Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

The Biblia Inabadili Maisha

The Biblia Inabadili Maisha

KWA nini mtu aliyekuwa na wake wengi na ambaye aliwapinga Mashahidi wa Yehova aliamua kuwa Shahidi? Nini kilichomchochea kasisi wa Kanisa la Pentekoste abadili imani yake? Ni nini kilichomsaidia mwanamke fulani aliyepatwa na msiba utotoni kushinda hali ya kujichukia na kisha kumkaribia Mungu? Kwa nini mtu aliyependa muziki wenye mdundo mzito alibadilika na kuwa mhudumu wa dini? Soma masimulizi haya ili upate majibu.

“Nimekuwa Mume Bora.”​—RIGOBERT HOUETO

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1941

  • NCHI: BENIN

  • HISTORIA: ALIKUWA NA WAKE WENGI NA ALIPINGA MASHAHIDI WA YEHOVA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa Cotonou, jiji kubwa nchini Benin. Nililelewa katika dini ya Katoliki lakini sikwenda kanisani kwa ukawaida. Katika eneo ambako niliishi, Wakatoliki wengi walikuwa na wake wengi, kwa sababu wakati huo ilikubalika kisheria kuoa wake wengi. Hatimaye, nilikuwa na wake wanne.

Mapinduzi yalipotokea katika miaka ya 1970, nilifikiri yataisaidia nchi yangu. Hivyo, niliyaunga mkono kwa moyo wote na nikajiingiza katika siasa. Wanamapinduzi hawakuwapenda Mashahidi wa Yehova kwa sababu hawakuunga mkono mambo ya kisiasa. Nilikuwa kati ya wale waliowatesa Mashahidi. Wakati wamishonari Mashahidi walipofukuzwa nchini Benin mwaka wa 1976, nilikuwa na hakika kwamba hawangerudi tena.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mapinduzi yaliisha mwaka wa 1990. Muda mfupi baadaye, wamishonari Mashahidi waliingia, jambo lililonishangaza sana. Nilianza kuwaza kwamba huenda Mungu alikuwa pamoja na watu hao. Wakati huo, nilipata kazi nyingine. Mmoja wa wafanyakazi wenzangu alikuwa Shahidi, na mara moja akaanza kunihubiria. Alinionyesha maandiko katika Biblia yanayoonyesha kuwa Yehova ni Mungu mwenye upendo na haki. (Kumbukumbu la Torati 32:4; 1 Yohana 4:8) Sifa hizo zilinivutia sana. Nilitaka kujifunza mengi kumhusu Yehova, hivyo, nikakubali kujifunza Biblia.

Muda mfupi baadaye nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na upendo wa kweli nilioona—hakukuwa na ubaguzi wa kikabila wala wa kijamii. Kadiri nilivyoendelea kushirikiana na Mashahidi, ndivyo ilivyokuwa wazi hata zaidi kwamba hao ndio wafuasi wa kweli wa Yesu.—Yohana 13:35.

Niliamua kwamba ikiwa ninataka kumtumikia Yehova ninapaswa kuacha Kanisa Katoliki. Hiyo haikuwa hatua rahisi, kwa sababu niliogopa kile ambacho wengine wangefikiria. Baada ya muda mrefu na kwa msaada wa Yehova, nilipata ujasiri na kuacha kanisa hilo.

Hata hivyo, bado kulikuwa na badiliko lingine kubwa nililohitaji kufanya. Kupitia funzo langu la Biblia, nilijifunza kwamba Mungu haungi mkono ndoa ya wake wengi. (Mwanzo 2:18-24; Mathayo 19:4-6) Machoni pake, ndoa yangu ya kwanza ndiyo iliyokuwa halali. Hivyo, niliiandikisha ndoa hiyo ya kwanza kisheria na kuwaacha wale wanawake wengine, na kupanga jinsi ambavyo mahitaji yao ya kimwili yangetimizwa. Baada ya muda, wake zangu wawili wa zamani wakawa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Ingawa mke wangu bado ni Mkatoliki, anaheshimu uamuzi wangu wa kumtumikia Yehova. Sote tunahisi kwamba nimekuwa mume bora.

Nilifikiri kwamba ningeweza kuboresha maisha ya jamii yangu kupitia siasa, lakini jitihada hizo hazikufanikiwa. Sasa ninatambua kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee kwa matatizo ya mwanadamu. (Mathayo 6:9, 10) Ninamshukuru Yehova kwa kunionyesha jinsi ya kuishi maisha yenye furaha kikweli.

“Haikuwa Rahisi Kufanya Mabadiliko Yaliyohitajiwa.”​—ALEX LEMOS SILVA

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1977

  • NCHI: BRAZILI

  • HISTORIA: KASISI WA KANISA LA PENTEKOSTE

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa kwenye kitongoji kimoja nje ya jiji la Itu, katika jimbo la São Paulo. Sehemu hiyo ilijulikana sana kwa kiwango cha juu cha uhalifu.

