Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa Mmoja wa Watoto wa Mungu

Kuwa Mmoja wa Watoto wa Mungu

Kuwa Mmoja wa Watoto wa Mungu

MIAKA 30 hivi iliyopita baada ya Vita vya Korea, Mfumo wa Utangazaji wa Korea ulianzisha programu ya kuwasaidia watu kuwapata washiriki wa familia yao ambao walipotea tangu wakati wa vita. Matokeo yalikuwa nini? Watu zaidi ya 11,000 waliungana tena na wapendwa wao, wakalia machozi, wakakumbatiana, na kufanya mambo mengine. Gazeti moja (Korea Times) liliripoti hivi: “Watu wa Korea hawajawahi kamwe kulia kwa furaha hivyo.”

Huko Brazili, wazazi wa Cézar walimkabidhi kwa mtu mwingine ili kulipia deni. Miaka kumi baadaye, alifurahi sana kumpata mama yake halisi hivi kwamba aliwaacha wazazi wake walezi waliokuwa matajiri ili aishi na mama yake.

Washiriki wa familia wanafurahi sana wanapokutana tena baada ya kutengana na kupoteana! Biblia inaeleza jinsi wanadamu walivyotenganishwa na familia ya Mungu kwa njia yenye kusikitisha. Inatuambia pia jinsi wanavyoungana sasa kwa furaha. Hilo lilitukia jinsi gani? Nawe unaweza kushiriki furaha hiyo namna gani?

Jinsi Familia ya Mungu Ilivyotenganishwa

Mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu Muumba, Yehova Mungu: “Kwako wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Yehova ndiye Baba ya familia kubwa ya ulimwenguni pote ya viumbe waaminifu wenye akili. Familia hiyo inatia ndani sehemu ya kimbingu yenye malaika ambao ni watoto wake wa kiroho, na sehemu ya kidunia ambayo ina wanadamu ambao ni watoto wake wa kidunia.

Adamu, mwanadamu wa kwanza aliyekuwa mwana wa Mungu, alipoasi kama habari iliyotangulia ilivyosema, kwa huzuni wanadamu walijitenga kutoka kwa Baba yao mwenye upendo na Muumba. (Luka 3:38) Hiyo ni kwa sababu Adamu alipoasi alipoteza na kuwapotezea wazao wake ambao hawakuwa wamezaliwa pendeleo la kuwa watoto wa Mungu. Kupitia mtumishi wake Musa, Mungu alieleza matokeo ya jambo lililotukia: “Wametenda kwa uharibifu; wao si watoto [wa Mungu], kasoro ni yao wenyewe.” “Kasoro,” au hali ya dhambi, iliwatenganisha wanadamu kutoka kwa Mungu, ambaye ni mtakatifu na mkamilifu katika kila njia. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Isaya 6:3) Hivyo basi, ni kana kwamba wanadamu walipotea na kuwa bila baba.—Waefeso 2:12.

Ili kukazia jinsi ambavyo wanadamu wametenganishwa na Mungu, Biblia inasema kwamba wale ambao si sehemu ya familia ya Mungu ni “adui.” (Waroma 5:8, 10) Wakiwa wametenganishwa na Mungu, wanadamu wameteseka chini ya utawala katili wa Shetani na madhara ya dhambi na kutokamilika ambako walirithi. (Waroma 5:12; 1 Yohana 5:19) Je, wanadamu wenye dhambi wanaweza kuwa sehemu ya familia ya Mungu? Je, viumbe wasio wakamilifu wanaweza kuwa watoto wa Mungu kwa njia kamili, kama Adamu na Hawa walivyokuwa kabla hawajatenda dhambi?

Kuwakusanya Watoto Waliotenganishwa

Kwa upendo, Yehova alifanya mipango ambayo ingewafaidi watu wasio wakamilifu ambao wanampenda. (1 Wakorintho 2:9) Mtume Paulo anaeleza hivi: “Mungu kupitia Kristo alikuwa akiupatanisha ulimwengu kwake mwenyewe, bila kuwahesabia makosa yao.” (2 Wakorintho 5:19) Kama ilivyoelezwa katika habari iliyotangulia, Yehova Mungu alimtoa Yesu Kristo kuwa dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya dhambi zetu. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Mtume Yohana aliandika hivi kwa uthamini: “Oneni namna ya upendo ambao Baba ametupa sisi, ili tuitwe watoto wa Mungu.” (1 Yohana 3:1) Hivyo, njia ilifunguliwa ili wanadamu watiifu wawe tena sehemu ya familia ya Yehova.

Ingawa wanadamu wote wanaokusanywa katika familia ya Mungu watakuwa na umoja mzuri ajabu wanapotunzwa na Baba yao wa mbinguni, ona jinsi Biblia inavyoeleza namna wanavyokusanywa katika vikundi viwili. Tunasoma hivi: “Ni kulingana na upendezi [wa Mungu] mwema alioukusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi, yaani, kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:9, 10) Kwa nini Mungu anasimamia vitu kwa njia hiyo?

