Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Alitoka Wapi?

Yesu Alitoka Wapi?

Yesu Alitoka Wapi?

‘Pilato aliingia ndani ya jumba la gavana tena na kumwambia Yesu: “Wewe ni mtu wa kutoka wapi?” Lakini Yesu hakumjibu.’—YOHANA 19:9.

GAVANA Mroma Pontio Pilato aliuliza swali hilo Yesu alipokuwa akikabili hukumu iliyohusisha uhai wake. * Pilato alijua sehemu ambayo Yesu alitoka katika nchi ya Israeli. (Luka 23:6, 7) Pia, alijua kwamba Yesu hakuwa mwanadamu wa kawaida. Je, huenda Pilato alifikiri kuwa Yesu aliwahi kuishi kabla ya kuzaliwa duniani? Je, mtawala huyu wa kipagani alikuwa tayari kukubali ukweli na kutenda kupatana nao? Vyovyote vile, Yesu alikataa kumjibu na mwishowe ikathibitika wazi kuwa Pilato alipendezwa zaidi na kazi yake kuliko alivyopendezwa na kufuata ukweli na haki.—Mathayo 27:11-26.

Inapendeza kujua kwamba wale wanaotaka kujua kwa moyo mnyofu mahali Yesu alikotoka wanaweza kufanya hivyo kwa urahisi. Biblia inaeleza waziwazi mahali ambako Yesu Kristo alitoka. Fikiria mambo yafuatayo.

Mahali alikozaliwa Makadirio ya kisasa yanaonyesha kuwa mwanzoni mwa mwezi wa Oktoba (Mwezi wa 10), mwaka wa 2 K.W.K., Yesu alizaliwa katika hali za chini katika kijiji cha Yudea huko Bethlehemu. Amri ya kuandikisha watu iliyotolewa na Kaisari Augusto ilimfanya Maria, mama ya Yesu, pamoja na mume wake Yosefu wasafiri hadi Bethlehemu, eneo la watu wa ukoo wa Yosefu. Wakati huo Maria alikuwa “karibu kuzaa.” Kwa kuwa hawakuweza kupata mahali pa kukaa katika kijiji hicho ambacho wakati huo kilikuwa na watu wengi, Yosefu na Maria waliamua kukaa kwenye zizi. Yesu alizaliwa hapo na kuwekwa kwenye hori.—Luka 2:1-7.

Biblia ilikuwa imetabiri karne kadhaa mapema kuhusu mahali ambapo Yesu angezaliwa, ikisema: “Nawe, Ee Bethlehemu Efratha, wewe uliye mdogo sana kuwa kati ya maelfu ya Yuda, kutoka kwako atanijia yeye atakayekuwa mtawala katika Israeli.” * (Mika 5:2) Yaelekea Bethlehemu ulikuwa mji mdogo sana hivi kwamba haungewekwa kwenye orodha ya majiji ya Yuda. Hata hivyo, mji huo mdogo ungekuja kupata heshima ya pekee. Masihi aliyeahidiwa, au Kristo, angezaliwa Bethlehemu.—Mathayo 2:3-6; Yohana 7:40-42.

Mahali alikolelewa Baada ya kukaa kwa muda mfupi huko Misri, familia ya Yesu ilihamia Nazareti, jiji lililokuwa katika wilaya ya Galilaya, kilomita 100 hivi kaskazini ya Yerusalemu. Wakati huo Yesu alikuwa na umri usiozidi miaka mitatu. Katika eneo hilo maridadi ambapo wakulima, wachungaji, na wavuvi waliendesha biashara zao, Yesu alilelewa katika familia kubwa, ambayo yaelekea haikuwa familia tajiri.—Mathayo 13:55, 56.

Karne kadhaa mapema Biblia ilitabiri kuwa Masihi angekuwa “Mnazareti.” Mathayo, mwandikaji wa Injili anasema kuwa familia ya Yesu ilihamia “Nazareti, ili lipate kutimizwa lile lililosemwa kupitia manabii: ‘Yeye ataitwa Mnazareti.’” (Mathayo 2:19-23) Inaonekana kuwa jina Mnazareti linahusiana na neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “chipukizi.” Bila shaka, Mathayo alikuwa akirejelea unabii wa Isaya uliomwita Masihi “chipukizi” kutoka katika kisiki cha Yese, ikimaanisha kwamba Masihi angekuwa mzao wa Yese, baba ya Mfalme Daudi. (Isaya 11:1) Hivyo,Yesu alikuwa mzao wa Yese kupitia Daudi.—Mathayo 1:6, 16; Luka 3:23, 31, 32.

Mahali alikotoka Biblia inafundisha kuwa maisha ya Yesu yalianza miaka mingi kabla ya kuzaliwa katika zizi huko Bethlehemu. Unabii wa Mika, ulionukuliwa mwanzoni, unaendelea kusema, “asili yake ni kutoka nyakati za kale, kutoka siku za wakati usio na kipimo.” (Mika 5:2) Kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu hapa duniani Yesu, Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu, alikuwa kiumbe wa roho huko mbinguni. Yesu mwenyewe alisema: “Nimeshuka kutoka mbinguni.” (Yohana 6:38; 8:23) Hilo liliwezekana jinsi gani?

Kupitia roho takatifu, Yehova Mungu alifanya muujiza wa kuhamisha uhai wa Mwana wake wa kimbingu hadi katika tumbo la uzazi la bikira Myahudi, Maria, ili azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu. * Si jambo gumu kwa Mungu Mweza-Yote kufanya muujiza kama huo. Kama tu malaika alivyomweleza Maria, “kwa Mungu hakuna tangazo lolote lisilowezekana.”—Luka 1:30-35, 37.

Kando na kutupa habari kuhusu mahali ambako Yesu alitoka, Biblia inatueleza mengi zaidi. Vitabu vinne vya Injili—Mathayo, Marko, Luka, na Yohana—vinatueleza mengi kuhusu jinsi alivyoishi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa habari zaidi kuhusu kukamatwa kwa Yesu na kesi yake, ona makala yenye kichwa “Kesi Iliyoendeshwa Vibaya Zaidi Kuliko Zote,” kwenye ukurasa wa 18-22 wa gazeti hili.

^ fu. 6 Efratha (au Efrathi) ni jina la awali la Bethlehemu.—Mwanzo 35:19.

^ fu. 10 Katika Biblia, jina la kibinafsi la Mungu ni Yehova.