Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Maisha Yanaonekana Kama Hayana Maana Yoyote?

Kwa Nini Maisha Yanaonekana Kama Hayana Maana Yoyote?

Kwa Nini Maisha Yanaonekana Kama Hayana Maana Yoyote?

KWA nini uamini kwamba sikuzote maisha hayatakuwa tu “mafupi yasiyo na faida” ambayo “hupita kama kivuli,” kama Mfalme Sulemani anavyoeleza? (Mhubiri 6:12, Biblia Habari Njema) Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake, ambayo ni chanzo cha habari kinachotegemeka, inaahidi kuwa wakati ujao maisha yatakuwa na maana kwelikweli.—2 Timotheo 3:16, 17.

Biblia inatueleza Mungu alikuwa na kusudi gani mwanzoni alipoiumba dunia. Pia inaeleza kwa nini dunia imejaa ukosefu wa haki, ukandamizaji, na kuteseka. Kwa nini ni muhimu tuelewe mambo hayo? Kwa sababu jambo kuu linalowafanya watu wafikiri kuwa maisha hayana maana yoyote ni kwamba hawajui—au wanaamua kupuuza—kusudi la Mungu kuelekea dunia na wanadamu wanaoishi juu yake.

Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?

Yehova Mungu * aliiumba dunia ikiwa paradiso kamilifu—mahali ambapo wanaume na wanawake wangefurahia milele maisha kamili wakiwa wanadamu wakamilifu. Ukweli huo muhimu unapingana kabisa na wazo linalokubaliwa na wengi lakini lisilopatana na Maandiko kwamba Mungu aliiumba dunia iwe mahali ambapo angewajaribu wanadamu ili kuona kama wanastahili kuishi maisha yenye maana zaidi katika ulimwengu wa roho.—Ona sanduku  “Je, Ni Lazima Tuondoke Duniani Ili Kufurahia Maisha Yenye Maana?” katika ukurasa wa 6.

Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke kwa mfano wake, na kuwapa uwezo wa kuiga sifa zake nzuri. (Mwanzo 1:26, 27) Aliwaumba wakiwa wakamilifu. Walikuwa na kila kitu walichohitaji ili kufurahia maisha mazuri na yenye maana milele. Hilo lingetia ndani kuijaza dunia, kuitiisha, na kuibadilisha yote kuwa paradiso kama tu bustani ya Edeni.—Mwanzo 1:28-31; 2:8, 9.

Ni Nini Kilichotokea?

Bila shaka, kuna tatizo lililotokea. Wanadamu kwa ujumla hawaigi sifa nzuri za Mungu. Nayo dunia si paradiso. Basi, ni nini kilichotokea? Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walitumia vibaya uhuru wao wa kuchagua. Walitaka kuwa “kama Mungu,” wakijiamulia “mema na mabaya.” Kwa kufanya hivyo waliiga uasi wa Shetani Ibilisi.—Mwanzo 3:1-6.

Hivyo basi, uovu si hali isiyoeleweka, iliyopangwa mapema na Mungu. Uovu ulianza wakati Shetani na baadaye Adamu na Hawa, walipoasi utawala wa Mungu. Matokeo ya uasi huo yalifanya wazazi wetu wa kwanza wapoteze Paradiso na ukamilifu, wakajiletea dhambi na kifo wao wenyewe, na pia wazao wao, yaani, wanadamu wote. (Mwanzo 3:17-19; Waroma 5:12) Uasi huo ndio uliosababisha hali zinazofanya maisha yaonekane kuwa bila maana yoyote.

Kwa Nini Mungu Hakuondoa Uovu Mara Moja?

Watu fulani hujiuliza, ‘Kwa nini Mungu hakuondoa uovu mara moja kwa kumharibu Shetani na waasi wengine kisha kuanzisha maisha upya?’ Je, hilo lingekuwa jambo la busara? Ungehisi jinsi gani ikiwa ungesikia kwamba kuna serikali fulani yenye nguvu ambayo humuua mara moja mtu yeyote anayeipinga? Bila shaka, jambo kama hilo lingewafanya watu walio na usawaziko wajitenge na serikali hiyo. Pia, haingekuwa ikiwawekea raia wake mfano unaofaa kuhusu viwango vya mema na mabaya.

Mungu aliamua kutowaondoa waasi hao mara moja. Kwa busara, aliruhusu wakati upite ili masuala ambayo yalizushwa katika Edeni kuhusu njia yake ya kutawala, yatatuliwe milele.

Uovu Wote Utaondolewa

Jambo muhimu la kukumbuka ni: Mungu ameruhusu uovu uendelee kwa muda fulani tu. Amefanya hivyo akijua kuwa ana uwezo wa kuondoa matokeo mabaya ya uovu huo. Atafanya hivyo wakati ambapo masuala yaliyozushwa na uasi dhidi ya utawala wake yatakapotatuliwa.

