Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Makusanyiko ya Wilaya ya Wakati wa Kiangazi Nchini Urusi Yaleta Baraka

Makusanyiko ya Wilaya ya Wakati wa Kiangazi Nchini Urusi Yaleta Baraka

Makusanyiko ya Wilaya ya Wakati wa Kiangazi Nchini Urusi Yaleta Baraka

KILA wakati wa kiangazi, Warusi wengi wanaopenda mazingira ya asili huondoka katika nyumba zao za mijini ili kutembelea maeneo ya mashambani na kuishi katika nyumba za wakati wa kiangazi zinazoitwa dachas. Wao hufanya hivyo ili kuepuka kwa muda maisha ya mijini yenye shughuli nyingi. Katika majira kadhaa ya kiangazi yaliyopita, Mashahidi wa Yehova nchini Urusi wamekuwa pia wakienda katika maeneo hayo ya mashambani kwa wingi—lakini wakiwa na kusudi tofauti.

Ingawa katika majiji fulani nchini Urusi Mashahidi wa Yehova wamezuiwa wasihubiri, bado wanaendelea kukutana waziwazi kwa ajili ya ibada kwa kuwa wanafanya kulingana na haki yao ya kikatiba ya kuabudu kwa uhuru. Hata hivyo, nyakati nyingine shida na upinzani wanaopata kutoka kwa makasisi wa Kanisa Othodoksi au kutoka kwa wenye mamlaka waliopashwa habari za uwongo kutuhusu, umefanya iwe vigumu kwao kupata mahali panapofaa pa kufanyia makusanyiko ya wilaya ya kila mwaka, ambayo hufanywa wakati wa kiangazi. Hivyo Mashahidi wamekuwa wakifanya makusanyiko yao “msituni” au “mashambani.” Kuanzia mwaka wa 2007 hadi 2009, makusanyiko hayo yamefanywa karibu mara 40 kotekote nchini Urusi katika maeneo 25 tofauti-tofauti ya mashambani.

Ndugu mmoja ambaye amekuwa akihudhuria makusanyiko nchini Urusi kwa miaka mingi, anasema: “Katika miaka iliyopita, wakati tulipokuwa tukitumia viwanja vya michezo na majumba ya kukodi katika majiji makubwa, wenye mamlaka na watu wengi wanyofu waliweza kuelewa tengenezo letu ni la aina gani kwa sababu ya usafi na utaratibu walioona. Sasa tunalazimika kukutana msituni. Inasikitisha kuwa hakuna mtu anayeweza kuona makusanyiko hayo yenye kupendeza yanayohudhuriwa na watu wa tabaka, jamii, na dini mbalimbali.”

Ingawa wakati wa makusanyiko hayo ni pindi zenye furaha, Shahidi mmoja alikiri hivi: “Inapendeza kuona ushikamanifu wa Mashahidi wenzangu na jinsi wanavyojitolea katika kumtumikia Yehova hata wakiwa chini ya hali ngumu. Lakini, kusema kweli, wenye mamlaka wanapofanya iwe vigumu kwetu kufanya makusanyiko, inaweza kutuathiri kimwili na kihisia. Jambo hilo pia hutuzuia tusimwabudu Mungu mweza-yote kwa uhuru na kwa njia inayomletea heshima.” Mashahidi wa Yehova nchini Urusi wamekabiliana jinsi gani na hali hiyo?

Makusanyiko ya Msituni Yafanywa Kotekote Nchini

Mara nyingi, mikataba ya kukodi mahali pa kufanyia kusanyiko inapovunjwa dakika za mwishomwisho, hilo humaanisha kuwa wasimamizi wa makusanyiko watakuwa na siku chache tu za kutafuta mahali pengine kwa ajili ya maelfu ya wajumbe wanaotazamiwa kuhudhuria. Kwa mfano, mwaka wa 2008, Mashahidi wanaoishi jijini Cheboksary, katika Jamhuri ya Chuvash, walilazimika kufanya kusanyiko lao la wilaya katika uwanja mkubwa wa kupigia kambi uliozungukwa na mibetula, karibu na Mto Volga. Walihitaji kufanya kazi nyingi. Kati ya wajumbe 1,930 waliotazamiwa kuhudhuria, 1,700 walihitaji kutayarishiwa mahali pa kulala katika uwanja huo. Walihitaji kuwa na mabafu na mabeseni ya kunawia mikono yenye mabomba ya maji moto na baridi, vyoo, na umeme. Pia, wajumbe wote walihitaji chakula.