Nilikuwa mjeuri sana na mpotovu wa maadili. Zaidi ya hayo, nilijihusisha na ulanguzi wa dawa za kulevya. Baada ya muda, niligundua kwamba maisha hayo yangenifanya nifungwe jela au niuawe; hivyo nikayaacha. Kisha, nikajiunga na Kanisa la Pentekoste, na baadaye nikawa kasisi.

Nilihisi kwamba ningeweza kuwasaidia watu kupitia huduma yangu kanisani. Hata nilitangaza vipindi vya dini kupitia redio ya jamii na hivyo nikajulikana sana katika eneo hilo. Hata hivyo, baada ya muda niliona kwamba kwa ujumla kanisa halikujali hali ya waumini wake—hata halikumheshimu Mungu. Nilitambua kwamba kanisa hilo lilikuwa na lengo moja tu, yaani, kukusanya pesa. Hivyo, nikaamua kuliacha.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilitambua mara moja kwamba wao ni tofauti na dini nyingine. Mambo mawili yalinivutia sana. Kwanza, Mashahidi wa Yehova hawazungumzi tu kuhusu kumpenda Mungu na jirani; wanaonyesha hivyo kwa matendo. Pili, hawajiingizi katika mambo ya kisiasa au vita. (Isaya 2:4) Mambo hayo mawili yalinisadikisha kwamba nimeipata dini ya kweli—barabara nyembamba inayoongoza kwenye uzima.—Mathayo 7:13, 14.

Nilitambua kwamba ikiwa nilitaka kumpendeza Mungu, nilipaswa kufanya mabadiliko makubwa. Nilihitaji kushughulikia mahitaji ya familia yangu hata zaidi. Pia, nilihitaji kuwa mnyenyekevu zaidi. Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa, lakini kwa msaada wa Yehova nilifanikiwa. Mke wangu alifurahia sana mabadiliko hayo. Alikuwa ameanza kujifunza Biblia kabla yangu, lakini sasa akajifunza Biblia haraka zaidi. Muda si muda, sote tulitambua kwamba tulitaka kuwa Mashahidi wa Yehova. Tulibatizwa siku moja.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Mimi na mke wangu tunafurahi kuwasaidia watoto wetu watatu kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova. Familia yetu ina furaha. Ninamshukuru Yehova kwa kunisaidia kuijua kweli inayopatikana katika Neno lake, Biblia. Kwa kweli Biblia inabadili maisha ya watu! Mimi ni uthibitisho wa jambo hilo.

“Ninajihisi Nikiwa Safi, Mzima, na Ninafurahia Kuwa Hai.”​—VICTORIA TONG

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1957

  • NCHI: AUSTRALIA

  • HISTORIA: ALIPATWA NA MSIBA UTOTONI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa katika jiji la Newcastle, huko New South Wales. Mimi ni mtoto wa kwanza kati ya watoto saba. Baba yetu alikuwa mlevi kupindukia na mjeuri. Mama alikuwa mjeuri pia na alinipiga na kunitukana. Aliniambia tena na tena kwamba nilikuwa mbaya na kwamba nitateswa katika moto wa mateso. Vitisho hivyo viliniogopesha sana.

Mara nyingi majeraha ambayo nilipata kwa kupigwa na mama yangu yalinifanya nikose kwenda shuleni. Nilipokuwa na umri wa miaka 11, wenye mamlaka walinichukua kutoka kwa wazazi wangu na kunipeleka kwanza katika taasisi ya serikali na baadaye kwenye makao ya watawa. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilitoroka katika makao hayo. Sikutaka kwenda nyumbani, hivyo, niliishi kwenye barabara za Kings Cross, kitongoji kimoja cha jiji la Sydney.

Nilipokuwa nikiishi mitaani, nilijihusisha na dawa za kulevya, pombe, ponografia (picha au habari za ngono), na ukahaba. Jambo fulani lilitukia na kuniogopesha sana. Nilikuwa nikiishi kwenye ghorofa la mmiliki wa klabu moja ya usiku. Usiku mmoja, wanaume wawili walikuja kumwona. Aliniambia niende katika chumba cha kulala, lakini niliweza kusikia mazungumzo yao. Mmiliki huyo wa klabu alikuwa akifanya mipango ya kuniuza kwa wanaume hao. Walikuwa waniingize kwenye meli ya mizigo na kunisafirisha hadi Japani ili nikafanye kazi katika baa. Nilishtuka, nikaruka kutoka barazani na kukimbia ili nipate msaada.

