Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Biblia Inashutumu Kucheza Kamari?

Je, Biblia Inashutumu Kucheza Kamari?

Je, Biblia Inashutumu Kucheza Kamari?

MARA nyingi sinema na vipindi vya televisheni vinavyopendwa na wengi vimeonyesha mchezo wa kamari—hasa kwenye kasino (majengo ya kuchezea kamari)—kuwa burudani inayofurahiwa na watu wenye kuvutia, matajiri, na wastaarabu. Ingawa hivyo, kwa ujumla watazamaji wa mchezo huo wanajua kuwa mambo wanayotazama si ya kweli.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba uuzaji wa tikiti za bahati na nasibu, mapatano ya kulipa kiasi fulani cha pesa ikitegemea matokeo ya mchezo fulani, na kucheza kamari kwenye Intaneti ni mambo yanayowapa ushindani mkali wale wanaendesha mchezo wa kamari kwenye kasino. Mchezo wa kamari ni “zoea baya ambalo limeenea kama moto wa msitu,” kinasema kitabu Internet Gambling. Sasa mchezo wa karata unaonyeshwa kwenye televisheni na Intaneti kuwa mchezo unaopendwa na wengi. Kulingana na gazeti moja la habari, wataalamu wanakadiria kuwa idadi ya watu wanaocheza karata nchini Marekani imeongezeka mara mbili katika miezi 18 ya hivi karibuni.

Mchezo wa kamari umefafanuliwa kuwa mchezo wa kubahatisha ambapo wachezaji hutoa kiasi fulani cha pesa. Watu wengi husema kwamba mchezo wa kamari si mbaya ikiwa mtu anayeucheza anatumia pesa zake mwenyewe na mchezo huo haumfanyi kuwa mtumwa. Hata, kitabu kimoja cha marejeo (New Catholic Encyclopedia) kinasema kuwa mchezo wa kamari “hauonwi kuwa dhambi isipokuwa yule anayeucheza awe anapuuza majukumu yake.” Hata hivyo, hakuna Maandiko yanayotajwa ili kuunga mkono maneno hayo. Hivyo basi, Mkristo anapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kucheza kamari? Je, Biblia inaunga mkono au kushutumu mchezo huo?

Ni vizuri kukumbuka kwamba Maandiko Matakatifu hayataji mchezo wa kamari moja kwa moja. Hata hivyo, hilo halimaanishi kuwa hakuna mwongozo wowote kuhusu jambo hilo. Badala ya kutoa sheria kuhusu kila jambo au hali, Biblia inatutia moyo ‘tuendelee kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.’ (Waefeso 5:17) Kulingana na msomi wa Biblia E. W. Bullinger, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kufahamu,” linamaanisha kupata uelewaji wa mambo mbalimbali yanayohusu suala fulani kupitia “ujuzi unaopatikana kwa kutafakari kwa uzito kuhusu suala hilo.” Hivyo, Mkristo anaweza kufahamu mapenzi ya Mungu kuhusu mchezo wa kamari kwa kupata uelewaji na kutafakari kwa uzito kanuni mbalimbali za Biblia kuuhusu. Unaposoma maandiko yaliyotajwa katika mazungumzo yanayofuata, huenda ukajiuliza: ‘Je, andiko hili linaunga mkono mchezo wa kamari? Neno la Mungu linaonyesha mapenzi yake ni nini kuhusu mchezo huu?’

Kishawishi cha Kupata Ushindi

Kwa kuwa kamari ni mchezo wa kubahatisha tu, imani katika bahati—nguvu fulani isiyojulikana ambayo inasemekana kuwa inadhibiti matukio hayo yasiyopangwa—inahusika sana, hasa ikiwa pesa zinashindaniwa. Kwa mfano, namba ambazo zinaaminika kuwa zinaleta ushindi ndizo zinazowekwa kwenye tikiti za bahati nasibu; wachezaji wenye ushirikina wa mah-jongg (mchezo wa kamari wa Kichina) wanakatazwa kutaja maneno fulani; na dadu hupuliziwa hewa kabla ya kurushwa. Kwa nini? Mara nyingi, wachezaji wa kamari wanaamini kwamba bahati itakuwa, au angalau inaweza kuwa, na uvutano juu ya matokeo.

Je, kutegemea bahati ni mchezo tu usio na madhara yoyote? Watu fulani katika Israeli la kale walikuwa na maoni hayo. Waliamini kuwa bahati ingeweza kuwaletea mafanikio. Yehova Mungu alihisi jinsi gani kuhusu jambo hilo? Kupitia nabii wake Isaya, Mungu aliwaambia: “Ninyi ndio wale watu wanaomwacha Yehova, wale wanaousahau mlima wangu mtakatifu, wale wanaoandaa meza kwa ajili ya mungu wa Bahati Njema na wale wanaojaza divai iliyochanganywa kwa ajili ya mungu wa Majaliwa.” (Isaya 65:11) Machoni pa Mungu, imani katika bahati ni aina fulani ya ibada ya sanamu na haipatani na ibada ya kweli. Inaonyesha kuwa mtu anatumaini nguvu fulani za kuwaziwa tu badala ya kumtumaini Mungu. Hakuna sababu ya kuamini kwamba Mungu amebadili maoni yake.

Jinsi Watu Wanavyoshinda Zawadi

Iwe mtu anacheza kamari kwenye Intaneti, ananunua tikiti ya bahati nasibu, anafanya mapatano ya kulipa kiasi fulani cha pesa ikitegemea matokeo ya mchezo fulani, au kucheza kamari katika kasino, mara nyingi wachezaji wa kamari hupuuza chanzo cha zawadi wanayotaka kushinda. Mchezo wa kamari ni tofauti na mapatano halali ya kibiashara au ununuzi wa bidhaa fulani, kwa sababu mchezaji anataka kushinda pesa ambazo wachezaji wengine wamepoteza. * Kituo cha Uraibu na Afya ya Akili cha Kanada kinasema, “Ili mtu mmoja aweze kushinda na kuwa milionea katika mchezo wa bahati nasibu, mamilioni ya wengine hupoteza pesa zao!” Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kumsaidia Mkristo aelewe maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo?