Ndugu walifanya kazi kwa bidii ili kufanikisha kusanyiko hilo. Walitafuta maseremala, mafundi wa umeme, na wa mabomba. Mashahidi wapatao 350 walijitolea kusaidia katika kazi hiyo, na 14 kati yao waliishi katika eneo hilo kwa siku kumi. Walikata mbao kwa misumeno, wakabeba nyasi, na kujenga mahema, mabafu, na vyoo. Ndugu wengine walisafiri mara kadhaa hadi mjini ili kununua vitu mbalimbali vilivyohitajika. Kwa kuwa hakukuwa na mahali pa kuhifadhia chakula, akina ndugu waliamua kuandaa milo mitatu kila siku kwa ajili ya kila mtu aliyekuwapo. Chakula hicho kilipikwa papo hapo uwanjani. Wasimamizi wa uwanja huo waliunga mkono mpango huo kwa kukodi watu wa kuwapikia wajumbe chakula. Hatimaye, wajumbe 500 walikuja na mahema yao wenyewe, 150 wakakodi nyumba zilizokuwa karibu na uwanja huo, 15 wakalalia nyasi kavu kwenye banda la farasi, nao waliobaki wakalala ndani ya mahema yaliyojengwa na akina ndugu.

Wajumbe walipowasili, waliona viti vingi vya plastiki vya rangi ya bluu vilivyopangwa vizuri. Mbele kulikuwa na majukwaa mawili yaliyopambwa kwa maua—moja kwa ajili ya programu ya lugha ya Kirusi na lingine kwa ajili ya programu ya lugha ya Kichuvashi. Kila mtu alifurahia programu hiyo ya kiroho na kuthamini kazi ngumu iliyofanywa na ndugu waliojitolea. Mmoja wa watu waliokuwa wakitayarisha chakula alisema hivi, “Kama nisingeona kwa macho yangu, nisingeamini kuwa kuna tengenezo lenye utaratibu na adabu kama lenu!” Wengine walifananisha makusanyiko hayo na Sherehe ya Vibanda iliyofanywa na taifa la Israeli nyakati za Biblia.

Katika majiji mengine, mara nyingi Mashahidi walikuwa na siku moja tu ya kutafuta na kutayarisha mahali pengine pa kufanyia kusanyiko la wilaya. Hali ilikuwa hivyo huko Nizhniy Novgorod, ambako wajitoleaji walihitaji kufanya kazi kwa zamu usiku na mchana ili kutayarisha mahali pa kufanyia kusanyiko katika kiwanja fulani cha mtu binafsi. Walihitaji kukata miti, nyasi na kuondoa kupe na chungu. Kufikia Ijumaa (Siku ya 5) asubuhi wakati wajumbe walipowasili, wajitoleaji walikuwa wameleta viti 2,000 vya plastiki na vyoo kumi vinavyoweza kubebwa, wakatayarisha mabeseni ya kunawia mikono, wakajenga jukwaa, na kutayarisha jenereta na mfumo wa sauti. Ndugu mmoja alisema: “Jambo la kushangaza ni kwamba ndugu waliofanya kazi usiku na mchana hawakutaka watendewe kama mashujaa. Waliendelea kuwahudumia wengine kwa unyenyekevu wakati wa kusanyiko hilo. Walitumia nguvu zao ili ndugu na dada zao wajihisi wamestarehe na kufurahia mafundisho ya kiroho.”

Ndugu mwingine anaandika: “Kulikuwa na roho ya ushirikiano kati ya wafanyakazi. Ingawa ilikuwa mara ya kwanza kwa akina ndugu kupanga kusanyiko kama hilo na hawakuwa na wakati mwingi, bado walifikiria kila kitu kilichohitajika ili wakati wa programu, kusiwe na mambo mengi yenye kukengeusha fikira. Baada ya kazi hiyo, hatukuhisi uchovu. Tulihisi kana kwamba Yehova alitupa kila mmoja wetu mabawa!”

Roho ya Mungu Yatenda Kazi

Kushughulikia matatizo yaliyotokana na kukosa mahali pa kufanyia makusanyiko kuliwasaidia akina ndugu katika njia nyingi kuwa na uhusiano mzuri, na pia kuthibitisha kwamba roho ya Mungu inatenda kazi. Huko Smolensk, sehemu nyingi za kulala zilizokuwa zimekodiwa zilifutiliwa mbali siku moja kabla ya kusanyiko kuanza. Mzee mmoja anasema hivi: “Wakati mabasi kadhaa ya wajumbe yalipowasili saa saba usiku, hatukuwa tumepata mahali pa kulala. Nilianza kulia kwa kuwa singeweza kuwasaidia. Nilisali kwa Yehova, nikimsihi atatue tatizo hilo. Nilifurahi kama nini kwa kuwa baada ya muda wa saa moja tulikuwa tumepata mahali pa kulala kwa ajili ya kila mtu! Hilo ni jambo lenye kushangaza sana, na ni uthibitisho kuwa Yehova hawezi kuwaacha waadilifu wake bila msaada!” Katika kusanyiko lingine la msituni, akina ndugu waliamua kuomba mahali pa kulala katika kijiji kimoja, na kwa sababu ya sifa nzuri za Mashahidi katika eneo hilo, wanakijiji walijitolea kuwapa wajumbe 2,000 mahali pa kulala katika nyumba zao wakati wa kusanyiko.