Nilikutana na mwanamume fulani aliyekuja Sydney kutalii na nikamweleza hali yangu nikitarajia kwamba angenipa pesa. Badala yake, alinikaribisha mahali alipokuwa akiishi ili nioge na kula chakula. Niliendelea kukaa naye na mwaka mmoja baadaye, tukaoana.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilikumbwa na hisia mbalimbali. Nilikasirika sana nilipojifunza kwamba Shetani ndiye chanzo cha uovu; siku zote nilikuwa nimefundishwa kwamba Mungu ndiye anayefanya tuteseke. Nilifurahi sana nilipojifunza kwamba Mungu hawaadhibu watu katika moto wa mateso, fundisho ambalo lilikuwa limeniogopesha kwa miaka mingi sana.

Nilivutiwa na jinsi Mashahidi wanavyofanya maamuzi yao kwa kutegemea Biblia. Wao wanaishi kulingana na imani yao. Haikuwa rahisi kushughulika nami, lakini hata kama ningesema au kufanya jambo gani, bado Mashahidi walinitendea kwa upendo na heshima.

Tatizo langu kubwa limekuwa kukabiliana na hali ya kujihisi kwamba sifai. Nilijichukia sana, na niliendelea kuhisi hivyo kwa muda mrefu hata baada ya kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Nilijua kwamba ninampenda Yehova, lakini nilikuwa na hakika kwamba hawezi kumpenda mtu kama mimi.

Mawazo yangu yalibadilika kabisa miaka 15 baada ya ubatizo wangu. Ndugu fulani aliyekuwa akitoa hotuba katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, alisoma andiko la Yakobo 1:23, 24. Mistari hiyo inalilinganisha Neno la Mungu na kioo ambacho tunaweza kujiangalia na kuona jinsi Yehova anavyotuona. Nilianza kujiuliza ikiwa jinsi nilivyojiona ni tofauti na jinsi Yehova alivyoniona. Mara ya kwanza, nilipinga maoni hayo mapya. Bado nilihisi kwamba sikupaswa kabisa kumtarajia Yehova anipende.

Siku chache baadaye, nilisoma andiko lililobadili maisha yangu. Andiko hilo ni Isaya 1:18, ambapo Yehova ananukuliwa akisema: “Sasa, njooni, nasi tunyooshe mambo kati yetu. . . . Hata dhambi zenu zikiwa nyekundu, zitafanywa kuwa nyeupe kama theluji.” Nilihisi kana kwamba Yehova alikuwa akiniambia: “Njoo, Vicky tunyooshe mambo kati yetu. Ninakujua, ninajua dhambi zako, ninaujua moyo wako, na ninakupenda.”

Sikuweza kulala usiku huo. Bado nilikuwa na shaka ikiwa Yehova anaweza kunipenda, lakini nilianza kufikiria fidia, au dhabihu ya ukombozi, ya Yesu. Mara moja nikakumbuka kwamba Yehova amekuwa akinivumilia kwa muda mrefu na kunionyesha kwa njia nyingi sana kwamba ananipenda. Hata hivyo, ni kana kwamba nilikuwa nikimwambia: “Hunipendi vya kutosha. Dhabihu ya mwana wako haiwezi kufunika dhambi zangu.” Ni kana kwamba nilikuwa ninaikataa dhabihu ambayo Yehova ametoa. Lakini sasa, baada ya kutafakari kuhusu zawadi hiyo ya dhabihu, nilianza kuhisi kwamba Yehova ananipenda.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Ninajihisi nikiwa safi, mzima, na ninafurahia kuwa hai. Ndoa yangu imekuwa bora, na ninafurahi kwamba ninaweza kutumia mambo yaliyonipata kuwasaidia wengine. Ninajihisi kuwa niko karibu zaidi na Yehova.

“Jambo Hilo Lilikuwa Ni Jibu kwa Sala Yangu.”​—SERGEY BOTANKIN

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1974

  • NCHI: URUSI

  • HISTORIA: ALIPENDA MUZIKI WENYE MDUNDO MZITO

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa mjini Votkinsk, ambapo Pyotr Ilich Tchaikovsky, mtunzi maarufu wa muziki, alizaliwa pia. Familia yetu ilikuwa maskini. Baba yangu alikuwa na sifa nyingi nzuri, hata hivyo, alikuwa mlevi kupindukia, hivyo, mara nyingi tuliishi kwa wasiwasi.

Sikufanya vizuri shuleni, hivyo, kadiri miaka ilivyopita, nilihisi kwamba sifai. Nilijitenga na watu wengine na sikuwaamini. Sikufurahia kwenda shuleni. Kwa mfano, nilipohitajika kutoa ripoti fulani mbele ya darasa, mara nyingi nilishindwa kueleza hata mambo ya kawaida ambayo nyakati nyingine ningeweza kueleza. Nilipohitimu darasa la nane, kadi yangu ya ripoti ilisema: “Hajui maneno mengi na hawezi kujieleza vizuri.” Maneno hayo yalinivunja moyo sana na kunifanya nijihisi sifai hata zaidi. Nilianza kujiuliza ikiwa maisha yangu yana kusudi.