Kusudi la Mungu kuelekea dunia na wanadamu halijabadilika. Kupitia nabii Isaya, Yehova anatuhakikishia kuwa Yeye ndiye Mtengenezaji wa dunia, “ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Hivi karibuni, atairudisha dunia katika hali kamilifu aliyokusudia mwanzoni. Baada ya kuthibitisha kuwa njia yake ya kutawala ndiyo ya haki, atakuwa na sababu ya kutumia nguvu zake zisizo na kipimo kutimiza mapenzi yake na kuuondoa uovu wote. (Isaya 55:10, 11) Katika sala ya mfano, Yesu Kristo alimwomba Mungu achukue hatua hiyo. Yesu alitufundisha tusali hivi: “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Hayo yanatia ndani nini?

Mapenzi ya Mungu Kuelekea Dunia

Kati ya baraka nyingine nyingi, “wapole wataimiliki dunia.” (Zaburi 37:9-11, 29; Methali 2:21, 22) Yesu Kristo “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka.” Atawakomboa kutoka katika “ukandamizaji na katika jeuri.” (Zaburi 72:12-14) Hakutakuwa na vita tena; wala kifo, machozi, maumivu, au kuteseka. (Zaburi 46:9; Ufunuo 21:1-4) Maelfu ya watu ambao wamekufa wakati huu ambapo Mungu ameruhusu uovu uwepo, watafufuliwa waishi hapa duniani, na watakuwa na nafasi ya kufaidika na baraka hizo na nyinginezo.—Yohana 5:28, 29.

Kwa kweli, Yehova ataondoa madhara yoyote ambayo yamesababishwa na uasi wa Shetani. Yehova atayaondoa kabisa hivi kwamba “taabu za zamani [mambo yote yanayosababisha majonzi na maumivu] kwa kweli zitasahauliwa.” (Isaya 65:16-19) Hatuna shaka yoyote kuhusu wakati huo ujao. Mungu hasemi uwongo. Ahadi zake zote zinatimia. Maisha hayatakuwa tena “ubatili na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 2:17) Badala yake yatakuwa na maana tele.

Lakini namna gani wakati huu? Je, kujua yale ambayo Biblia inafundisha na kuelewa kusudi la Mungu kuelekea dunia kunaweza kufanya maisha yako yawe na maana zaidi? Makala ya mwisho katika mfululizo huu inazungumzia swali hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Katika Biblia, jina la kibinafsi la Mungu ni Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

 Je, Ni Lazima Tuondoke Duniani ili Kufurahia Maisha Yenye Maana?

Kwa miaka mingi, watu wasiojua kusudi la Mungu kuelekea dunia, wamefundisha kwamba ni lazima tuondoke duniani ili tuweze kufurahia maisha yenye maana.

Wengine wamesema kwamba nafsi, ambazo haziwezi kufa, “zilifurahia maisha bora kabla ya kuingia ndani ya miili ya wanadamu.” (New Dictionary of Theology) Nao wengine wamesema kwamba nafsi hizo “zimefungwa ndani ya mwili ili kuadhibiwa kwa dhambi zilizofanya zilipokuwa mbinguni.”—Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature.

Wanafalsafa Wagiriki, kama Sokratesi na Plato, walifundisha hivi: Wakati nafsi inapotoka kwenye mwili wa mwanadamu ndipo tu “inapoacha upumbavu, woga, kutangatanga, tamaa mbaya, na maovu mengine yanayompata mwanadamu,” kisha inaenda kuishi “pamoja na miungu milele.”—Plato’s Phaedo, 81, A.

Baadaye wale wanaoitwa viongozi wa Kikristo waliingiza katika mafundisho yao “wazo hilo la kutokufa kwa nafsi” lililofundishwa na wanafalsafa hao Wagiriki.—Christianity—A Global History.

Linganisha mambo hayo na mafundisho matatu ya msingi yaliyo katika Biblia:

1. Kusudi la Mungu kwa dunia ni kwamba iwe makao ya kudumu ya wanadamu, bali si mahali pa muda pa kuwajaribu wanadamu ili kuona kama wanastahili kuishi pamoja naye mbinguni. Kama Adamu na Hawa wangemtii Mungu, bado wangekuwa hai hapa duniani katika paradiso.—Mwanzo 1:27, 28; Zaburi 115:16.

2. Ingawa dini nyingi zinafundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa, yaani, kitu fulani kinachokaa ndani yake, Biblia inafundisha jambo tofauti na rahisi kueleweka. Mwanadamu ni “nafsi hai” aliyeumbwa kutokana na “mavumbi ya nchi.” (Mwanzo 2:7) Biblia haisemi kamwe kwamba nafsi haiwezi kufa. Inasema kuwa nafsi inaweza kuuawa au kuharibiwa, na hivyo kufanya isiwepo kabisa. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4, 20) Adamu, aliyekuwa nafsi ya kwanza, alikufa hakika na kurudi mavumbini ambako alitoka. Alirudia hali ya kutokuwapo.—Mwanzo 2:17; 3:19.

3. Wakati ujao wa mwanadamu hautegemei kuwa na nafsi isiyoweza kufa ambayo huondoka na kwenda katika makao fulani ya roho, badala yake inategemea ahadi ya Mungu ya kuwafufua watu waishi katika dunia paradiso.—Danieli 12:13; Yohana 11:24-26; Matendo 24:15.