Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Alimuumba Ibilisi?

Je, Mungu Alimuumba Ibilisi?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Mungu Alimuumba Ibilisi?

▪ Kwa kuwa Biblia inasema kwamba Mungu ndiye “aliyeviumba vitu vyote,” wengine wamefikia mkataa kuwa lazima yeye ndiye aliyemuumba Ibilisi. (Waefeso 3:9; Ufunuo 4:11) Lakini Biblia inaonyesha waziwazi kuwa hakumuumba.

Yehova aliumba kiumbe aliyegeuka kuwa Ibilisi. Hivyo, lazima kuwapo kwa Ibilisi akiwa mpinzani mkuu wa Mungu kupatane na yale ambayo Maandiko yanafunua kumhusu Yehova akiwa Muumba. Maandiko yanasema hivi kumhusu Mungu: “Kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.” (Kumbukumbu la Torati 32:3-5) Kupatana na andiko hilo tunaweza kusema kuwa mwanzoni Shetani alikuwa mkamilifu na mwadilifu, yaani, alikuwa mmoja wa malaika wa Mungu. Katika andiko la Yohana 8:44, Yesu alisema kuwa Ibilisi “hakusimama imara katika kweli,” akimaanisha kuwa kuna wakati ambapo Shetani hakuwa mwongo wala mwenye hatia.

Hata hivyo, kama viumbe wengine wenye akili wa Yehova, malaika aliyegeuka kuwa Shetani alikuwa na uhuru wa kuchagua kati ya mema na mabaya. Kwa kuchagua kumpinga Mungu na kuwachochea wanadamu wawili wa kwanza wajiunge naye, alijifanya mwenyewe kuwa Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani.”—Mwanzo 3:1-5.

Kiumbe huyo wa roho ambaye ni mwovu pia alijifanya mwenyewe kuwa Ibilisi, jina linalomaanisha “Mchongezi.” Shetani ndiye yule kiumbe asiyeonekana ambaye alitumia nyoka na kwa ujanja akamdanganya Hawa asitii sheria ya Muumba iliyokuwa wazi. Hiyo ndiyo sababu Yesu alimwita Shetani “baba ya uwongo.”—Yohana 8:44.

Hata hivyo, ingewezekana jinsi gani kwa kiumbe wa roho aliye mkamilifu—asiyekuwa na udhaifu wowote ndani yake wala uvutano mwovu kutoka kwa wengine—kuwa na mwelekeo mbaya? Shetani alitamani ibada ambayo ni ya Mungu peke yake na akaona uwezekano wa kuwaweka wanadamu chini ya utawala wake badala ya utawala wa Yehova. Shetani aliendelea kufikiria uwezekano wa kuwatawala wanadamu na badala ya kuliondolea mbali wazo hilo, akaliacha libaki katika akili yake, na hatimaye akachukua hatua. Kitabu cha Yakobo kinasema hivi kuhusu hali hiyo: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”—Yakobo 1:14, 15; 1 Timotheo 3:6.

Kwa mfano: Fikiria mtunzaji wa hesabu anayepata nafasi ya kubadili-badili rekodi za hesabu ili kuiibia kampuni pesa. Anaweza kuondolea mbali wazo hilo baya. Lakini ikiwa badala ya kufanya hivyo ataendelea kufikiria uwezekano huo wa kuiba, jambo hilo litaanza kumvutia, na yaelekea ataiba. Akiiba, kwa kweli atajifanya mwenyewe kuwa mwizi. Akidanganya kuhusu wizi huo, atakuwa mwongo pia. Vivyo hivyo, kwa kusitawisha tamaa mbaya na kutenda kulingana na tamaa hizo, malaika ambaye Mungu alimuumba alitumia uhuru wake wa kuchagua kudanganya na kumwasi Baba yake, na hivyo kujifanya mwenyewe kuwa Shetani Ibilisi.

Tunafurahi kuwa Shetani Ibilisi ataharibiwa na Mungu katika wakati Wake unaofaa. (Waroma 16:20) Sasa, waabudu wa Yehova Mungu wanajua mbinu za Shetani na wanalindwa dhidi ya hila zake. (2 Wakorintho 2:11; Waefeso 6:11) Hivyo basi, jitahidi kadiri uwezavyo ‘kumpinga Ibilisi, naye atakukimbia.’—Yakobo 4:7.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Kwa kuchagua kumpinga Mungu, malaika mkamilifu alijifanya mwenyewe kuwa Shetani