Kwa kweli, Yehova anapopanga watoto wake katika vikundi viwili anatokeza upatano katika familia yake. Si vigumu kuelewa jambo hilo. Familia ya Mungu ni kubwa sana hivi kwamba inaweza kulinganishwa na taifa. Katika taifa lolote lile, ni watu wachache wanaochaguliwa kuunda serikali ili wengine wafurahie amani na utaratibu. Bila shaka, hakuna serikali yoyote ya wanadamu ambayo imeleta amani ya kweli, lakini Mungu anaweka serikali kamilifu isimamie familia yake. Kikundi cha kwanza, “vitu vilivyo mbinguni,” kinatia ndani watoto wa Mungu ambao wanachaguliwa na Yehova kuunda serikali, au Ufalme, mbinguni. Wakiwa huko, “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.”—Ufunuo 5:10.

Watoto wa Mungu Duniani

Yehova anakusanya pia “vitu vilivyo duniani,” yaani, mamilioni ya watu duniani pote, ili mwishowe wawe watoto wake wa kidunia. Akiwa Baba mwenye fadhili, anawafundisha njia zake za upendo ili waungane kwa umoja ingawa wanatoka katika mataifa mengi. Hata watu ambao ni wajeuri, wenye ubinafsi, wenye maadili mapotovu, na wasiomtii Mungu wanaalikwa ili ‘wapatanishwe pamoja na Mungu.’—2 Wakorintho 5:20.

Namna gani wale ambao wanakataa mwaliko wa Mungu wa kupatanishwa naye wakiwa watoto wake? Ili kuhakikisha kwamba familia yake ina amani na umoja, Yehova atawachukulia watu kama hao hatua kali. Kutakuwa na “siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Petro 3:7) Mungu atawaondoa waasi wote duniani. Hilo litawaletea faraja kama nini wale wanaotii!—Zaburi 37:10, 11.

Kisha kutakuwa na miaka 1,000 ya amani. Wakati huo, wote wanaoitikia upendo wa Mungu watarudishiwa hatua kwa hatua maisha makamilifu ambayo Adamu alipoteza. Hata wafu watafufuliwa. (Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:6; 21:3, 4) Hivyo, Mungu atatimiza ahadi hii: “Uumbaji wenyewe [wanadamu] pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:21.

Kuunganishwa na Baba Yako

Cézar na maelfu ya Wakorea wengine waliotajwa mwanzoni mwa habari hii walihitaji kuchukua hatua ili waungane tena na familia zao. Watu hao wa Korea walihitaji kujiunga na programu ya kuwaunganisha watu wa familia, naye Cézar aliwaacha wazazi wake walezi. Vivyo hivyo, huenda ukahitaji kuchukua hatua thabiti ya kupatanishwa na Baba yako wa mbinguni, Yehova Mungu, na kuwa sehemu ya familia yake. Unapaswa kufanya nini?

Ili umkaribie Mungu akiwa Baba yako, ni lazima ujifunze Neno lake, Biblia, ili usitawishe imani yenye nguvu katika Mungu na katika ahadi zake. Utajifunza kuamini kwamba yale ambayo Mungu anataka ufanye ni kwa faida yako. Pia, utahitaji kukubali Mungu akurekebishe na kukutia nidhamu, kwa kuwa Biblia inawaambia Wakristo hivi: “Mungu anawatendea ninyi kama wana. Kwa maana ni mwana gani ambaye baba hamtii nidhamu?”—Waebrania 12:7.

Njia yako ya maisha itabadilika kabisa ukichukua hatua hizo. Biblia inasema: ‘Unapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yako, na unapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’ (Waefeso 4:23, 24) Kisha, fuata himizo hili la mtume Petro: “Kama watoto wenye utii, msikubali kamwe kufuata tena tamaa mbaya mlizokuwa nazo wakati mlipokuwa wajinga.”—1 Petro 1:14, Biblia Habari Njema.

Kupata Familia Yako ya Kweli

Cézar alipompata mama yake, alifurahi sana kujua kwamba alikuwa pia na ndugu na dada yake. Vivyo hivyo, unapomkaribia Baba yako wa mbinguni, utagundua kwamba una ndugu na dada wengi katika kutaniko la Kikristo. Unaposhirikiana nao, huenda utaona kwamba mna uhusiano wa karibu zaidi kuliko washiriki wa familia yenu ya kimwili.—Matendo 28:14, 15; Waebrania 10:24, 25.

Unaalikwa uungane na Baba yako wa kweli na ndugu na dada zako wa kweli. Furaha ambayo utapata inaweza kuwa kubwa kama furaha ambayo Cézar na maelfu ya watu huko Korea walipata walipoungana tena na familia zao.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Cézar mwenye umri wa miaka 19 akiwa na mama yake

[Picha katika ukurasa wa 10]

Chukua hatua za kumkaribia Mungu