wa nuru? Kama vile tu mwezi unavyoangaza nuru kutoka kwenye jua, ndivyo wafuasi wa Kristo wanavyoangaza “nuru” kutoka kwa Yehova Mungu. Wanaangaza nuru hiyo kupitia ujumbe wenye kuelimisha wanaohubiri na pia kupitia matendo yao mazuri.​—1 Petro 2:12.

Zaidi ya hayo, Yesu alieleza uhusiano uliopo kati ya kuwa nuru na kuwa mwanafunzi aliposema: “Watu huwasha taa na kuiweka, si chini ya kikapu cha kupimia, bali juu ya kinara cha taa, nayo huangazia watu wote waliomo ndani ya nyumba. Vivyo hivyo acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu.” Taa inayong’aa ambayo imewekwa juu ya kinara inaonekana na watu wote wanaoizunguka. Vilevile, kazi ya kuhubiri na matendo mengine mazuri ambayo Wakristo wa kweli wanatenda yanapaswa kuonekana waziwazi na watu wanaowazunguka. Kwa nini? Yesu alisema kwamba wale wanaoona matendo hayo mazuri watamtukuza Mungu bali si Wakristo.​—Mathayo 5:14-16.

Daraka la Wakristo Wote

Yesu aliposema, “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu” na “acheni nuru yenu iangaze,” alikuwa akiwaagiza wanafunzi wake wote. Amri ambayo Yesu alitoa haiwezi kutimizwa na watu wachache waliotawanyika katika dini mbalimbali. Badala yake, waamini wote ni “nuru.” Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi ambao wanaishi katika nchi zaidi ya 235, wanaamini kwamba wana jukumu la kuwatembelea jirani zao na kuwaeleza kuhusu ujumbe ambao Kristo anataka wafuasi wake watangaze.

Kichwa kikuu cha ujumbe wa Mashahidi wa Yehova ni nini? Yesu alipotoa amri ya kuhubiri, hakuwaagiza wafuasi wake wahubiri kuhusu mabadiliko ya kijamii au kisiasa, muungano wa Kanisa na Serikali, au sera nyingine za wanadamu. Badala yake, alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hivyo, Wakristo wa kweli leo wanatii maagizo ya Yesu kwa kuendelea kuongea na jirani zao kuhusu Ufalme wa Mungu ambao ni serikali pekee iliyo na uwezo wa kukomesha mfumo mwovu wa Shetani na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu.

Unaposoma masimulizi ya Injili, utaona mambo mawili makuu kuhusu huduma ya Yesu ambayo yanaongoza matendo ya Wakristo wa kweli leo. Mambo hayo mawili yanazungumziwa katika makala inayofuata.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Kwa nini ujumbe wa Kikristo ni kama chumvi?

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Kwa nini ujumbe wa Kristo ni kama nuru inayoangaza gizani?