Amri ya mwisho kati ya zile Amri Kumi walizopewa Waisraeli inasema: “Usimtamani mke wa mwenzako, wala mtumwa wake wala kijakazi wake wala ng’ombe-dume wake wala punda wake wala chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Kutamani vitu vya mtu mwingine—vitu vyake vya kimwili, mali, na pesa—ilikuwa dhambi nzito, sawa na kumtamani mke wake. Karne kadhaa baadaye, mtume Paulo alirudia amri hiyo kwa Wakristo, akisema: ‘Msitamani.’ (Waroma 7:7) Je, Mkristo anayetaka kushinda kile ambacho mtu mwingine amepoteza anaweza kuwa na hatia ya kutamani?

“Iwe [wachezaji wengi wa kamari] wanakubali au la,” anasema mwandishi J. Phillip Vogel, “kabla ya mchezo kuanza, wachezaji hao hutamani moyoni kushinda pesa nyingi ingawa walitumia pesa kidogo.” Wachezaji hao hutamani kupata utajiri bila kutoa jasho. Kwa kweli, jambo hilo ni kinyume cha shauri la Biblia kuwa Mkristo anapaswa ‘kufanya kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.’ (Waefeso 4:28) Naye mtume Paulo alisema hivi waziwazi: “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, basi na asile chakula.” Aliongeza kusema: “Wale chakula ambacho wao wenyewe wanafanyia kazi.” (2 Wathesalonike 3:10, 12) Lakini je, mchezo wa kamari unaweza kuonwa kuwa kazi halali?

Ingawa mchezo wa kamari unaweza kuwa na ushindani mkali, pesa zozote ambazo mtu hupata huwa ameshinda tu, bali si malipo kwa ajili ya utumishi au kazi ambayo amefanya. Katika mchezo wa kamari, mtu hutoa pesa kujaribu bahati yake, na matokeo hutegemea sana bahati. Mchezaji hutumaini kuwa siku moja atashinda. Kwa ufupi, mchezaji wa kamari hutaka kuvuna mahali ambapo hakupanda. Kwa upande mwingine, Wakristo wa kweli wanatiwa moyo wafanye kazi kwa unyofu ili wapate pesa. “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu,” akaandika Mfalme Sulemani mwenye hekima. Aliongeza kusema: “Hilo . . . linatoka kwenye mkono wa Mungu wa kweli.” (Mhubiri 2:24) Ndiyo, watumishi wa Mungu hawaweki tumaini lao katika mambo ya kubahatisha tu wala hawatafuti njia za mkato za kupata pesa, badala yake wao humtegemea Mungu ili kupata furaha na baraka.

“Mtego” Unaopaswa Kuepukwa

Hata kama mchezaji ataweza kushinda, anapaswa kufikiria si msisimuko wa muda mfupi anaopata baada ya kushinda, bali madhara ya muda mrefu ya kucheza kamari. Andiko la Methali 20:21 linasema: “Urithi hupatikana kwa pupa mwanzoni, lakini wakati wake ujao hautabarikiwa.” Watu wengi wanaoshinda katika mchezo wa bahati nasibu na wachezaji wengine wa kamari wametambua kwa masikitiko kuwa utajiri walioshinda haujawaletea furaha. Inafaa kama nini kufuata shauri la Biblia la kutotumaini “utajiri usio hakika, bali kumtumaini Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.”—1 Timotheo 6:17.

Mbali na kushinda au kupoteza katika mchezo wa kamari, kuna “mtego” mwingine unaopaswa kuepukwa. “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu,” linasema Neno la Mungu. (1 Timotheo 6:9) Mtego unakusudiwa kumnasa mnyama. Watu wengi waliokusudia kutumia pesa kidogo tu katika mchezo wa kamari au kucheza mara chache tu, wamenaswa kabisa na zoea hilo wasiweze kujinasua. Mchezo wa kamari umefanya watu wapoteze kazi, waumize wapendwa wao, na umevunja familia.

Baada ya kuzungumzia maandiko mengi yanayohusu mchezo wa kamari, je, umetambua maoni ya Mungu ni nini kuhusu mchezo huo? Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Mkristo anapaswa kuongozwa na mapenzi ya Mungu, bali si maoni yanayopendwa na wengi. Akiwa “Mungu mwenye furaha,” Yehova anataka tufurahie maisha, bila kupatwa na mabaya yanayotokana na kucheza kamari.—1 Timotheo 1:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Toleo la Amkeni! la Oktoba 8, 2000 (8/10/2000), ukurasa wa 25 mpaka 27, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova, lilieleza jinsi uwekezaji katika soko la hisa unavyotofautiana na mchezo wa kamari.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Watumishi wa Mungu hupata pesa kwa kufanya kazi kwa unyofu

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

Msisimko wa Kushinda

Je, kucheza kamari ni zoea linaloweza kumnasa mtu, na kwa urahisi kumfanya awe mchezaji sugu? Baada ya kufanya uchunguzi kuhusu jinsi wachezaji wa kamari wanavyohisi baada ya kushinda au kupoteza, Dakt. Hans Breiter anasema kwamba “msisimko ambao mtu hupata katika ubongo baada ya kushinda pesa katika mchezo wa kamari, unakuwa sawa na ule ambao mtumiaji wa kokeini hupata baada ya kuitumia.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wachezaji wa kamari hutazamia kushinda pesa za nani?