“Kwa kuwa tulifaulu kufanya kusanyiko letu, hilo lilituonyesha wazi umuhimu wa kumtegemea Yehova chini ya hali zote,” anasema Shahidi mmoja. Jambo hilo lilionekana wazi wakati watu fulani wasiotazamiwa walipotokea na kutaka kuvuruga kusanyiko. Katika mji wa Novoshakhtinsk, kiongozi wa Kanisa Othodoksi la Urusi na waandamanaji wenzake walitokea wakiimba nyimbo za dini na kupiga kelele wakitumia vikuza-sauti ili wasikilizaji wasiweze kumsikia msemaji. Hata hivyo, polisi waliwazuia wasivuruge programu. Wakati mwanamke mmoja, mfuasi wa Kanisa Othodoksi aliyekuwa katika maandamano hayo alipozirai kwa sababu ya joto, akina ndugu walimpeleka kwenye Idara ya Huduma ya Kwanza na kumsaidia. Alishangazwa sana na kitendo hicho.

Washangazwa na Mambo Waliyoona

Kwa sababu ya wasiwasi wa kushambuliwa na magaidi, maofisa wa usalama na watu wenye udadisi nchini Urusi hutaka kujua kinachoendelea wakati watu wanapokusanyika kwa wingi. Kwa mfano, katika kusanyiko la msituni lililofanywa Volzhskiy kulikuwa na maofisa kadhaa wa kikosi cha kupambana na watu wenye msimamo mkali kisiasa. Mmoja wao alipoteza simu yake ya mkononi programu ilipokuwa ikiendelea, na akina ndugu walimsaidia kuitafuta na wakaipata kwenye Idara ya Vilivyopotea na Kupatikana. Muda mfupi baadaye, alipigiwa simu na mkubwa wake aliyetaka kujua kama kwenye kusanyiko hilo kulikuwa na uchochezi wowote wa kufanya jeuri au watu wenye msimamo mkali kisiasa. Ofisa huyo alimjibu: “Kila kitu ni shwari; watu 5,000 wamekusanyika na hakuna anayevunja sheria. Ati unasema watu wenye msimamo mkali! Fikiria hili. Nilipoteza simu yangu nao wakaitafuta na kunirudishia!”

Mlinzi mmoja alishangazwa sana na usafi katika eneo hilo la kusanyiko. Ingawa kulikuwa na watoto wengi waliohudhuria, hakupata hata karatasi moja ya kufungia peremende. Mmiliki wa lile eneo la kupigia kambi ambapo kusanyiko lingine lilifanyiwa, alikutana na polisi aliyekuwa amepashwa habari kuwa kuna mkutano mkubwa wa kidini uliokuwa ukiendelea. Alimpeleka luteni huyo wa polisi kwenye baraza ya ghorofa ya tatu ya nyumba iliyokuwa karibu na uwanja huo na kumwambia: “Hebu watazame! Unaweza kujionea mwenyewe. Wana utaratibu mzuri sana!” Mmiliki huyo alishangaa kwa kuwa Mashahidi hawakunywa pombe wala kuvuta sigara, na waliondoka na kuacha mahali hapo pakiwa safi, hata takataka zao waliondoka nazo. Alisema hivi kwa mshangao: “Ilikuwa kama paradiso!”

Umoja Kati ya Watu wa Mungu Unaonekana Wazi

Baada ya kusanyiko moja la msituni, msimamizi wa kijiji kilichokuwa karibu alisema hivi: “Ninaelewa kuwa ninyi ni watu wenye kiasi, lakini mna nguvu nyingi. Wakati sisi hatutaki kuchangamana na watu wengine, ninyi mna uwezo wa kuwaunganisha watu!” Kuanzia Kaliningrad hadi Kamchatka, raia wa nchi hii kubwa wanaendelea kushangazwa sana na umoja unaoonyeshwa na watumishi wa Mungu katika makusanyiko yao makubwa ambako wanafunzwa Biblia. Ingawa nyakati nyingine huenda ikawabidi kubadili mipango yao kwa haraka na bila kutazamia, jambo moja halitawahi kubadilika, yaani, mtazamo wao wenye heshima kuwaelekea wenye mamlaka na wanadamu wenzao.

Hata hali iweje, Mashahidi wa Yehova nchini Urusi wanaendelea kukutana kwa shangwe ili kupokea mafundisho ya kiroho. Wanasali “kwa ajili ya wafalme na wale wote walio katika cheo cha juu; ili [waendelee] kuishi maisha shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.”—1 Timotheo 2:2.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Shahidi mmoja aliyejitolea, akisaidia kufanya matayarisho kwa ajili ya kusanyiko

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Mashahidi wa Yehova nchini Urusi wanaendelea kuishi “maisha shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili”

[Picha katika ukurasa wa 28]

Wajitoleaji walifanya kazi pamoja kusafisha uwanja kabla ya kusanyiko na kutayarisha chakula kwa ajili ya maelfu ya wajumbe waliohudhuria kusanyiko

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kila mtu alifurahia programu ya kiroho na kuthamini kazi ngumu iliyofanywa na ndugu waliojitolea