Nilipokuwa kijana, nilianza kunywa pombe. Mwanzoni, pombe ilinifanya nijisikie vizuri. Lakini nilipokunywa kupita kiasi dhamiri yangu ilinisumbua. Maisha yangu yalionekana kama hayana maana. Nilianza kushuka moyo hata zaidi na nyakati nyingine sikutoka ndani ya nyumba. Nilianza kufikiria kujiua.

Nilipofikia umri wa miaka 20, nilipata kitulizo kipya cha muda mfupi. Nilivutiwa na muziki wenye mdundo mzito. Kusikiliza muziki huo kulinitia nguvu na nikaanza kutafuta watu wengine waliousikiliza. Niliacha nywele zangu zikawa ndefu, nikatoboa masikio, na kuvaa kama wanamuziki niliowapenda. Hatua kwa hatua, nikawa mzembe na mjeuri, na kubishana na watu wa familia yetu mara kwa mara.

Nilifikiri kwamba kusikiliza muziki wenye mdundo mzito kungenifurahisha, hata hivyo, mambo yalikuwa kinyume cha hilo. Nilianza kubadilika na kuwa mtu tofauti! Na nilipojua mambo fulani mabaya kuhusu wanamuziki niliowapenda, nilihisi kuwa nimesalitiwa.

Kwa mara nyingine tena, nilianza kufikiria kwa uzito kujiua. Nilifikiria jinsi ambavyo mama yangu angeathiriwa na uamuzi huo na jambo hilo likanizuia nisijiue. Alinipenda sana na alikuwa amenifanyia mengi. Hali hiyo ilikuwa ngumu sana. Sikutaka kuendelea kuishi, lakini singeweza kujiua.

Ili kuepukana na mawazo hayo, nilianza kusoma vitabu vya hadithi za kale za Kirusi. Hadithi moja ilihusu mtu fulani aliyekuwa shujaa ambaye alitumika kanisani. Papo hapo nikaanza kutamani kumtumikia Mungu na kuwasaidia watu wengine. Nilimweleza Mungu yote yaliyokuwa moyoni mwangu kupitia sala, jambo ambalo sikuwa nimewahi kufanya maishani mwangu. Nilimwomba Mungu anionyeshe jinsi ninavyoweza kuishi maisha yenye kusudi. Nilipokuwa nikisali, nilihisi nimetulia sana na jambo lililofuata ndilo lenye kushangaza hata zaidi. Muda wa saa mbili tu baadaye, Shahidi mmoja wa Yehova alibisha mlango wangu na kuniomba nijifunze Biblia naye. Ninaamini kwamba jambo hilo lilikuwa ni jibu kwa sala yangu. Huo ulikuwa mwanzo wa maisha mapya, yenye furaha.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Ingawa ilikuwa vigumu sana, nilitupa vitu vyote vilivyohusiana na muziki wenye mdundo mzito. Hata hivyo, muziki huo ulibaki akilini mwangu kwa muda mrefu sana. Kila nilipopita mahali ambapo muziki huo ulipigwa, mara moja nilianza kukumbuka maisha yangu ya zamani. Sikutaka kuchanganya kumbukumbu hizo mbaya na mambo mazuri ambayo nilikuwa nimeanza kuingiza katika akili na moyo wangu. Hivyo, nilianza kuepuka sehemu hizo. Na kila nilipoanza kufikiria maisha yangu ya zamani, nilisali kwa bidii. Kufanya hivyo kulinisaidia kupata “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”—Wafilipi 4:7.

Nilipojifunza Biblia, nilielewa kwamba Wakristo wana jukumu la kuwaeleza wengine kuhusu imani yao. (Mathayo 28:19, 20) Kwa kweli, niliamini kuwa nisingeweza kufanya hivyo. Wakati huohuo, mambo mapya niliyokuwa nikijifunza yaliniletea shangwe kubwa na amani ya akili. Nilijua kwamba watu wengine wangehitaji kujifunza mambo hayo pia. Ingawa nilikuwa na woga, nilianza kuwaeleza wengine kuhusu mambo niliyokuwa nikijifunza. Kwa kushangaza, kuwaeleza wengine kuhusu Biblia kulinipa ujasiri zaidi. Pia, imani yangu iliimarika hata zaidi.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Sasa nimeoa na ndoa yetu ni yenye furaha. Pia, nimepata shangwe ya kuwasaidia watu kadhaa kutia ndani dada na mama yangu kujifunza Biblia. Kumtumikia Mungu na kuwasaidia wengine wamjue kumefanya maisha yangu yawe na kusudi halisi.