Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Wakati Unapojihisi Mpweke na Mwenye Woga?

Je, Kuna Wakati Unapojihisi Mpweke na Mwenye Woga?

Wafundishe Watoto Wako

Je, Kuna Wakati Unapojihisi Mpweke na Mwenye Woga?

WATU wengi leo hujihisi wapweke na kufikiri kuwa hakuna mtu anayewajali kikweli. Mara nyingi wazee huhisi hivyo. Lakini watoto wengi leo, hata wale wanaomtumikia Mungu, hujihisi wapweke na wenye woga. Je, unajua ni kwa nini? *

Kunaweza kuwa na sababu nyingi. Hebu tuone mfano wa mtu aliyeishi zamani sana—miaka elfu moja hivi kabla ya Yesu kuzaliwa. Jina lake ni Eliya. Aliishi wakati ambapo watu katika taifa la Israeli walikuwa wameacha kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova. Wengi wao walikuwa wameanza kumwabudu mungu wa uwongo Baali. Eliya alisema: “Ni mimi peke yangu nimebaki.” Lakini unafikiri Eliya tu ndiye aliyekuwa bado anamtumikia Yehova?

Eliya hakujua kwamba kulikuwa na watu wengine nchini Israeli ambao bado walikuwa wanamtumikia Mungu wa kweli. Lakini walikuwa wamejificha. Waliogopa. Je, unajua ni kwa nini?

Ahabu mfalme wa Israeli alikuwa ameacha kumtumikia Yehova; alikuwa akiabudu Baali, mungu wa uwongo wa mke wake mwovu ambaye aliitwa Yezebeli. Kwa hiyo, Yezebeli na mume wake Ahabu walikuwa wakijaribu kuwatafuta wale waliomtumikia Yehova ili wawaue. Walitaka sana kumuua Eliya na hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Eliya akimbie. Alisafiri umbali wa kilomita 480 hivi, mpaka kwenye jangwa la Horebu, eneo ambalo pia linaitwa Sinai katika Biblia. Miaka mingi kabla ya siku za Eliya, Yehova aliwapa watu wake zile Amri Kumi na Sheria nyinginezo wakiwa katika eneo hilo. Eliya alijificha pangoni huko Horebu akiwa peke yake. Je, unafikiri kwamba Eliya alipaswa kuogopa?

Biblia inaonyesha kwamba awali Yehova alimtumia Eliya kufanya miujiza mikubwa. Wakati mmoja Yehova alijibu sala ya Eliya ya kutaka moto utoke mbinguni na kuteketeza dhabihu fulani. Kwa njia hiyo, Yehova alithibitisha kwamba Yeye ndiye Mungu wa kweli, bali si Baali. Sasa, akiwa pangoni, Yehova alizungumza naye.

“Una kazi gani hapa, Eliya?” Yehova akamuuliza. Naye akasema, ‘Ni mimi peke yangu nimebaki kati ya wale wanaokuabudu.’ Kisha Yehova akamrekebisha Eliya akisema, ‘Bado nina watu elfu saba wanaonitumikia.’ Yehova alimwambia Eliya arudi, akimweleza kwamba Alikuwa na kazi nyingi sana aliyotaka afanye.

Unafikiri tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Eliya?— Hata wale wanaomtumikia Yehova wanaweza kuwa na woga nyakati nyingine. Kwa hiyo, sote, vijana kwa wazee, tunahitaji kukumbuka kumwomba Yehova atusaidie. Biblia inaahidi hivi: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.”

Kuna jambo lingine tunalojifunza: Tuna ndugu na dada kila mahali ambao wanampenda Yehova na wanatupenda pia. Biblia inasema: “Mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu [zetu] ulimwenguni.” Je, hufurahi kujua kwamba hakuna wakati tunapoachwa peke yetu kabisa?

Soma katika Biblia yako

1 Wafalme 19:3-18

Kumbukumbu la Torati 5:1-22

Zaburi 145:18

1 Petro 5:9

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.